Bunge lilitumia mamlaka yake kuchunguza na kulinda Katiba
· Wenye taswira ya kidekteta waliliandama Bunge
MWAKA 1992, Zanzibar ilijiunga kwa siri na Shirika la Kiislamu (OIC-
Organization of Islamic Conference) na taarifa hizo zilipovuja kwenye
vyombo vya habari, Bunge likaamua kuchunguza.
Uchunguzi ulilenga kubaini mambo matatu. Kwanza, kupata ukweli wa
jambo lenyewe kwa kuwa lilikuwa limejitokeza kwa njia ya vyombo vya
habari hususan magazeti. Pili, kubaini uhalali wa Zanzibar kujiunga na
Shirika hilo; na tatu, kujiridhisha kama kwa kufanya hivyo Zanzibar
haijakiuka Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Wakati Bunge lilipokuwa linaendelea na uchunguzi malalamiko
yalijitokeza kutoka Zanzibar na kwa baadhi ya viongozi wa dini ya
kiislamu upande wa Bara. Baadaye Zanzibar ilijitoa kwenye Shirika hilo
ambalo kwa sasa limebadili jina. Shirika hilo sasa linajulikana kama
OIC (Oragazation of Islamic Cooperation) na malengo yake pia
yamerekebishwa.
Tangu wakati huo, baadhi ya Waislamu na hata baadhi ya viongozi kutoka
Zanzibar wameendelea kunung'unika na kuitaka Serikali ya Jamhuri ya
Muungano ijiunge kwa madai kwamba kuna mambo ya kufaidika kimaendeleo
kwa Zanzibar na kwa Waislam wa Tanzania kwa ujumla.
Madai hayo yanasisitiza kwamba OIC ya sasa ni ya kimaendeleo zaidi
kuliko kidini. Kibaya zaidi kuna mwandishi mmoja, Said Mohammed katika
kitabu chake kiitwacho: Christian Hegemony and the Rise of Muslim
Militancy in Tanzania, sura ya nane, ameandika kwamba Bunge
lilichunguza Zanzibar kujiunga OIC kwa msukumo wa dini ya Kikristo na
kwamba wabunge Waislam hawakushiriki.
Huu ni upotoshaji wa hali halisi iliyokuwapo wakati huo. Na kama sisi
tuliokuwapo wakati huo tusipoweka mambo haya sawa upotoshaji huo
utachukuliwa kwamba ni ukweli.
Kwa kuwa mimi nilikuwepo bungeni na nilishiriki katika sakata hilo
kutoka mwanzo hadi mwisho nitatoa ufafanuzi wa jambo hili katika hatua
mbili.
Hatua ya kwanza nitachapisha taarifa ya ufafanuzi niliyoitoa mwaka
1993, bila kubadili neno, na katika hatua ya pili, nitajadili kwa
kifupi OIC ni nini na kugusia madai kwamba Serikali ya Tanzania
iliahidi kujiunga na OIC na kwamba ijiunge sasa.
Wengine wanakwenda mbali zaidi na kutaka suala la OIC liingizwe kwenye
katiba mpya. Kwa kuwa Tanzania ni mwanachama wa mashirika mengi tu ya
kimataifa sijui OIC itaingizwaje kwenye Katiba mpya! Ifuatayo ni
taarifa ya ufafanuzi kama ilivyochapishwa katika gazeti la Mwananchi
Aprili 19—25, 1993:
Bunge lina haki ya kuchunguza suala la OIC
KIKAO cha Bunge kilichofanyika Februari 1993, mjini Dodoma, kilijadili
pamoja na mambo mengine taarifa ya Marmo (Philip) iliyochunguza
uhalali wa Zanzibar kama sehemu ya Jamhuri ya Muungano, kujiunga na
Shirika la Nchi za Kiislamu (OIC).
