SITTA AMEPUNGUKIWA SIFA SITA ZA UONGOZI
Watanzania tuna bahati kubwa maana kwa kupitia Bunge Maalum la Katiba angalao tumeweza kufahamu vema tabia ya Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba Samweli Sitta. Katika kutekeleza majukumu yake kwenye Bunge hilo Sitta amejibainisha wazi kuwa anapungukiwa sifa SITA alizotakiwa kuwa nazo kiongozi yeyote katika nchi yetu ikiwa ni pamoja na Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba. Sitta amepungukiwa sifa sita zifuatazo.
(1) Uwezeshaji wa maridhiano
Samweli Sitta ametudhihirishia kwamba hana ujuzi wala dhamira ya kujenga maridhiano pale watu wanapotofautiana. Tumeona wazi kuwa ameshindwa kujenga maridhiano miongoni wa wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba kama alivyofanya Jaji Joseph Sinde Warioba kwenye Tume ya Mabadiliko ya Katiba. Hii ni ishara kwamba Sitta akipewa uongozi wa nchi ataipasua nchi vipande vipande hata kama angeweza kuepuka kwa kujifunza kutoka kwa kiongozi aliyemtangulia. Kwa mfano angeweza kujifunza kutoka kwa kiongozi wetu mahiri na mzalendo wa ukweli, Jaji Joseph Sinde Warioba ambaye aliweza kujenga maridhiano miongozi wa wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba. Hakuna ubishi kwamba wajumbe wa Tume ya Warioba waliingia kwenye tume hiyo wakiwa vipande vipande maana walikuwa na itikadi tofauti za kisiasa, imani tofauti za dini na hata viwango tofauti vya uelewa wa masuala yanayohusu nchi yetu. Lakini wote waliweza kufanya kazi kubwa tena kwa wakati na iliyopokelewa kwa kishindo cha furaha na umma wa Watanzania. Tume iliweza kufanya kazi hiyo kwa sababu bila shaka Mwenyekiti wake hakuwa mbabe. Akijinyenyekeza akamsikiliza kila mjumbe na kujifunza kutoka kwao na hivyo akafanikiwa kujenga muafaka na ndipo tume ikaweza kujinyenyekeza kwa wananchi ili kusikiliza wananchi wanataka nchi yao iendeshwe vipi. Baada ya kukusanya maoni tume iliweza kuyachakata na kuandika Rasimu kwa maridhiano tena bila kupiga kura. Hivyo, tume iliweza kutoa mfano wa kuigwa kwa umma kwamba MARIDHIANO yanawezekana na yanaweza kujengwa katika kila hatua ya mchakato wa kuandika Katiba Mpya.
Lakini baada ya Rasimu kufikishwa katika Bunge Maalum la Katiba na Samweli Sitta kukabidhiwa kazi ya kuongoza Bunge hilo kuijadili na kuipitisha Rasimu hiyo, badala ya kuhakikisha kuna MARIDHIANO baina ya wajumbe yanakuwepo, tumeshuhudia akikumbatia ushabiki wa kivyama, ubabe na unafiki na mwishowe baadhi ya wajumbe wamesusia mchakato na wamekataa kurejea Bungeni. Tena anajinasibu kwamba Katiba itaandikwa hata kama baadhi ya wajumbe hawapo Bungeni. Lo! laiti angelijua kwamba kiongozi wa ukweli angeugua moyoni hata kama ni mjumbe mmoja tu ameudhika na kukataa kushiriki kazi hiyo muhimu maana Katiba ni MARIDHIANO au MUAFAKA wa Kitaifa. Laiti pengine hajui kuwa mbabe na mnafiki hawezi kuongoza timu ikafikia maridhiano. Anapaswa kujua kwamba hata mchunga kondoo wa ukweli ikitokea kondoo wake mmoja amebaki porini kitamuuma sana na atarudi porini kumtafuta hata kama kundi la kondoo wengine elfu moja litakuwa limerejea kwenye zizi.
(2) Ujasiri wa kutetea nchi na wananchi
Kupitia kazi muhimu aliyopewa ya kuongoza Bunge Maalum la Katiba tumeshuhudia jinsi anavyoweka mbele maslahi yake binafsi na ya chama chake badala ya maslahi ya wananchi na nchi yetu, TANZANIA. Mfano alivunja kanuni za Bunge Maalum la Katiba na kumpotosha Rais wetu kutoa maoni yake Bungeni badala ya kufanya kazi yake kama mkuu wa nchi ya kufungua Bunge hilo. Hapa Sitta alipaswa kuonyesha ujasiri kwa kumshauri Rais kufanya alichotakiwa kwa wakati husika. Kwa kutokuwa na ujasiri wa kumshauri Rais kwa upendo na ukweli ameweka wazi kwamba hana chembe ya ujasiri wa kutetea wananchi na nchi yetu. Amedhihirisha kwamba yeye anaweka mbele zaidi maslahi yake binafsi na dirisha lake analopitia kutafuta uongozi (chama chake cha siasa) naanasahau kwamba Tanzania ni kiubwa kuliko sisi sote.
