[Mabadiliko] Kingunge Anaangalia Miaka 50 Nyuma, JK Anaangalia Miaka 50 Mbele !

Saturday, August 31, 2013


 Ndugu zangu,

Ndugu Kingunge Ngombale Mwiru ni mmoja wa wanasiasa ninaowaheshimu sana.  Nimemsikia Kingunge tangu nikiwa na miaka saba.

Lakini, kama ilivyokuwa kwa Mwalimu Nyerere, hakuwa malaika, Kingunge naye ni mwanadamu kama wengine. Si malaika.

Nimeyasikia mawazo ya Kingunge juu ya Serikali Tatu na hata Uraia wa Nchi Mbili. Kwa mtazamo wangu, Kingunge hayuko sahihi kwenye yote mawili.

Na hapa nitalizungumzia hili moja tu la mapendekezo ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba juu ya muundo wa Muungano wa Serikali Tatu.

Kimsingi haya ni mapendekezo yenye kutokana na maoni Wananchi. Hivyo, Tume imewasilisha tu. Si mapendekezo ya Jaji Warioba au wajumbe wake.

Hii ni tofauti kubwa na mazoea ya ' Ukale' ya Mzee Kingunge ambayo hata sasa anataka yafuatwe; kuwa jambo kubwa la muundo wa Muungano liachiwe Chama Cha Mapinduzi na vikao vyake.

Ni jambo jema kwa mwanadamu kujifunza kutokana na historia, lakini, si jambo jema kwa mwanadamu kuwa mtumwa wa historia. Ni bahati mbaya, kuwa Mzee wetu mpendwa, Kingunge Ngombare Mwiru, anataka tubaki kwenye utumwa wa historia. Hatutaki.

Na hakika Mzee Kingunge anapaswa kuelewa, kuwa nchi hii ni zaidi ya Chama cha Siasa. Na chama cha siasa kilicho madarakani hakiongozi mawe. Na  hata kama kingekuwa kinaongoza tumbiri, bado kingekumbwa na changamoto ya uwepo wa tumbiri wenye kutaka mabadiliko, kulingana na mahitaji ya wakati.

Tukubali, kuwa yalifanyika makosa makubwa ya kiuongozi huko nyuma. Ni pale masuala makubwa ya kitaifa kuachwa maamuzi yake kufanywa na kundi dogo la watu kwa kutumia nyadhifa za uongozi wa chama. Kwenye masuala makubwa ya nchi Chama kiliamua juu ya vichwa vya watu bila kushirikisha mawazo ya wananchi wenyewe, iwe kwa kupitia kura za maoni au kukusanya tu maoni ya makundi wakilishi. Huo ni msingi wa manung'uniko mengi ya sasa.

Kwangu mimi, Jakaya Kikwete ni mwanamageuzi wa kweli ambaye, kama kiongozi, ameonyesha ujasiri mkubwa wa kuzipa mgongo fikra za ukale na kuiangalia zaidi nchi na mustakabali wake kwa miaka mingi ijayo. Anafanya hivyo bila kujali nani au chama gani kitakuwa madarakani.

Wakati Mzee Kingunge na wahafidhina ( wasiotaka mabadiliko) wengine ndani ya mfumo uliopo  wanatoka mahandakini huku wakihaha kujaribu kuurudisha nyuma mshale wa mabadiliko chanya kwa jamii , Jakaya Kikwete anaonekana, kuwa sio tu  amesimama imara katika kuhakikisha mshale wa saa ya mabadiliko chanya kwa nchi unakwenda mbele, bali, unakwenda mbele kwa kasi.

 Ni imani yetu, Wananchi walio wengi, kuwa Jakaya Kikwete hatakatishwa tamaa wala kuyumbishwa katika kukamilisha ajenda yake njema ya mabadiliko chanya kwa jamii ya Watanzania kuelekea miaka 50 ijayo.

Mzee Kingunge aelewe pia, kuwa wakati umebadilika. Kuwa ya mwaka 1974 alipojiunga na TANU ni tofauti na ya sasa, mwaka 2013. Huu ni wakati wa kiongozi kuonyesha uwezo wa kusoma alama za nyakati. Hivyo, kujitahidi kuendana na mabadiliko ya nyakati.

Hiyo pia ndio tafsiri ya kuwa ' Kiongozi wa Kisasa na Kimaendeleo'- A modern and progressive leader. Jakaya Kikwete kwa sasa yumo kwenye kundi hilo.

Na wenzake ndani ya CCM wakimsaidia katika kazi yake, basi, ni fursa pia kwa Chama chao kuiteka tena  mioyo ya Wananchi wengi, mijini na vijijini. Maana, kati ya ambayo yanawachosha wananchi ni kukosekana kwa mawazo ya usasa na ya kimaendeleo kutoka kwa miongoni mwa viongozi wa CCM. Ni moja ya sababu ya chama hicho kupungukiwa na mvuto hususan kwenye kundi kubwa la vijana.

Na hakika, hata kama hatuoni leo, historia itakuja kumkumbuka Jakaya Kikwete kama mmoja wa viongozi Wana-Mageuzi ndani ya Chama chake CCM, na nchi kwa ujumla.

Maggid,

Iringa.

0754 678 252

http://mjengwablog.com

 

 

--
Unapokea Email hizi kwa sababu umejiunga na Jukwaa la 'Mabadiliko'.
Kuchangia mada tuma kwenye Email hii: mabadilikotanzania@googlegroups.com
 
Kujiondoa Tuma Email kwenda; mabadilikotanzania+unsubscribe@googlegroups.com
Utapokea Email ya kudhibitisha kujiondoa kwako.
 
TEMBELEA Facebook yetu:
http://www.facebook.com/MabadilikoForums?ref=hl
 
For more options, visit this group at:
http://groups.google.com/group/mabadilikotanzania?hl=en?hl=en
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Mabadiliko Forums" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to mabadilikotanzania+unsubscribe@googlegroups.com.
To post to this group, send email to mabadilikotanzania@googlegroups.com.
Visit this group at http://groups.google.com/group/mabadilikotanzania.
For more options, visit https://groups.google.com/groups/opt_out.

Share this :

Previous
Next Post »
0 Comments