Suala la Zanzibar kujiunga na OIC, shirika ambalo wanachama wake ni
mataifa kamili wakati Zanzibar ni sehemu tu ya Taifa la Tanzania
limezusha mgogoro wa kikatiba na kusababisha mjadala mkali bungeni.
Pia lilizusha hisia tofauti baina ya Wantanzania na hata wengine
wakadhani kuwa Bunge linahoji suala hili kwa vile Zanzibar imejiunga
na Shirika la Kiislam na si vinginevyo.
Ukweli ni kwamba Kamati ya Katiba na Sheria ilichunguza suala la
uanachama wa Zanzibar katika OIC kwa misingi ya kikatiba. Hapa pia
ningependa kuwaelewesha Watanzania kuwa Kamati ya Katiba na Sheria ni
moja ya kamati za kudumu za Bunge na wala haikuundwa na Naibu Spika,
Mheshimiwa Pius Msekwa kwa madhumuni ya kuchunguza uanachama wa
Zanzibar katika OIC kama vile ambavyo baadhi ya watu wangependa
ieleweke.
Mimi ni mmoja kati ya wabunge saba waliowasilisha waraka kwa Naibu
Spika kumwomba akabidhi kwa Kamati ya Katiba na Sheria suala la
uanachama wa Zanzibar ili lichunguzwe kuona kama kwa kufanya hivyo
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haikukiukwa.
Pia tuliomba kamati ichunguze tuhuma kuwa Tanzania ilikuwa mwanachama
wa siri wa Shirika la Kiislam la Afrika (Islam in Africa Organization-
IAO).
Wengi wameuliza kwa nini sisi wabunge saba tulifikia uamuzi wa kutaka
masuala haya mawili yachunguzwe na Kamati ya Bunge. Ikumbukwe kwamba
mwanzoni mwa mwezi Desemba 1992, Shirika la Utangazaji la Uingereza
(BBC) lilitangaza kwamba Zanzibar ilikuwa imejiunga na OIC.
Mbunge wa Kibondo, Bw. Arcado Ntagazwa alilizungumzia suala hilo
bungeni lakini serikali ilikaa kimya. Baadaye gazeti moja liliandika
kuwa ni kweli Zanzibar ni mwanachama wa OIC.
Baada ya gazeti hilo kuchapisha hivyo ndipo aliyekuwa Waziri wa Mambo
ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. Ahmed Hassan Diria,
alipokanusha na kusema kwamba kama Zanzibar imefanya hivyo imekiuka
Katiba ya Jamhuri ya Muungano.
Kwa mara nyingine tena gazeti hilo katika toleo la kwanza la mwezi
Januari 1993 lilichapisha habari kuwa Tanzania ilikuwa mwanachama wa
siri wa Shirika la Kiislam la Afrika (IAO). Gazeti hilo pia
lilichapisha maazimio ambayo yalidaiwa yalipitishwa na kikao cha
mwanzo cha IAO mjini Abuja, Nigeria, maazimio ambayo kwa Watanzania
wengi yalionekana kuwa ya kutisha kwa usalama na utangamano wa jamii
ya Kitanzania.
Katika kipindi hicho hicho gazeti lingine lilichapisha makala ambayo
yalionyesha kwamba ni kweli Zanzibar ilikuwa imejiunga na OIC licha ya
Waziri Diria kukanusha. Mpaka wakati huo, mbali ya taarifa ya Waziri
Diria hakuna taarifa nyingine iliyotolewa na ama Serikali ya Zanzibar
au Serikali ya Muungano kukanusha au kuthibitisha madai ya magazeti
hayo mawili.
Lakini mnamo Januari 9, 1993 taarifa ilitolewa na Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar kuthibitisha uanachama wake katika OIC. Katika
taarifa hiyo ilionekana wazi kuwa Serikali ya Muungano ilikuwa na
habari na suala la Zanzibar na OIC.
