[wanabidii] Lowassa, Dk. Slaa, tusipotoshe ukweli

Thursday, September 10, 2015

Privatus Karugendo

MSEMA kweli ni mpenzi wa Mungu. Hivyo tunapojikuta kwenye wakati mgumu kama taifa, tunapoanza kuchanganyikiwa na kupotea njia, ni lazima tukumbuke kwamba ukweli utatuweka huru. Tusipotoshe ukweli na kuwapotosha watu. Edward Lowassa, anataka madaraka kwa gharama yoyote ile, anataka kuwa Rais wa Tanzania kwa njia yoyote ile.

Amekatwa kwenye chama chake, CCM, akakimbilia Chadema - Ukawa. Hakuwa mpenzi wa Ukawa na wala hakuwa mtetezi wa Ukawa, alikuwa mwiba wa upinzani. Amekumbatia Ukawa kama njia ya kupita kutimiza kiu yake ya kutaka kuwa Rais. Huu ndiyo ukweli, tuukubali na tusiupotoshe. Dk. Slaa, anaeleza sababu zake za kutomuunga mkono Lowassa kushika nafasi ya urais wa Tanzania. Si chuki binafsi na wala si kwa vile yeye hakupata nafasi ya kugombea nafasi hii, alisema juzi, jana na leo anasema hivyo na kesho atasema hivyo, kwamba Lowassa hana maadili ya uongozi. Huu ndio ukweli, tuukubali na tusiupotoshe.

Wanaosema Dk. Slaa, ni mtakatifu wamesema wenyewe, yeye hajasema hivyo. Na wala hoja yake si utakatifu na wenye dhambi. Hoja yake ni uadilifu wa uongozi katika taifa letu. Hoja yake ni mtu kusema ukweli ukausimamia, hoja yake ni mtu kusimamia rasilimali za taifa letu. Kuwatumikia watu, kudumisha amani na usawa katika taifa letu. Kuondoa umasikini na kuleta maendeleo.

Tumemsikia Dk. Slaa, kwa makini Mtu aliye makini ni lazima alielewa maelezo yake. Ingawa ilishangaza kabisa kwamba baada ya mahojiano yake na waandishi wa habari, waandishi wote waliouliza maswali, walionyesha kutoelewa. Tunajiuliza kama huo ndio uelewa wa waandishi wetu wa Tanzania, au waandishi hao walikuwa wamepangwa kwa malengo maalumu? Huko nyuma Rais (mstaafu) Benjamin Mkapa, alisema waandishi wa Tanzania si makini, wakalalama kwamba aliwatukana! Huo ndo ukweli tusiupotoshe!

Kama waandishi hao walipangwa, basi ni upotoshaji na hizi ni dalili za kudidimiza uandishi wa habari hapa Tanzania. Waandishi watanunuliwa na kuelekezwa ya kuandika. Hii ni hatari kubwa. Lazima kupiga vita utamaduni huu kwa nguvu zote. Kama waandishi, ambao tunaamini ni wasomi, hawawezi kusikiliza na kuelewa, itakuwa vipi kwa watu wa kawaida kule vijijini? Mwandishi ambaye hakuelewa yale aliyoyasikia, ataandika nini na atawaelimisha wananchi wa vijijini na wale wanaosoma magazeti.

Dk Slaa, alimshambulia Lowassa kwa mwenendo wake juu ya maadili ya uongozi, juu ya ufisadi na tabia yake ya uongo juu ya mambo ya kuliongoza taifa letu. Hakusema chochote kuhusu maisha ya ndoa ya Lowassa na wala juu ya maisha binafsi ya Lowassa. Tunaamini Dk, Slaa kwa kiasi fulani anayafahamu maisha binafsi ya Lowassa, lakini kwa vile hoja ya msingi si maisha binafsi, yeye hakugusia jambo hili.

Sasa tumeanza kusikia upotoshaji juu ya maisha ya Dk. Slaa. Juu ya ndoa yake na maisha yake ya ukasisi. Huku ni kupotosha hoja kwa malengo fulani. Suala la msingi si maisha ya familia ya Dk Slaa. Suala la msingi ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Na Dk Slaa katika hoja yake aliweka wazi jambo hili na kulitetea kwa mifano na nyaraka. Hatuongelei familia na maisha ya ndoa, hatuongelei uaminifu katika ndoa, bali ni uongozi wa taifa na uaminifu juu ya rasilimali za taifa, maana kufuatana na Katiba yetu ya sasa Rais, ana mamlaka makubwa sana. Anaweza kuamua mambo mengi au ya kuliponya taifa au ya kuliangamiza. Ni muhimu tukafahamu ni mtu aina gani anataka kutuongoza. Si kuiongoza familia yake, bali kuliongoza taifa. Si kuwa mwaminifu kwa mke wake, bali kuwa mwaminifu kwa Katiba na taifa zima la Tanzania.

Maisha ya Dk. Slaa, kwenye ukasisi Maisha yake kwenye ndoa zake mbili, hayana uhusiano wa moja kwa moja na uongozi wa taifa letu au kazi yake aliyoifanya kwenye ubunge na kwenye wadhifa wa Katibu Mkuu wa Chadema. Katiba yetu, haisemi kwamba Rais awe ameoa, awe mwaminifu kwa mke wake. Haya ni maadili mazuri ambayo kila mtu ni muhimu awe nayo, lakini si masharti ya kumzuia mtu kuwa kiongozi wa taifa letu.

