[wanabidii] Matokeo ya utafiti kuhusu "Mtazamo wa Wananchi kuhusu ushiriki wa vijana katika siasa na matarajio kuelekea Uchaguzi Mkuu 2015"

Monday, February 09, 2015
Utangulizi
Nimeshuhudia miaka ya 1985 hadi 1995 ambapo mimi mtafiti1 wa kazi hii; nikiwa na uelewa kwa kiasi fulani, kuona watu waliokuja kugombea nyadhifa mbali mbali za kisiasa, hususani ubunge walikuwa watumishi wa umma au waajiriwa wenye umri wa miaka isiyopungua 50 na kuendelea, wakitumia wasifu wa kazi zao kujitangaza na hata yale waliokwishafanyia wananchi kupitia nyadhifa zao ili kupata kura na kuwatumikia wananchi. Wakati mwingine, wagombea walikuwa wamekwisha kustaafu ndipo wakagombea nyadhifa za kisiasa. Ilikuwa nadra sana, kukuta kijana ametoka shuleni au chuo ama kuacha ajira yake na kuingia katika siasa kama mgombea. Yawezekana hapakuwa na muamko, maslahi, ama hofu ya kushindwa, ama wananchi kwa wakati ule hawakuwa na imani sana na kijana, na mambo mengine kama hayo. Hii ilitokana na ukweli kwamba kila mwanasiasa aliyetaka kugombea alikuja kumuona baba yangu2 na kumuomba ushauri kabla ya kujitangaza kijijini na hata katika kata yetu kwa ujumla. Japokuwa sikuona kijana wa wa miaka 25 hadi 35 akitokea kugombea nyadhifa hizi, inakuwa jambo la kushangaza ambalo ni suala la kumbukumbu tu ya kihistoria kwamba Hayati Baba wa Taifa alikuwa Waziri Mkuu wa Tanganyika mwaka 1961 baada ya uhuru na Rais wa Tanganyika mwaka 1962. Hivyo, akiwa na miaka 39 alikuwa waziri Mkuu na akiwa na miaka 40 alikuwa Rais wa kwanza wa Tanganyika. Katika muonekano na uhalisia wa zama tulizonazo, tunasema mwalimu ndiye mtu pekee aliyekuwa Rais akiwa mdogo kuliko marais wote wane hadi kufikia sasa. Swali la msingi la kujiuliza, je nini maoni ya wananchi kuhusu utendaji wa wanasiasa vijana na Matarajio yao kwa vijana kuelekea uchaguzi mkuu wa 2015 yakoje?


1.1 Kuhusu Tanzania
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni Muungano wa nchi mbili za Tanganyika na Zanzibar, zilizokuwa nchi moja tangu tarehe 26 Aprili, 1964. Nchi hizi mbili zilipata uhuru wake kwa nyakati tofauti Tanganyika ikiwa imepata uhuru mwaka 1961 kutoka kwa Waingereza na Zanzibar ikipata uhuru wake mwaka 1963 kwa njia ya mapinduzi kutoka katika utawala wa Kisultani. Kufuatia Muungano wa Tanganyika iliyokuwa inaongozwa na Chama cha Siasa cha TANU na Zanzibar iliyokuwa inaongozwa na Chama cha Siasa cha ASP, vyama hivi vilikuja kuungana tarehe 05 Februari, 1977 na kuwa chama kimoja ambacho ni Chama cha Mapinduzi (CCM) ambacho ndicho chama tawala hadi sasa nchini Tanzania, na moja ya vyama vya siasa vikongwe barani Afrika.
Kwa kuzingatia wimbi la demokrasia duniani, Tanzania iliingia katika siasa za vyama vingi tangu mwaka 1992; mfumo uliopokelewa kama chachu ya kupanua fursa za kuendesha nchi kwa misingi ya utawala bora, uwajibikaji na uwazi ili kuongeza tija katika nyanja mbalimbali za kiutawala, siasa na hata uchumi. Kwa msukumo huo, siasa za vyama vingi ziliendeshwa kupitia chaguzi kuu nchini kuanzia mwaka 1995, 2000, 2005 na 2010; na hadi utafiti huu unafanyika, ni sehemu ya kutathmini utendaji wa kundi muhimu la kijamii, yaani kundi la vijana linalosongwa na pamoja na mambo mengine, ukosefu wa ajira. Hivyo basi, siasa inachukuliwa kama sehemu ya vijana kuonyesha uwezo na umahiri wao kiuongozi lakini pia ufumbuzi wa tatizo la ajira.
Katika kipindi chote cha siasa za vyama vingi hapa nchini, wagombea wamekuwa wakitumia fursa ya kikatiba kugombea nafasi mbalimbali bila ya kujali jinsia, itikadi, dini na hata kabila. Wanawake kwa namna ya pekee wamekuwa wakipewa nafasi za viti maalumu3 ili kuhakikisha wanapata uwakilishi katika nyadhifa muhimu kwa viti vya udiwani na ubunge. Nafasi hizi za viti maalumu hazijatokea kupendekezwa ama kutolewa kwa vijana kama kundi muhimu linalopaswa kupewa nafasi, na hivyo wengi wao katika zama hizi wanafanya jitihada kugombea nafasi mbalimbali za uchaguzi mkuu kama vile udiwani na ubunge.
Ni wazi kwamba Tanzania ni moja ya nchi duniani ambazo katika ngazi za vyama vya siasa i.e. Chama tawala na hata vyama vya upinzani, vijana wamekuwa wakipewa nafasi kubwa katika uongozi wa juu. Nafasi walizokwisha shika vijana ni pamoja na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Naibu Makatibu Wakuu Taifa, Wajumbe wa Mkutano Mkuu katika vyama vyao (Wa-NEC), Wasemaji wa vyama, n.k. Kupitia nafasi za kuchaguliwa kupitia Uchaguzi Mkuu, Taifa letu limeshuhudia vijana wanasiasa na hasa wabunge wa Chama Tawala wakipewa nyadhifa kubwa za Uwaziri, Naibu Waziri, Wenyeviti wa Kamati muhimu za Bunge, na wengine kwa jitihada zao na uzalendo kwa Taifa wakiibua mambo makubwa ya kimaslahi kwa Taifa kwa ujasiri mkubwa na umahiri.
Pia katika kipindi kifupi, tumeshuhudia vijana katika nyadhifa mbalimbali za kisiasa, wakiwajibika pale ambapo wanahusika aidha moja kwa moja au hata sio moja kwa moja, na hivyo kuachia nyadhifa zao kama sehemu ya uwajibikaji. Katika hali hiyo, tumeona misimamo ya vijana hao na uaminifu wao kwa vyama, serikali na hata kwa wananchi, huku wakipokea anguko za kisiasa kwa ukomavu wa kisiasa kama sehemu ya uawjibikaji.