Matukio haya yalizua mambo matatu. Kwanza ni kutaka kujua kama kweli
Zanzibar kujiunga na OIC ni kinyume na Katiba hasa kwa kuzingatia
maadili ya siasa za Tanzania tangu uhuru na Katiba ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania inayosema kuwa shughuli zote za dini zitafanywa
nje ya mamlaka ya nchi.
Pili madai kuwa Tanzania ilikuwa mwanachama wa siri wa IAO na
kuzingatia maazimio yaliyodaiwa kuwa ni ya IAO, wananchi wengi
waliingiwa na hofu na kuzusha minong'ono katika sehemu mbalimbali za
nchi yetu. Tatu, ilionekana kuwa kuhusika kwa nchi yetu katika
mashirika hayo mawili kulikuwa kwa siri na hivyo kuzusha hisia kwamba
huenda malengo na madhumuni yake hayakuwa mazuri.
Mimi nikiwa mbunge nilipoyapata haya yote sikujua lipi ni la kweli na
lipi si la kweli. Nilishindwa kujua kama taarifa ya Waziri Diria
ilikuwa sahihi au taarifa kutoka Zanzibar ndiyo iliyokuwa sahihi. Mimi
kama Watanzania wengi walivyokuwa wakati huo, sikujua kama IAO ipo au
haipo na kama maazimio yaliyotajwa ni ya kweli au si ya kweli.
Watanzania wengi walijikuta katika hali hiyo na kitu ambacho
kingeondoa tatizo hili katika mawazo yao ingekuwa ni taarifa ya
Serikali ya Muungano wa Tanzania. Nikiwa mbunge na kiongozi, nilikuwa
na njia mbili za kufuata. Moja ni kujiunga na vikundi
vinavyonung'unika na hivyo kuwa mmojawapo wa wapika majungu na kueneza
fikra potofu zisizo na msingi.
Pili, kufuata taratibu zilizopo ili kupata ukweli wa mambo ulivyo na
kuwaondoa wasiwasi wananchi.
Kama mbunge taratibu ninazoweza kufuata ni za kibunge, sina njia
nyingine. Mbunge akitaka kupata ukweli wa jambo lolote zito
lililotendwa na serikali hana budi kutumia Bunge lenyewe ambalo lina
uhalali wa kikatiba kupata majibu sahihi kutoka serikalini. Lazima
ikumbukwe kwamba kwa muundo wake serikali ni chombo kizito, chenye
maguvu na usiri mwingi katika utendaji wake wa kazi.
Serikali haina msimamizi isipokuwa watu wenyewe kupitia wawakilishi
wao bungeni. Bunge ndicho chombo pekee cha wananchi kilichopewa
madaraka na Katiba ya Nchi kuisimamia, kuihoji na inapobidi,
kuichunguza na hata kuiwajibisha serikali katika vitendo vyake.
Zanzibar kujiunga na OIC na tuhuma kwamba Serikali ya Tanzania ni
mwanachama wa IAO, vilidaiwa kutendwa na serikali na kwa hiyo chombo
halali cha kulichunguza na kuhoji suala hili ni Bunge.
Kwa misingi iliyoelezwa hapo juu mimi sikubaliani na wale wote
wanaodai kuwa Bunge la Tanzania halina haki ya kuchunguza suala la
uanachama wa Zanzibar katika OIC,wala tuhuma kwamba Tanzania ni
mwanachama wa siri wa IAO. Ninaamini hatua zilizochukuliwa na Bunge
zilikuwa halali na haki, sahihi na zenye manufaa kwa taifa hili hasa
ukitilia maanani jinsi masuala hayo mawili yalivyozusha hisia tofauti
baina ya Watanzania.
Hoja kwamba Bunge halina uwezo wa kuhoji wala kuchunguza masuala ya
kikatiba yanayohusu Muungano na yale yanayohusu uanachama wa Zanzibar
katika OIC ni potofu na haiwezi kukubaliwa. Wananchi lazima waikatae
hoja hiyo kwa sababu ina malengo ambayo si mazuri.