Dk. Slaa aliungama wazi kushiriki hatua za mwanzo za kumshawishi Lowassa kuingia Ukawa, lakini aliweka masharti ambayo si lazima sana kuyarudia kwenye makala hii. Tuliambiwa kwamba masharti hayo hayakufuatwa. Na Lowassa, akakaribishwa kujiunga na Ukawa- Chadema, bila masharti hayo kufuatwa. Hivyo wale wote wanaotetea jambo hili, tunawataka walieleze hili na wala si kukimbila kwenye maisha binafsi ya Dk. Slaa.

Tunamheshimu sana Freeman Mbowe, na sote tunafahamu juhudi zake za kukijenga chama chake, Chadema. Sote tumeshuhudia kwamba wakati wa uongozi wake chama hiki kimepiga hatua na kushika nafasi ya chama kikuu cha upinzani bungeni. Hii ni hatua kubwa na hakuna wa kuipuuza. Busara na hekima ambazo amekuwa akionyesha siku za nyuma, tulitarajia kuziona wakati huu. Hata kama ameamua kumkumbatia Lowassa, kwa dalili zake za kukipaisha chama na labda kuishika dola, tulitaraji atende haki kwa Dk. Slaa. Tunashangaa kuona hata yeye anakubali upotoshwaji unaofanywa dhidi ya Dk. Slaa. Kama kuna mtu anafahamu vizuri kabisa kwamba Dk. Slaa, hanunuliki ni Mbowe. Tunataka tusikie haya kutoka kwake na wala si hizi porojo za kununuliwa na maisha binafsi ya Dk. Slaa.

Ni wazi jinsi Chadema, inavyoendelea sasa hivi, jinsi watu wanavyovutiwa na kampeni zao, na umati mkubwa wa watu unaojitokeza kwenye mikutano yao, wanaelekea kukamata dola, hivyo wasingependa mtu kuingilia katikati na kubomoa nguvu zenye kuleta matumaini kwa upande wao. Ila wakumbuke kwamba, bila kulenga yale yale, kwa nia ya kuiondoa CCM na kuleta mabadiliko, wengine wakilenga kupata madaraka na kufurahia kuwamo madarakani, hakuna jipya litakalotokea. Si leo, na wala si kesho wakati ukifika. Mabadiliko, yanahitaji sadaka, mabadiliko yanahitaji kujitoa na kukubali kuto kukubaliana.

Tunamheshimu sana James Mbatia. Watanzania wengi wamejenga imani juu yake. Tunaamini ni mtu anayelipenda taifa letu. Hivyo hatukutarajia naye katika suala hili la Dk. Slaa na Lowassa, awe na ushabiki. Anaweza kuwa na matumaini kwa Lowassa, na hasa matumaini ya kushika dola, lakini amtendee haki Dk. Slaa.

Suala la ndoa ya Dk. Slaa na maisha yake binafsi vinajitokeza kwa nguvu, kana kwamba tunaongelea maisha ya ndoa. Kujitokeza kwa mke wake wa zamani kwenye vyombo vya habari ni jambo ambalo limetuletea mashaka. Kwa nini ajitokeze leo hii wakati wameachana na Dk. Slaa, miaka mingi ya nyuma?

Tunaamini, pale Dk. Slaa, aliposema familia yake ilikuwa inashindia mihogo, alikuwa akimaanisha familia yake na mke wake wa pili, Josephine Mushumbusi. Alisema hayo, baada ya kuelezea kwamba mke wake huyo alikuwa akitumia mshahara wake kuzunguka nchi nzima akijenga umoja wa wanawake wa Chadema. Kwa vile alitumia mshahara wake, yeye na watoto walishindia mihogo. Hakumaanisha mke wake wa kwanza ambaye amejitokeza kwenye vyombo vya habari.

Lengo ni kupotosha hoja za Dk Slaa, ambazo ni nzito na ni muhimu kwa kila Mtanzania kuzitafakari. Kama Chadema, walimshutumu Lowassa kuwa fisadi, amejisafisha kwa sabuni gani leo hii? Na je Chadema, wataendeleza vita yao kupinga ufisadi? Watanzania wanataka mabadiliko, je mabadiliko haya yanaletwa na wale wale, wenye mawazo yale yale na mfumo ule ule? Inawezekana CCM, wakatumia hoja ya Dk. Slaa, kujijenga. Si lazima Dk. Slaa, kuwa amelenga huko. Lakini wakiweza, maana ni mpaka mtu msafi, mtu mwenye maadili ya uongozi kusimama, bila kuogopa kusemwa au kukumbushwa ubovu wake, akatumia hoja ya Dk. Slaa kuisaidia CCM.

Wengi wanaamini Dk. Magufuli, ana ubavu wa kusimama na kuzungumza bila kuogopa. Labda huyu anaweza kuibeba hoja ya Dk. Slaa. Hili likitokea, Chadema wajilaumu wenyewe na wala wasimnyoshee kidole Dk. Slaa. Jambo la msingi hapa ni kukubali ukweli kwa yale yaliyotokea kati ya Lowassa na Dk. Slaa.Tusipotoshe ukweli. Tukubali ukweli utuweke huru.

Chanzo Raia Mwema

Share this :

Related Posts

0 Comments