1.2 Kuhusu TEDRO
Asasi isiyo ya kiserikali ijulikanayo kwa jina la TEDRO i.e. Tanzania Education Development Research Organization ilianzishwa Machi 2011 kwa lengo la kuendesha utafiti katika Sekta ya Elimu nchini. Hadi sasa asasi ya TEDRO inaendesha utafiti wa Mitandao ya kijamii inavyoathiri wanafunzi wa sekondari na kutazama njia rafiki katika kutumia mitandao hiyo kama njia ya kujifunzia na kuendeleza sekta nzima ya elimu.4 Pia kwa kutambua kuwa demokrasia ni suala mtambuka na vijana ni chachu katika jamii, TEDRO imeamua kuendesha pia utafiti huu wa Ushiriki wa Vijana katika Siasa kama wagombea. Utafiti tunaouendesha ni muendelezo wa uchambuzi wa changamoto za elimu, ndani ya dira ya TEDRO na program ya mchango wa elimu katika kufungua fursa za ajira, siasa ikiwa mojawapo ya fursa zenye kimbilio la vijana leo hii. Ni dhahiri kwamba, uwezo wa wahitimu wa ngazi yoyote kupata ajira hutokana na elimu waliyoipata, hutoa taswira ya ubora wa elimu yenyewe.
Kama inavyojieleza, maendeleo ya elimu yanaweza kujulikana katika utendaji wa wataalamu waliopatiwa elimu na ufanisi wao. TEDRO kwa kupitia programu ya "Tanzania Education System and Competence in the Career" inayotazama kwa kina jinsi gani elimu itolewayo inakidhi hitaji la soko na uwezo wa wahitimu katika soko; kwa awamu ya kwanza kabisa, shirika letu limetumia fursa na kipindi hiki cha kuelekea Uchaguzi Mkuu kukusanya maoni toka kwa wananchi ili kutathmini vijana walioingia katika siasa kupitia uchaguzi Mkuu tangu mwaka 2000 hadi sasa.
TEDRO yenye makao yake Makuu Dar es Salaam, kwa kupitia utafiti huu inawapa vijana walioko katika siasa fursa ya kujitathmini kupitia maoni ya wananchi yaliyotolewa katika ripoti hii na hivyo kuweza kujiaandaa kwa ufanisi zaidi wanapoelekea uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015. Utafiti huu unaojulikana kama "Vijana katika Siasa Kuelekea Uchaguzi Mkuu 2015" ni kichocheo muhimu katika kuwafanya vijana na hata wanasiasa wengine kuwa makini katika siasa na kuelewa kuwa, katika utendaji mzuri wenye kuwatumikia watu, siasa yaweza kuwa nyenzo muhimu katika kutatua changamoto za kimaendeleo katika Taifa letu.
Ni wazi kwamba vijana wamekuwa na msukumo mdogo sana kushiriki katika kupiga kura, na hata kuomba kupigiwa kura kama wagombea, jambo linaloweza kuwa na ushawishi hasi kwa jamii nzima. Likiwa ni kundi linalopenda mabadiliko kama ilivyo popote duniani, vijana wanakuwa na mwamko mkubwa pale wanapoona kijana mwenzao, wa rika lao, wa mazingira yao, ajuaye shida zao anagombea kwa nafasi ya kuchaguliwa. Kwa tathmini ya muonekano kupitia uchaguzi wa serikali za Mtaa, maeneo mengi vijana wamejitokeza kwa wingi kupiga kura na hata kugombea. Yawezekana, vijana wamejitokeza aidha kwa sababu wagombea waliokuwepo ni vijana pia, au vijana wamegombea zaidi kwa sababu wapiga kura vijana wameongezeka, au elimu ya uraia imetolewa vya kutosha.

1.3 Malengo ya utafiti huu
Ni dhahiri kwamba huu ni utafiti wa kwanza na wa pekee kufanywa na asasi ya TEDRO. Lengo kuu likiwa ni kutathmini ushiriki wa vijana katika siasa kama wagombea, namna vijana wanavyopokelewa na wanachi katika siasa na matarajio tunapoelekea uchaguzi mkuu wa 2015. Lengo hili kuu, limepelekea utafiti huu kuchambua malengo mahususi manne yafuatayo:
  1. Ushiriki wa vijana katika siasa kama wagombea
  2. Mchango wa wanasiasa vijana katika kufuata misingi ya utawala bora na uwajibikaji
  3. Utekelezaji wa ahadi za wagombea kwa wapiga kura
  4. Matarajio ya wananchi kwa vijana tunapoelekea uchaguzi Mkuu wa 2015.

1.4 Maswali ya msingi katika utafiti huu
  1. Kuna mwenendo gani wanasiasa vijana katika uchaguzi mkuu kama wagombea?
  2. Ni kwa kiasi gani vijana wanasiasa huongoza kwa kufuata misingi ya utawala bora?
  3. Ni kwa kiasi gani vijana wanasiasa wa kuchaguliwa wametekeleza ahadi na matarajio ya wapiga kura?
  4. Nini matarajio ya wananchi kwa vijana?