Katika nchi ya kidemokrasia serikali huwekwa madarakani na watu, na
watu ndio ambao huisimamia serikali hiyo kupitia Bunge. Madaraka ya
watu juu ya serikali hujitokeza katika sura mbili. Sura ya kwanza ni
wakati wa kupiga kura kumchagua Rais na wabunge, na sura ya pili ni
madaraka wanayokuwa nayo wabunge kwa niaba ya watu juu ya serikali
kati ya vipindi vya uchaguzi.
Bunge ndiyo kielelezo cha madaraka ya watu ndani ya nchi yao kwa
masuala yote yanayowahusu.
Kwa hiyo kiongozi yeyote anayelikataa Bunge maana yake anakataa
madaraka ya watu juu ya serikali yao. Kiongozi kama huyo anataka
kutawala bila kuwepo na chombo cha kumhoji anapopotoka. Kwa kifupi
kiongozi kama huyo anataka kuleta udikteta jambo ambalo Watanzania
lazima walikatae.
Kuhusu matamshi kutoka viongozi wa Zanzibar kwamba Bunge halina uwezo
wa kutamka kuwa Zanzibar imekosea katika jambo fulani na kwamba si
chombo chenye uwezo wa kutamka hivyo, usemi huu si kweli. Bunge lina
madaraka na uwezo juu ya Zanzibar katika masuala yote ambayo ni ya
Muungano, na ndio maana wabunge wake wanatoka pande zote mbili za
Muungano.
Kuwepo kwa wabunge wa Zanzibar katika Bunge la Muungano kunalipa
uhalali Bunge kushughulikia masuala yote ya Muungano popote Tanzania.
Zanzibar kujiunga na OIC ni suala la kikatiba na masuala ya Katiba ni
masuala ya Muungano. Kwa hiyo, Bunge kujishughulisha na suala la
uhalali wa Zanzibar kujiunga na OIC si nje ya madaraka yake. Unaposema
Bunge halina uwezo juu ya Zanzibar hata katika mambo ya Muungano ina
maana kuwa Muungano haupo, jambo ambalo si kweli – kisheria (dejure).
Mahakama ya Katiba inahusika pale inapotokea mgogoro wa tafsiri wa
vipengele vya Katiba baina ya pande mbili za Muungano. Kwa mfano,
Zanzibar walipoomba kutoka Serikali ya Muungano ruhusa ya kujiunga na
OIC, wangesubiri kupata jibu.
Kama Serikali ya Muungano ingewakataza kwa kutumia vipengele vya
Katiba ambavyo Zanzibar wanafikiri haviwazuii kufanya hivyo, basi
mgogoro wa kikatiba ungelikuwa umezuka na Mahakama ya Katiba ingeombwa
kutoa tafsiri sahihi ya vipengele hivyo. Na Katiba hiyo lazima iwe
Katiba ya Jamhuri ya Muungano, siyo ile ya Zanzibar.
Kuwepo kwa Mahakama ya Katiba kushughulikia tofauti za tafsiri ya
vipengele vya Katiba kati ya Bara na Zanzibar hakulizuii Bunge
kushughulikia ukiukwaji mwingine wowote wa Katiba unaoweza kufanywa na
Serikali ya Muungano au ya Zanzibar. Ni vizuri Bunge likashughulikia
suala la kulinda Katiba, vinginevyo tutakuwa na Katiba ambayo
inafuatwa tu pale inapokubaliana na matakwa ya viongozi na kukiukwa
pale inapowazuia kutekeleza matakwa yao.
Jambo jingine ambalo limeulizwa na baadhi ya wananchi na ambalo
ningependa kutoa maelezo ni lile linalouliza kwamba ilikuaje Naibu
Spika kuwapata haraka haraka wabunge saba kuja Dare es Salaam kutia
saini waraka uliofikishwa kwake wakati Bunge lilikuwa halikutani?
