Habari hii ilichapishwa kwenye gazeti la RAI miaka michache iliyopita ikisomeka...
Huyu Ndiye Pombe Magufuli:
- Wasema nyumba 8,000 kauza kwa mkono wake mwenyewe
- Apuuza maonyo ya wataalamu- Mafaili ya Sundi na Musa aliyabeba kwapani
ALIYEKUWA Waziri wa Ujenzi, John Magufuli, katika Serikali ya awamu ya tatu, aliteka madaraka na kuwa mwenyekiti wa zoezi la kuuza nyumba za serikali ambazo hadi sasa, zimeshauzwa 8,288 imefahamika.
Habari zilizopatikana ndani ya wakala wa Majengo ya Serikali (TBA), zimethibitishia Rai wiki hii kwamba Magufuli alihakikisha anashiriki kama Mwenyekiti katika zoezi zima la kuuza nyumba, ambalo kimsingi lilistahili kusimamiwa na Mtendaji Mkuu wa TBA.
Kwa mujibu wa vyanzo kadhaa vya habari ndani ya TBA, Magufuli alifanya kila aina ya 'fujo' katika zoezi la kuuza nyumba hizo, wakati mwingine akibatilisha maamuzi yaliyofanywa na Kamati ya TBA ya kuuza nyumba hizo, akiwapangia watu nyumba kwa utashi wake na wakati mwingine akiwakemea wale wote waliomshauri kinyume na matakwa.
Ni chini ya utaratibu huo, habari zinaeleza kwamba Magufuli, aliyabeba yeye mwenyewe mafaili ya ndugu zake; Musa Magufuli ambaye ni mdogo wake, na Sundi Malomo ambaye ni mzazi mwenzake na kuwalazimisha watendaji wa TBA wafuate matakwa yake katika kuwapatia nyumba ndugu zake hao.
Habari hizo zinaeleza kwamba awali Mtendaji Mkuu wa TBA alimshauri Magufuli kwamba suala la mauzo ya nyumba kwa ndugu zake ni kinyume cha utaratibu. Hata hivyo, imeelezwa kwamba Magufuli alilazimisha huku akisema mdogo wake hana tatizo kwa sababu alikuwa tayari mfanyakazi wa Serikali.
Musa aliajiriwa kwa mkataba wa miezi mitatu, baada ya mwezi mmoja akauziwa nyumba na baada ya miezi miwili akaacha kazi.
"Kwa upande wa Sundi, kwanza ilikuwa Sundi auziwe nyumba moja kwa moja. Lakini Magufuli alipoonywa akashtuka na kusema suala hilo aachiwe yeye mwenyewe. Na ndipo akaibuka na jina la Stanley Manongi kwamba ndiye mnunuzi halisi na baba yake Sundi," vinasema vyanzo hivyo vya habari, vingine ambavyo vilishiriki moja kwa moja katika mchakato wa uuzaji nyumba hizo.
Habari hizo zinaendelea kueleza kwamba baadaye, Sundi alishtuka akitilia shaka uaminifu wa Manongi, kwamba angeweza kumdhulumu nyumba hiyo.
"Ndipo Magufuli aliibuka na mpango wa Sundi kuwa mtoto wa Manongi na mrithi wake na kisha kwa kuhakikisha kwamba hakuna dhuluma yoyote, mtoto wa Sundi naye akarithishwa na kama mrithi wa pili," chanzo hicho cha habari kinaeleza.
Chini ya sheria ya Executive Agency Act No. 30 ya mwaka 1997, TBA ilipewa madaraka yote ya kuuza nyumba za Serikali, kujenga nyumba mpya, kuzikarabati zilizopo pamoja na kugawa nyumba za madaraja A, B na C kwa wafanyakazi wa Serikali.
Sheria hiyo inaipa mamlaka ya kipekee ya kufanya shughuli zote bila kuingiliwa na chombo chochote.
Chini ya sheria hiyo, Waziri anaruhusiwa kuteua wajumbe wa bodi ya ushauri watakaomshauri Katibu Mkuu wa Wizara juu ya namna nzuri ya TBA kusimamia mamlaka yake.