1.5 Matarajio ya utafiti huu
  1. Kwa matokeo ya utafiti huu, ni matarajio ya asasi yetu ya TEDRO kuwa wasomaji wetu na watanzania kwa ujumla, hususani wananchi na vijana wenye nia za kujihusisha na siasa, watatambua kuwa kundi la vijana lina wajibu mahususi katika kukuza demokrasia na utawala bora. N hivyo, kuongeza ushiriki wa vijana katika kutatua changamoto za maendeleo katika Taifa letu.
  2. Pia utafiti huu umetoa nafasi ya wananchi kutoa maoni yao kuhusu namna vijana wanavyotumikia nafasi zao za kisiasa kama viongozi wa watu kwa kufuata misingi ya utawala bora; hivyo basi wananchi wamezingatia mambo yaliyoulizwa kama ushirikishwaji katika maamuzi, kupiga vita rushwa na uwazi katika mambo yanayohusu maslahi ya taifa kwani ndio dhana zilizoweza kufafanua maana ya utawala bora.
  3. Kwa kuelewa usemi wa wahenga kuwa "ahadi ni deni" utafiti huu unatoa changamoto kwa vijana walioko madarakani na wanaotarajia kugombea nyadhifa mbalimbali kutambua kuwa kutekeleza ahadi ni moja ya vitu vinavyopelekea kijana na hata mgombea mwingine kupata ushawishishi, kukubalika na hata kuaminika katika jamii.
  4. Kutoa mtazamo wa jumla toka kwa wananchi kuhusiana na wanasiasa vijana Taifa linapoelekea Uchaguzi Mkuu wa 2015.

2. Mapitio ya maandiko na tafiti zilizopita
2.1 Tafsiri ya kina kuhusu dhana ya Vijana
Utafiti huu unaohusisha vijana katika nyanja ya siasa, unaanza kwa kuchambua dhana ya kijana. Tafsiri mahususi ni ile ya umri kati ya miaka 18 hadi 25, na wakati mwingine kati ya miaka 18 hadi 35. Zaidi ya maana za kidemographia, katiba inatambua kijana kwa misingi ya kupiga kura kwamba inaanzia miaka 18 na kuendelea, wakati kugombea nafasi za uongozi katika siasa umri wa kuanzia in miaka 25 na kuendelea kwa nafasi ya udiwani na ubunge, wakati nafasi ya uraisi huanzia miaka 40 na kuendelea.
Licha ya kwamba maana ya kidemographia, kijana ni miaka 18 hadi 35, ni dhahiri kwamba kwa maana ya kijana ileambapo tunaenda zaidi kwa kuweka bayana kwamba umri halisi wa kikatiba wa kugombea nafasi za kisiasa za udiwani na ubunge huanzia miaka 25 hadi 35 na kwa nafasi ya uraisi huanzia miaka 40 na kuendelea. Tafsiri hii pana ya "kijana" imeweza hata kuzishawishi fikra za wananchi na umma wa ulimwengu huu kwamba endapo mtu akiwa raisi katika umri wa hadi kufikia miaka 55 bado anachukuliwa ni raisi kijana.
Ni wazi kwamba hata Mheshimiwa Raisi Jakaya Mrisho Kikwete aliyeanza kutumikia Wadhifa wa Uraisi akiwa na miaka 55 watu walimpokea kama Rais kijana, japo katika maana halisi ya kijana sio sahihi ila katika mtazamo mpana na ulinganishi na watanglizi wake, alitambulikana kama kijana. Ni wazi kwamba historia inabaki kuwa aliyebeba madaraka haya makubwa ya Urais akiwa kijana zaidi ni Hayati Baba wa Taifa Julius Kambarage Nyerere akiwa na miaka 39 alikuwa Waziri Mkuu wa kwanza wa Tanganyika na akiwa na miaka 40 akawa Raisi wa kwanza wa Tanganyika.
Kuondoa utata wa tafsiri ya neno "kijana" kutoka uhalisia wa miaka 18 hadi 35, utafiti huu unawajumuisha vijana wanasiasa wote waliokuwa na miaka isiyozidi 35 kuanzia mwaka 2000 ili kuweza kukidhi tafsiri pana ya mtazamo wa walio wengi kuhusu neno kijana katika nyanja ya siasa na utawala kwa utamaduni wa Afrika.
Ikiwa vijana ni kundi lenye watu wengi nchini ukilinganisha na makundi mengine, faida ya uwingi wa kundi hili, ni pale tu litakapotumika kama nyezo ya kujenga demokrasia na ushawishi; na ili kuwafanya wawe chachu ya mabadiliko katika siasa.5
Kuna ushahidi hadi likitoka andiko la Ellis (2007) kuwa ushiriki wa vijana katika siasa ulikuwa mdogo ukilinganisha na watu wa rika zingine popote duniani. Upigaji kura kama moja ya misingi ya ushiriki katika siasa na demokrasia ni mfano halisi uliokwisha kuwa na ushiriki mdogo wa vijana. Hii inaenda hata katika ushiriki wa vijana katika uanachama na uongoi katika siasa na hata mabunge. Hali hii imetafsiriwa na Ellis (2007) kuwa inatokana na mifumo ya kiutawala nje ya serikali, mfano utawala wa kimila ambao hufuata umri katika uongozi na kutotoa fursa kwa vijana kuwa viongozi (Ellis, 2007).
Vikwazo katika ushiriki wa kijana ni pamoja na umri wa kikatiba katika kupiga kura au kugombea nafasi za kisiasa. Umri wa kupiga kura kwa nchi ya Tanzania huanzia miaka 18, wakati nchi a Amerika ya kusini ni miaka 16, wakati Indonesia na Korea ni miaka 17, Cameroon na Japan miaka 20, Cote D'Vore, Gabon, Singapore, UAE na Pakistan ni miaka 21. Ila umri wa kupiga kura kwa Africa ni kama Tanzania ambao wastani wake pote ni miaka 18. Hakuna tafiti zilizotoa angalizo au pingamizi la umri endapo, kuwaacha vijana hadi miaka 18 ndio waanze kushiriki kupiga kura ni chanzo cha wao hata pale umri unapofika huacha kushiriki ama vinginevyo (UNICEF & United Nations Programme on Youth, 2011).