Ukweli ni kwamba hakuna mbunge aliyeitwa na Naibu Spika (Pius Msekwa)
kuja Dar es Salaam kushughulikia suala hili. Wabunge wote saba
walikuwepo Dar es Salaam kuhudhuria mikutano ya kamati mbalimbali za
Bunge. Na zaidi ya hayo Naibu Spika hakututaka tuandike bali
tuliandika kwa kujituma wenyewe.
Bado kuna baadhi ya wananchi ambao waliuliza kwa nini mara baada tu ya
kuwasilisha waraka wetu kwa Naibu Spika tukatangaza suala hili kwa
waandishi wa habari. Kuna sababu tatu za msingi ambazo zilitufanya
tutangaze hatua tulizochukua. Kwanza, mbunge ni mwakilishi wa watu na
hivyo yote anayoyafanya kwa wadhifa wake kama mbunge lazima yajulikane
kwa wananchi anao wawakilisha.
Pili, suala la uanachama wa Zanzibar katika OIC na tuhuma kwamba
Tanzania ni mwanachama wa IAO yaliwagusa watu wengi na wote katika
kipindi hicho walisubiri kuona hatua gani inachukuliwa na nani. Kwa
hiyo tulipenda kuwajulisha wananchi kwamba Bunge lao lilikuwa
linachukua hatua za kupata ukweli wa mambo hayo.
Tatu, hatua ya kutaka uchunguzi ufanywe juu ya masuala hayo mawili
ilichukuliwa na wabunge saba na tukaomba matokeo ya uchunguzi huo
yafikishwe bungeni Dodoma katika kikao cha Februari, 1993. Kwa
kulitangaza jambo hili tulikusudia liwafikie wabunge wote popote
walipokuwepo ili wajiandae na hata kufanya mawasiliano na wananchi
wanaowawakilisha kabla ya kufika Dodoma.
Kabla ya kumaliza maelezo haya nataka nigusie kidogo hisia
zilizojitokeza kuonyesha kwamba uchunguzi wa masuala ya OIC na IAO
ulianzishwa kwa vile tu mambo hayo yana uhusiano na dini ya Kiislam.
Hapa ningependa kuwahahakishia waumini wa dini hiyo na Waanzania wote
kwa ujumla kwamba sisi wabunge saba katika kuomba uchunguzi ufanywe
katika masuala haya mawili hatukuwa na nia yoyote mbaya na dini ya
Kiislam. Hatukuwa na chuki wala uhasama wa aina yoyote ile.
Madhumuni yetu ilikuwa ni kupata ukweli wa mambo hayo na kuona kama
Katiba ya nchi haikuwa imekiukwa. Mimi (nina amini na wenzangu wana
msimamo kama huo), siwezi kutumia wadhifa wangu kukandamiza au
kupendelea dini moja dhidi ya dini nyingine.
Msimamo wangu ni kuyaacha masuala ya dini kwa wale wanaoamini na wala
serikali isijiingize katika kuendeleza imani ya dini moja dhidi ya
imani nyingine. Ingawa katika gazeti moja la Januari 21, 1993
nilitajwa kuwa mimi ni mchungaji wa kanisa, nataka kutumia nafasi hii
kukanusha kwamba mimi si mchungaji wala padre wa kanisa.
Katika maisha yangu mimi sijawahi kushika wadhifa wowote katika kanisa
wala katika dini nyingine yoyote. Aliyenitangaza kwamba mimi ni
mchungaji alifanya hivyo kwa madhumuni yake binafsi.
Endelea Kuhabarika
Zanzibar: Kwa kujitangaza nchi, imekiuka katiba ya Muungano?
Makala/Source: Gazeti la Raia Mwema
--
Jobs in Africa - www.wejobs.blogspot.com
International Jobs - www.jobsunited.blogspot.com
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Wanabidii" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com.
For more options, visit https://groups.google.com/groups/opt_out.
0 Comments