Hadi Machi mwaka huu, wajumbe hao walikuwa ni J. Kijazi, E. Lipambila, E. Lugwisha, Msangi, E. Mwakalinga, D. Kisasi, P. Ncheye, F. Werema na A. Bukuku.
Hata hivyo, sheria haitoi nafasi yoyote kwa Waziri kusimamia shughuli za uuzwaji au upangaji wa nyumba za serikali.
Mtendaji Mkuu wa TBA Togolayi Makumba Kimweri, alipoulizwa kupitia kwa Katibu Muhtasi wake, alimwambia mwandishi wa Rai aandike maswali kisha asubiri kuruhusiwa kuingia ndani ya ofisi.
Hata hivyo, baada ya kusubiri kwa muda wa saa moja, mwandishi alipokwenda kuuliza akaambiwa kwamba Kimweri tayari alikwishaondoka ofisini kupitia mlango wa nyuma na asingeweza kurudi ofisini.
Lakini baadhi ya wafanyakazi wa TBA wameiambia Rai kwamba kinachoandikwa kwenye magazeti kuhusu ushiriki wa Magufuli kuuza nyumba za Serikali ni kidogo mno kuliko hali halisi.
Kama ilivyokuwa kwa mdogo wake Musa, waziri Magufuli alishinikiza mtoto wa dada yake anayeitwa James Doto Mgosha auziwe nyumba za serikali kwa kumtengenezea ajira ya muda mfupi katika TANROADS.
Tofauti na Musa, Doto ameuziwa nyumba hiyo kwa jina la mtu mwingine lakini anaishi katika nyumba hiyo, namba 64 iliyopo Kinondoni Flats.
Habari kutoka TBA zinaonyesha jina la mtu mwingine (tunalihifadhi) kuwa ndiye aliyeuziwa nyumba hiyo mtu huyo alipata kupitia utaratibu wa Magufuli kupeleka jina lake kwenye wakala wa majengo na kulazimisha apewe nyumba.
Alipoulizwa kwa njia ya simu, Doto alisema suala la ajira na nyumba waulizwe waliomwajiri na kumpa nyumba. Akakata simu.
Mfanyakazi mwingine alieleza Rai kwamba msichana mwingine (jina tunalihifadhi) akiwa na miezi minne tu kazini alipelekwa na Magufuli katika Wakala wa Majengo akilazimisha auziwe nyumba hata kabla ya kuthibitishwa kazini. Nyumba hiyo iko Block A, Ocean Road.
Hata hivyo, habari hizo zinaeleza kwamba msichana huyo ambaye hadi sasa anaishi na wazazi wake, ameipangisha nyumba hiyo kwa mfanyakazi mmoja wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa na analipwa kwa dola za kimarekani.
"Kuuza nyumba za serikali sawa, lakini kweli katika mtindo huu? Sisi tunaoshiriki kuzikagua na kuziratibu tukiomba hatupati, lakini wengine wanaingia serikalini miezi miwili wanapata nyumba. Na wengine hata si wafanyakazi, wanapata, hii si sahihi, alilalamika mfanyakazi mmoja aliyeandikia Rai kwa njia ya barua pepe.
Hadi Machi mwaka huu Wakala wa Majengo wa Serikali (TBA) walishauza nyumba 8,288 ambazo hata hivyo zilitakiwa kuuzwa kwa watumishi wa serikali.
Katika mauzo hayo, Serikali ilitarajia kupata jumla ya shilingi 60,016,556,439.00. Hata hivyo hadi sasa Serikali imepata shilingi 22,684,108,115.08.
Kwa sasa, Serikali imebakiwa na nyumba 1,098 zinazosimamiwa na TBA. Kati ya hizo, nyumba 692 zimetengwa kwa wafanyakazi wa Serikali, nyumba 675 kama tied quarters, nyumba 111 zinatumika kama Rest House za Serikali, wakati nyumba 40 zinatumika kama state lodges. Nyumba 24 zinatumika kama ofisi na nyingine 29 ni kama karakana na bohari.
SALVA RWEYEMAMU
RAI
Recent
Since February 1st, 2014
9960220
Send Emails to wanabidii@googlegroups.com
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Wanabidii" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com.
For more options, visit https://groups.google.com/d/optout.
0 Comments