Imethibitika kwamba demokrasia ya zama hizi zenye kuwahusisha kwa kiasi kikubwa vijana katika mchakato wa siasa ni jambo la msingi. Ushiriki wa kundi la vijana hufanya zile tunu msingi za kidemokrasia zionyeshe uhai wake na hivyo kuzuia utawala usio na kikomo kudumu katika siasa za leo na hata baadae.
Andiko lililofanywa na shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa – UNDP (2011) limeweka wazi dhamira ya dhati iliyo nayo jumuiya ya kimataifa katika kutambua umuhimu wa vijana katika siasa, kwa kuzingatia kwamba vijana ni chachu ya mabadiliko, kama ilivyo katika kanuni za Umoja wa Mataifa.6
Katika andiko la mwanazuoni nguli wa zama za leo, hayati Chachage (2005), amejadili mtazamo wa tafsiri ya wanasayansi ya jamii kuhusu kuibuka na kushamiri kwa muamko wa vijana katika siasa ikiwa ni pamoja na mapungufu ya watangulizi katika kutimiza mahitaji ya jamii husika. Wengine wakienda mbali zaidi na kusema ni ishara ya vijana kutoridhika na hali iliyopo au ilivyo kwa wakati husika; na hivyo shauku na muamko wa vijana ni tamaa ya kutaka kufanya vizuri zaidi ama tofauti kwa maslahi na matakwa ya kizazi cha vijana. Iwe iwavyo, tafsiri inabaki kuwa msukumo wa vijana hautokani na kingine chochote, bali shauku ya mabadiliko, yote yakiwa ni msukumo utokanao na mabadiliko yatokeayo kwinginepo duniani (Chachage, 2005).
Pia upo mtazamo kuwa, msukumo wa vijana unatokana na mfumo wa kidesturi kushindwa kutimiza matakwa ya kizazi na jamii ya sasa; ikiwa ni pamoja na ongezeko la uelewa wa haki na wajibu wa kiraia alionao kijana katika jamii; huku wakijiona kuwa wanaweza kuwa na njia mbadala na madhubuti za kutatua matatizo yaliyopo (Ibid).
Chachage (2005) anaweka bayana mtazamo kinzani7 na msukumo wa vijana katika zama za leo. Japokuwa imezoeleka kwamba "vijana ni taifa la kesho", fikra hizi zilipata upinzani mkubwa nchini Tanzania miaka ya 1980, vijana walipaza sauti zao wakisema, "vijana ni taifa la leo"8. Pia utafiti huu umemnukuu mwanafalsafa na mwanahistoria nguli wa Ufaransa Frantz Fanon aliyesema (Nukuu niliyoitafsiri):
"Kila kizazi ni lazima kuyatambue malengo yake, kiyatekeleze au kuyasaliti"9
Usemi huu umetafsiriwa kuwa wajibu wa vijana kwa siku zijazo hutegemeana na jinsi wanavyotumia fursa walizonazo wakati huu, rasilimali walizonazo wakati huu, na hivyo, kuacha jukumu la kuiandaa kesho waitamaniyo kwa kizazi kingine ni usaliti.
Katika hotuba yake ya kuhitimisha siku ya Viongozi vijana duniani kupitia, US-Africa Leaders Summit, Rais wa Marekani Barack Obama alisema mataifa ya Africa hayana budi kuwekeza kwa viongozi vijana kwani kundi hili linaweza kupaza sauti na kusikika (huenda ni kwa sababu ni wapenda mabadiliko, wana nguvu na pia ni wengi). Kundi hili laweza kuwa chachu ya kuleta mabadiliko katika kilimo, kupiga vita maradhi na hata kuleta amani katika bara la Afrika (Washington D.C, Agusti 6, 2014).10
Ushawishi katika kuwahusisha vijana katika siasa na uongozi pia umesisitizwa na watu maarufu duniani akiwepo Dr. Koffi Annan, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, katika nukuu inayotafsirika kama ifuatavyo:
"Hakuna aliyezaliwa raia mwema, hakuna taifa lililoanza likiwa la kidemokrasia. Bali, yote ni michakato inayokuja katika kipindi fulani cha kihistoria wa uhai wa mtu au taifa husika. Hivyo, vijana wanatakiwa kuhusishwa kutoka wanapozaliwa, kwa kuwa taifa llinalowatenga vijana linajilaani a kujichimbia kaburi la kifo"11 (Koffi Annan, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa).
Katibu Mkuu wa UN aliyeko madarakani Ban Ki Moon ameendelea kuiagiza taasisi ya Umoja wa Mataifa ya United Nations Inter-Agency Network on Youth and Development kutoa hamasa kwa vijana ulimwenguni pote kushiriki katika siasa, uongozi na kukuza demokrasia na utawala bora. 12 Andiko la ripoti ya UNDP (2012) limetoa msisitizo,13 kama ilivyowekwa katika tafsiri ya Kiswahili ya utafiti huu:
"Ni lazima vijana wapewe nafasi katika kufanya maamuzi kuanzia ngazi za chini, ngazi ya taifa and hata kimataifa" (Katibu Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon).