(3) Kulinda maadili na utamaduni wa Mtanzania
Kwa kipindi chote alichoongoza Bunge Maalum la Katiba tumeshuhudia jinsi alivyokaa kimya huku baadhi ya wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba wakirushiana matusi ya nguoni. Aidha alikaa kimya pia hata pale baadhi ya wajumbe wa Bunge hilo walipomtukana, kumbeza na kumdhihaki Mwenyekiti wa Tume ya mabadiliko ya Katiba Jaji Joseph Sinde Warioba. Watu makini wanaamini kwamba waliomtukana na kumbeza Jaji Warioba waliwabeza na kuwatukana pia Watanzania wote, Tanzania na Rais wetu aliyeiteua tume hiyo kufanya kazi. Bunge Maalum la Katiba limeacha sifa mbaya sana kwa jamii kuwa viongozi wanawake na wanaume wanaweza kusimama hadharani na kuporomosha matusi ya nguoni. Lakini ni wazi kuwa kama Sitta angekuwa ni mtu anayejali na kuthamini maadili ya taifa letu, angalao angekemea wajumbe waliokuwa wanaporomosha matusi na hata ikibidi kuwachukulia hatua za kisheria.
4) Kuheshimu uhuru wa kujieleza
Tumeshuhudia Samweli Sitta akivinyooshea kidole vyombo vya habari hasa televisheni na redio za kitaifa kwa kutangaza midahalo kuhusu Rasimu ya Pili ya Katiba Mpya. Alijidhihirisha zaidi hasa pale Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilipotokeza hadharani kusahihisha upotoshaji mkubwa uliokuwa unafanywa kimkakati na wahafidhina wa mabadiliko kuhusu Rasimu ya Pili ya Katiba Mpya. Mtu huyu akipewa uongozi wa nchi siyo tu kwa kukosa uvumilivu katika kukuza demokrasia, ataweza kuvifungia vyombo vya habari ambavyo vitakuwa vinakosoa uwajibikaji wa serikali, bali pia hata kufuta usajili wa mashirika ya kijamii yatakayokosoa utendaji wa viongozi wa nchi na pengine hata vyama vya siasa vya upinzani. Kiongozi wa namna hii ni mtu hatari kwa amani na maendeleo ya nchi yetu.
(5) Kukubali mabadiliko.
Mtu yeyote ambaye anaogopa mabadiliko chanya ni mtu hatari maana bila mabadiliko ya kimfumo na kifikra nchi yetu haiwezi kupata maendeleo ya kweli kwa zama hizi mpya. Rasimu ya Pili ya Madadiliko ya Katiba kwa mujibu wa Jaji Warioba ikipitishwa italeta mabadiliko makubwa ya kimfumo na kiuongozi na hivyo maendeleo makubwa nchini. Lakini kwa jinsi Sitta alivyokimbilia kubadilisha kanuni za Bunge Maalum la Katiba katika awamu hii ya pili inadhihirisha wazi kuwa amedhamiria kabisa kukwamisha kwa makusudi mabadiliko chanya katika nchi yetu ambayo yangeletwa na Katiba Mpya iliyotokana na maoni ya wananchi. Hii inadhihirisha kwamba Sitta anakumbatia uafidhina na waafidhina wanaodhani kuwa wao ni wakubwa kuliko nchi yetu.
(6) Hana huruma kwa wananchi
Sitta anajuwa wazi kwamba Katiba Mpya itakayokubalika na kuheshimiwa na umma mpana wa wananchi haiwezi kupatikana bila maridhiano ya kitaifa. Lakini tumemuona aking'ang'ania Bunge Maalum la Katiba liendelee hata pale wajumbe kadhaa wa Bunge hilo akiwepo Naibu Waziri wa Fedha Mwingulu Mchemba alipoinuka kwa ujasiri akamshauri kwamba tathmini ifanyike kwanza kuona kama theluthi mbili inayotakiwa kupitisha vifungu vya Katiba hiyo inafikiwa. Endapo haifikiwi Bunge lisitishwe maana ni likiendelea ni sawa na kubariki kupoteza mabilioni ya fedha za kodi za wananchi ambao wanakabiliwa na hali duni ya maisha. Yeye Sitta kwa ubabe alishupaa na kusema theluthi inayotakiwa ipo na walioko nje watakuja tu.! Je kama ikibainika theluthi hiyo haipo na wasiokuwepo wasipokuja atalipa fedha za umma ambazo kila mjumbe wa Bunge hilo Maalum la Katiba anayehudhuria kikao cha sasa atakuwa ameweka mfukoni mwake zaidi ya shilingi milioni 25 ili hali wananchi wengi wakiwa hawana hata uwezo wa kula milo miwili kwa siku?
Hivyo, sisi wananchi tunapotafakari tunaona kwamba endapo nchi yetu itakuwa imekwama kupata Katiba Mpya iliyotokana na maoni ya wananchi, Mwenyekiti wa Bunge Maalum la katiba Samweli Sitta ndiye wa kubebeshwa lawama zote .
Send Emails to wanabidii@googlegroups.com
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Wanabidii" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com.
For more options, visit https://groups.google.com/d/optout.
0 Comments