3. Maelezo Kuhusu Mbinu ya Utafiti
3.1 Utangulizi
Utafiti huu umeandaliwa na kufanyika Tanzania Bara (Tanzania Visiwani haikuhusishwa katika awamu hii) na ni utafiti wa kwanza kufanywa unaousiana na ushiriki wa vijana katika siasa. Maeneo yaliyohusishwa katika utafiti huu ni kanda za kijiographia hapa nchini ili kuwezesha uhusishwaji mpana wa Watanzania. Katika kila kanda, utafiti huu umehusisha wilaya 1 hadi 3, na katika kila wilaya, wamehojiwa wananchi wa vijiji vitatu, ambavyo vingine vipo katika kata moja ama kata tofauti kwa kuzingatia siasa za eneo husika. Katika kila kijiji, wamehojiwa watu 15. Vijiji hivi vimechaguliwa makusudi katika kila wilaya kwa kuzingatia vuguvugu za kisiasa zama hizi za vyama vingi, ili mitazamo isiathiriwe na mwelekeo wa wananchi wa vijiji vilivyo chini ya ushawishi wa chama kimoja.

3.2 Mgawanyo wa maeneo yaliyohusishwa
Awali ya yote, watafiti wa TEDRO kwa kutambua ukumbwa wa nchi yetu ya Tanzania, hususani Tanzania bara ambapo utafiti huu umefanyika kwa awamu ya kwanza waliweza kutafuta tafsiri ya migawanyo kikanda, wilaya, majimbo ya uchaguzi na vijiji. Mambo mengine ni pamoja na tofauti ya itikadi za kisiasa, upatikanaji wa habari muhimu kuhusiana na siasa na uhalisia wa wananchi waishio mijini na vijijini. Mgawanyo huu ulikuwa kama jedwali linavyoonyesha:
Kanda
Wilaya/ majimbo ya Uchaguzi
Vijiji
Mashariki na Pwani
Morogoro, Kinondoni & Kisarawe
Vijiji 3 kila Wilaya
Kusini
Kilwa, Lindi Mjini & Mtwara Mjini
Vijiji 3 kila Wilaya
Nyanda za Juu Kusini
Njombe, Mbeya Mjini na Ludewa
Vijiji 3 kila Wilaya
Kanda ya Kati & Kaskazini Magharibi
Singida Mjini, Kasulu & Kigoma
Vijiji 3 kila Wilaya
Kanda ya Kaskazini
Tanga Mjini, Moshi Vijijini & Arumeru
Vijiji 3 kila Wilaya
Kanda ya Ziwa
Bukoba Vijijini, Biharamulo & Nyamagana
Vijiji 3 kila Wilaya
Jumla
Wilaya 18 Tanzania
Vijiji 54 Tanzania
IDADI YA WAANCHI WALIOHOJIWA

WANANCHI 910


3.3 Hatua zilizofuatwa katika kuufanya utafiti huu
Wataalamu wa TEDRO walitoa mafunzo kwa ajili ya kukusanya taarifa za utafiti huu, ambapo watafiti wasaidizi 25 walipatiwa mafunzo. Watafiti wasaidizi hao ni wahitimu vyuo ambao walichukuliwa kwa kazi hii kwa kuzingata uzoefu na uadilifu wao katika kufanya kazi ya aina hii. Watafiti hawa walishiriki mafunzo na kisha kufanya majaribio (Pilot) ambapo pamoja na mambo mengine, majaribio yalipima endapo dodoso linaeleweka kwa wananchi na muda ambao watafiti wasaidizi watatumia ili kukamilisha kazi hii. Marekebisho ya muhimu yalifanyika ili kuwezesha walengwa kuelewa na hivyo kutoa taarifa sahihi kwa kazi hii.

3.4 Mambo ya kiitifaki, ruhusa na maadili
Kama ilivyo kwa tafiti zinginezo, utafiti huu uliandaliwa na andiko lake limekabidhiwa kwa Tume ya Sayansi na Teknolojia, ambayo ndio mamlaka yenye dhamana ya kutoa ruhusa ili utafiti kufanyika. Pia utafiti huu umehusisha kujitambulisha kwa watafiti wa TEDRO katika mamlaka za kiutawala mikoani na wilayani. Mara nyingi, watafiti walipeleka barua ya utambulisho kwa Ofisi ya Mkurugenzi wa kila wilaya iliyohusika, na wakati mwingine barua ya utambulisho ilianzia kwa Katibu Tawala wa Mkoa (RAS), Wilaya (DAS) nas kwa Mkurugenzi (DED).
Baadhi ya Wilaya watafiti walipatiwa barua za ruhusa na baadhi ya wilaya ambapo walichelewa kutoa ruhusa, watafiti waliendelea kukusanya taarifa, hasa pale ilipotokea kuwa wanagharamika wilayani kwa siku zaidi ya mbili bila kufanya kazi tangu wafikishe barua wilayani, na kulazimika kutumia nakala ya barua ya Utambulisho kutoka TEDRO kukusanya taarifa; na pale ilipotokea kuwa ruhusa haikutolewa ofisi ilishauri waende wilaya walizotoa ruhusa kufanikisha zoezi la utafiti kwa wakati na kwa gharama iliyokuwa katika uwezo wa ofisi yetu. Kwa sababu za kiitifaki na urasimu katika kufuatilia ruhusa, utafiti huu uliotarajiwa kuhusisha wilaya 24 hapo awali kwa sampuli ya vijiji 72 na wahojiwa 1,080, hatimaye ni asilimia 84.2% maeneo yaliyotarajiwa yaliweza kufikiwa.
Kila watafiti walipoenda kukusanya taarifa walijitambulisha kwa mhojiwa ambaye alikuwa mwananchi mwenye umri wa miaka 18 na zaidi, waliyemkuta katika kaya, maeneo ya kazi na hata katika biashara na kuomba kufanya mazungumzo naye yanayohusu vijana na ajira, hususani wale walioko katika siasa tayari ama wagombea watarajiwa.
Kaya ilitambulika pale ambapo kijiji au mtaa husika uliweza kufahamika sehemu ya huduma muhimu kwa umma kama hospitali, shule ama kitua cha magari au soko, wakati mwingine njia panda na hata makutano ya barabara yalitumika ili kupata sehemu ya kuanzia. Mtafiti wa TEDRO alitumia eneo hili kama sehemu ya kuanzia huku akihesabu nyumba tano kwenda pande kuu tatu kufuatia mahali alipofikia palivyo. Kila kaya alipohoji, aliruka kaya tatu na kuchukua kaya ya nne kwa kila upande hadi kukamilisha idadi ya wahojiwa. Mambo yaliyozingatiwa ni jinsia ya mhojiwa na umri kwa maana pana ya motto wa kike ama wa kiume kwenye miaka 18 katika kaya, mzazi wa kiume au mzazi wa kike. Makundi yalizingatiwa kila mtafiti alipotoka kaya moja kwenda nyingine.
Watafiti waliaswa na kusimamiwa ili kuhakikisha wanakusanya taarifa za kweli ili kufanya utafiti huu uakisi ukweli wa kimtazamo wa wananchi waliohojiwa na kuufanya kuwa andiko lenye kuweza kufanyiwa rejea wakati wa kufanya tathmini za kisiasa na hata kuwezesha kundi la vijana wanasiasa kutumia utafiti huu kujifunza na kujitathmini wanapojiandaa kushiriki uchaguzi mkuu wa mwaka 2015. Angalizo lingine kwa watafiti lilikuwa ni kuhakikisha wanakwepa makundi yenye ushawishi wa ghasia na ushabiki wa kisiasa ili kuwaepusha na vurugu pale ambapo hakuna uvumilivu wa kisiasa ama maeneo yenye migogoro yenye kutafsiriwa kuwa ya kisiasa. Haya yote yalizingatiwa hadi hatua ya ukusanyaji taarifa ikakamilika bila kupokea taarifa za uvunjifu wa amani maeneo taarifa zilipokusanywa.


3.5 Kuingiza taarifa na kuandaa ripoti
Taarifa zimeingizwa kwa kutumia SPSS14 i.e. ambao ni mfumo wa uingizaji data na kuziweka katika namna ziwezavyo kuhusianishwa kirahisi. Waingiza taarifa walipatiwa mafunzo maalumu na wakisimamiwa na Msimamizi wa uingizaji taarifa aliyeandaa mfumo mzima wa kuingizia taarifa. Wataalamu katika utafiti waliohusishwa katika uandaaji wa andiko la utafiti huu walishirikishwa katika kutumia taarifa zilizokusanywa na kuingizwa katika mfumo wa data wa komputa.
4. Matokeo ya Utafiti
4.1 Taarifa binafsi za kidemografia
Utafiti huu uliotarajiwa kuhusisha wilaya 24 Tanzania Bara, umeendeshwa katika wilaya 18, kila wilaya ikiwa imewakilishwa na wahojiwa 45 waliochaguliwa 15 kutoka kila kijiji; hivyo utafiti huu kuhusisha vijiji 54 kwa ujumla. Wilaya ambapo utafiti umefanyika ni Njombe Mjini, Ludewa, Mbeya Mjini, Kilwa, Lindi Mjini, Mtwara Mjini, Morogoro Mjini, Kisarawe, Kinondoni, Tanga Mjini, Vunjo, Arumeru, Singida, Kasulu, Kigoma Mjini, Bukoba Vijijini, Biharamulo na Mwanza Mjini (Nyamagana). Katika utafiti huu, taarifa binafsi za wahojiwa zilizokusanywa ni pamoja na zile zinazohusu umri wa wahojiwa, jinsia, hali ya ndoa, kazi, kiwango cha elimu na vyama vya siasa vinanvyoongoza majimbo sehemu uchaguzi ulipofanyika.
Taarifa binafsi za Wahojiwa
  1. Wahojiwa walikuwa wa makundi ya umri mbalimbali, na taarifa zinaonyesha wahojiwa wa umri kati ya miaka hadi 20 ni 8%, miaka 21 hadi 30 ni 32%, miaka 31 – 40 ni 32%, miaka 41 – 50 ni 13%, miaka 51 hadi 60 ni 13% na Zaidi ya miaka 60 ni 2%.

  1. Kuhusiana na jinsia ya waliohojiwa, taarifa zinaonyesha kuwa wanaume ni 58% na wanawake ni 42%. Uwiano huu katika jinsia unatoa fursa ya kwamba hakuna kundi lililozidi kwa kiasi kikubwa kinachoweza kuathiri matokeo ya utafiti kwa sababu tu kundi moja limetawala zaidi. Isitoshe, wanaume wana ujasiri kuliko wanawake katika kukubali kuhojiwa, na hivyo hii huenda imesababisha uwiano huu wa wanaume kuwa wengi zaidi kuliko wanawake.
  1. Hali ya ndoa nayo imepewa uzito katika kukusanya taarifa binafsi maana ushiriki katika siasa na mambo ya kijamii kuna uhusiano wa karibu sana na hali ya ndoa ya mhojiwa. Katika utafiti huu, wahojiwa ambao hawajaoa au kuolewa ni 37% na waliooa/olewa ni 51% huku makundi mengine yakiwa ni 12% ambayo ni yale ya mzazi mmoja, watalaka na wajane.

  1. Taarifa nyingine muhimu kwa wahojiwa ilikuwa ya kiwango cha elimu, inayoonyesha kuwa wahojiwa waliohitimu elimu ya msingi ni (40%), sekondari (33%), chuo (23%) na wasiosoma wakiwa (4%).

  1. Wahojiwa wamejitambulisha na kutaja itikadi zao ambapo, kwa ujumla wapo wasio na vyama, na wapo wafuasi wa CCM, CHADEMA, CUF, TLP na NCCR Mageuzi. Pia mahojiano yalihusisha majimbo ya uchaguzi ya vyama vya siasa vyote vilivyoorodhoshwa hapa, isipokuwa UNDP na vyama visivyo na uwakilishi bungeni.


4.2 Ushiriki wa Vijana katika nafasi za Uchaguzi Mkuu
4.2.1 Kugombea na Matokeo ya Uchaguzi
Utafiti huu umeandaliwa kwanza kutazama mwenendo wa ushiriki wa vijana katika nafasi za uchaguzi mkuu kama wagombea, hususani udiwani na ubunge. Matokeo yanaonyesha kuwa 65% ya wananchi waliohojiwa wanakiri kuwa vijana wameshiriki katika kugombea nafasi za udiwani, huku 35% wakisema vijana hawajashiriki kugombea nafasi hizo katika maeneo utafiti ulipofanyika. Kwa upande wa vijana kugombea ubunge, 63% wanakiri kuwa vijana wamekuwa wakigombea nafasi za ubunge na 37% wakisema hapana, hakujawa na ushiriki wa vijana kugombea nafasi hizo katika maeneo yao.
Pia utafiti ulienda zaidi kutaka kujua endapo pale vijana walipoonyesha nia ya kugombea, waliweza kushinda au walishindwa. Matokeo ya utafiti huonyesha kuwa 20% wanasema kijana alishinda udiwani tu, 32% wanasema kijana alishinda ubunge tu, 30% wanasema vijana waliogombea walishinda maeneo yao katika udiwani na ubunge pamoja, huku 18% wakisema vijana waliogombea hawakushinda udiwani wala ubunge.


4.2.2 Sababu za kushinda Vijana
Utafiti huu umepelekea majibu mbalimbali ya sababu zilizofanya vijana washinde katika nafasi walizogombea za uchaguzi mkuu, hususani udiwani na ubunge. Sababu hizo ni kama zifuatazo na asilimia za waliozipendekeza:
Na.
Sababu
Asilimia
1.
Kiwango cha elimu na uwezo wa kuelezea sera za vyama vyao
16%
2.
Kutaka mabadiliko, hivyo kuondoa waliokaa sana na kuweka vijana
48%
3.
Kutoa ahadi zinazotekelezeka, ikiwepo ajira kwa vijana
6%
4.
Kuungwa mkono na vijana katika kampeni hadi siku ya kura
17%
5.
Kada mahiri wa chama chake, hivyo kaungwa mkono na chama chake
8%
6.
Kugombea kupitia chama cha upinzani kupelekea vijana kushinda
13%
9.
Ni chagua na kipenzi cha watu, kila kigombea kijana huleta ushawishi
7%
10.
Kulinda kura zisiibiwe, na hivyo kufanya vijana wakashinda
10%
11.
Kupendelewa na kura kuibiwa
2%
12.
Udhaifu wa watangulizi kushindwa kutekeleza ahadi walizotoa
6%
13.
Amekuwa na jamii kwa karibu akitoa misaada mbalimbali
16%


4.2.3 Sababu za vijana kushindwa katika uchaguzi
Matokeo ya utafiti yanaonyesha kuwa, sio vijana wote walioshinda wakati wa uchaguzi mkuu. Katika kutafuta sababu za kushindwa, zimejitokeza sababu nyingi kama ifuatavyo:
Na.
Sababu
Asilimia
1.
Rushwa ilitumika kuhakikisha kijana hapiti naye hakuwa na hela
23%
2.
Vijijini hawajaamua kuwapa vijana, bado wanataka wazee
3%
3.
Vijana wamekuja kwa kupitia Upinzani ambayo bado haikubaliki maneo mengi ya vijijini
32%
4.
Aliyekuwepo ni mzee na anakubalika sana hadi aachie mwenyewe
6%
5.
Vijana hawaombi ushauri kwa wazee, wanakuja tu na kutukana majukwaani
7%
6.
Kijana hakuwa amejipanga, na hivyo kushindwa kutetea kiti, hakuwa na hela
24%
9.
Alikubali hongo ili matokeo yabadilishwe na hivyo kupoteza nafasi yake
26%
10.
Kuibiwa kura
4%
11.
Kazi nzuri iliyofanywa na Mbunge aliyekuwepo haikuwapa vijana nafasi tena
13%
12.
Matusi na karaha za vijana waliotaka nafasi mbalimbali zilikera wapiga kura, hasa wazee
6%
13.
Hawana uzoefu na kazi hiyo
11%


4.2.4 Kuhusu ongezeko la Vijana katika siasa
Utafiti huu umetoa fursa kwa wananchi kutoa maoni kuhusiana na mtazamo kuwa kumekuwa na ongezeko la vijana kuingia katika siasa kama wagombea wa nafasi mbalimbali za uchaguzi mkuu. Mtazamo huu umetolewa majibu kama ifuatavyo: 83% wamesema ndio wanakubali kuwa kuna ongezekola vijana kuingia katika siasa; 4% wamesema kuwa hawakubaliani na mtazamo kuwa kuna ongezeko la vijana kuingia katika siasa kama wagombea; na 13% hawajui. Mtazamo huo, umewakilishwa katika mchoro unaofuata hapa chini.


4.2.5 Sababu za Vijana kuingia katika siasa kwa nafasi za Uchaguzi Mkuu
Utafiti huu uliweka sababu mbalimbali zinazoweza kuwa kichocheo cha vijana kuingia katika siasa. Sababu kadhaa zimechukua uzito, hasa pale ambapo wananchi aliohojiwa kuzikubali kuwa zimechangia vijana kuingia katika siasa. Sababu zilizopewa nafasi kubwa na asilimia zake ni uzalendo 67%, kimbilio baada ya kukosa ajira 57%, uwezo mdogo wa watangulizi wao katika nafasi husika 60%, mafanikio ya wanasiasa vijana walio mahiri 72%, vyma vya siasa kuwapa vijana nafasi katika vyama vyao 59%, kukubalika kwa vijana tu sababu ni vijana 63%. Matokeo haya yameonyeshwa katika jedwali linalofuata chini:
Na.
Sababu
Asilimia
Ndio
Hapana
1
Uzalendo
67%
33%
2
Uchu wa madaraka
37%
63%
3
Kimbilio baada ya kukosa ajira
43%
57%
4
Kushauriwa kugombea sababu ya umahiri wa vijana katika siasa za zama hizi
50%
50%
5
Uwezo mdogo wa watangulizi wao
60%
40%
6
Mafanikio ya wanasiasa mahiri
72%
28%
7
Vyama vya siasa kuwapa nafasi vijana
59%
41%
8
Uwezo wa kielimu, hasa wanapohitimu shule na vyuo
47%
53%
9
Kukubalika kwa vijana
63%
37%
10
Kutumiwa na wanasiasa wakongwe wanaotaka kuwa na watetezi wa maslahi yao
33%
67%

4.3 Wanasiasa vijana na misingi ya Utawala Bora
Utafiti huu ulitaja mambo ya kuzingatiwa katika hali ya kawaida ili kutambua endapo misingi ya utawala bora imepewa nafasi katika utafiti huu. Mambo ya msingi yalikuwa kujua ni kwa kiasi gani wanasiasa vijana wanafuata misingi ya utawala bora wakiwa katika nyadhifa za kisiasa. Kwa vigezo vya utafiti wetu, mambo yaliyopewa kipaumbele ni endapo hawajihusishi na vitendo vya rushwa (23%), wanapinga na kukemea wala rushwa (67%), wanatumia mbinu shirikishi katika utawala (42%), wanaweza kutengeneza mfumo wa kiuwajibikaji (31%), uwazi (45%) na kufuata misingi ya utawala wa sheria (17%).

4.5 Matarajio ya Wananchi kwa Wanasiasa Vijana
4.5.1 Uwezekano wa Wanasiasa vijana kuendelea kushikilia nafasi zao uchaguzi Mkuu 2015
Wananchi walipata fursa kupitia utafiti huu, kutoa mtazamo wao na maoni kuhusiana na Matarajio yao kwa wanasiasa vijana katika nafasi ya udiwani. Katika sehemu ya kwanza ya dhana hii, wananchi wametoa maoni yao kuhusiana na wanasiasa hawa kuendelea kushikilia nafasi walizo nazo katika uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015. Mtazamo wa wananchi kwa kufuata vigezo vya utafiti wetu ni kwamba waliosema watarejea wote (21%), Sio wote lakini zaidi ya nusu (23%), nusu yao (11%), robo yao watarejea (6%), hawatarejea katika nafasi zao hata kidogo (33%) na sijui (5%).
Upande wa Ubunge, wananchi walikuwa na maoni tofauti na yale ya udiwani. Matokeo huonyesha kuwa 63% wanasema wabunge vijana wote watarejea katika nafasi zao za kuchaguliwa; 20% wansema watarejea zaidi ya nusu, 4% wanasema nusu yao watarejea, 2% watarejea robo, 4% hakuna atakayerejea tena katika nafasi yake na 7% hawajui. Maoni haya yamewekwa katika kielelezo cha mchoro kama ifuatavyo:

Sababu mbalimbali zimetolewa kutokana na maoni ya wananchi kwa upande wa ubunge na upande wa udiwani, kila upande kwa nafasi yake. Jedwali lifuatalo linaelezea sababu za kurejea na kutorejea kwa wanasiasa vijana katika nafasi zao. Kwa upande wa udiwani sababu kuu zilizopelekea 21% kupendekeza kuwa watarejea katika nafasi zao hutokana na kujituma, kutekeleza ahadi zao na kuwa na uongozi shirikishi katika kutoa taarifa za maendeleo kwa wananchi. Kwa upande wa ubunge, 62% waliosema watarejea katika nafasi zao uchaguzi mkuu ujao wametoa sababu kuwa wanapigania wananchi, maslahi ya taifa na harakati zao zinaonekana bungeni katika sakata za ufisadi ikiwamo Richmond na Escrow.
Pale ambapo 33% ya wananchi wamesema kuwa viongozi vijana wanasiasa hawatarejea katika nafasi ya udiwani tena wametoa sababu kuwa ni kutowashirikisha wananchi taarifa za maendeleo, kuwepo wagombea wanaokubalika zaidi watakaogombea uchaguzi mkuu wa 2015 na pia hali ngumu ya maisha walio nayo madiwani kwa kuishi kwa posho na sio mishahara yenye tija ukilinganisha na wabunge. Kwa upande wa maoni toka kwa 4% ya wananchi kuwa wabunge vijana hawatorejea nafasi zao, sababu ni kwamba hawajatimiza ahadi zao kwa wananchi walizozitaja kuwa ni barabara za vijijini, huduma za maji afya na ajira kwa vijana.

4.5.2 Mtazamo wa Wananchi kukubali Rais kijana
Matokeo yanaonyesha kuwa wananchi wapo tayari kukubaliana na Rais kijana endapo vyama vya siasa vitapendekeza mmoja wa wanasiasa vijana katika nafasi hiyo. Kukubalika huko kumepokelewa kwa viwango tofauti, ambapo 82% wamesema atakubalika, 11% wamesema hatakubalika, 7% wamesema hawajui. Maoni haya yamewekwa katika kielelezo chini.


4.5.3 Wanasiasa Vijana wanaopewa nafasi kubwa endapo watasimamishwa na chama tawala
Katika utafiti huu, tumetoa nafasi za kila mhojiwa kupendekeza wanasiasa vijana watatu kwa nafasi ya Urais anaodhani kuwa wakisimamishwa na chama tawala wana uwezo wa kutetea ilani ya chama, wana uwezo wa kutetea sera za chama na kuhimili ushindani wa wapinzani na kukipelekea chama tawala kushinda katika uchaguzi Mkuu wa 2015. Kati ya wote waliohusishwa katika kutoa maoni, ni 78% tu waliotaja wanasiasa vijana, huku 13% wakitaja wasio vijana na 9% wakisema hawaoni kijana anayefaa kwa nafasi hiyo.
Kwa kutumia mapendekezo yaliyotolewa na 78% ya wananchi waliohusishwa katika utafiti huu, wanasiasa vijana 8 wamependekezwa na kila mmoja kupata asilimia kadhaa ya waliotoa maoni. Wanasiasa vijana hao ni Mwigulu Nchemba 38%, Emmanuel Nchimbi 24%, William Ngeleja 11%, Lazaro Nyalandu 10%, Hamisi Kigwangala 7%, Deo Filikunjombe 5%, Esther Bulaya 2%, Wengine Wasio vijana 13, Hakuna anayefaa 9%. Matokeo haya yamewakilishwa katikakielelezo kinachofuata kama ifuatavyo:

4.5.4 Wanasiasa Vijana wanaopewa nafasi kubwa endapo watasimamishwa na vyama vya Upinzani na ukiwamo umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa)
Kwa upande wa wanasiasa vijana kutoka chama cha upinzani na kupitia vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), utafiti huu ulitoa nafasi tatu za kupendekezwa majina ambayo kila mhojiwa alipendekeza majina ya Wanasiasa vijana akifahamu kuwa wana uwezo wa kutetea sera za vyama vyao na ambao wakitokea kupendekezwa na vyama vyao kugombea nafasi ya Uraisi, wanangekubalika zaidi kwa wananchi.
Matokeo yanaonyesha kuwa ni 77% tu yawahojiwa walipendekeza majina ya vijana hao, huku 16% wakisema hawaoni kijana kutoka upinzani na hata katika umoja wa vyama vinavounda umoja wa katiba ya wananchi (UKAWA), na 7% wakisema hawajui. Wanasiasa waliopendekezwa na wananchi katika utafiti huu ni James Mbatia (15%), Zitto Kabwe (18%), Tundu Lissu (11%), Halima Mdee (6%), David Kafulila (9%), Julius Mtatiro (7%), John Mnyika (11%), Joshua Nassari (3%) na Moses Machali 6% na waliosema hawajui wakiwa 7%. Matokeo haya yamewakilishwa katika kielelezo kinachofuata.


Katika sehemu hii ya ripoti, uchambuzi wa waliopendekezwa unaweza uwe umeathiriwa na mambo mengi ikiwa ni pamoja na mazingira na mwenendo wa kisiasa wa kila aliyependekezwa.
Awali ya yote, waliopata nafasi za juu katika mapendekezo haya, walishaonyesha dalili za kutangaza nia ya kuwania Urais, na hivyo yawezekana kuwa wamejenga ushawishi kwa kiwango fulani, kiasi kinachoweza kuathiri maoni yaliyopendekezwa.
Pili, historia a siasa nchini imekuwa ikipita katika hatua mbalimbali kufuatia matukio kadhaa yahusuyo maslahi ya taifa, rasilimali za nchi, ufisadi na hata uwajibishwaji kisiasa. Vijana wanasiasa vijana wamehusika aidha katika kuibua hoja, au kuwajibishwa dhidi ya hoja zenye maslahi kwa taifa na wakati mwingine wakiwa mstari wa mbele kupiga vita ufisadi. Matukio haya yanweza kuwa sababu za nafasi za wanasiasa mbalimbali katika utafiti huu.
Tatu, kwa wanasiasa wa chama tawala wenye nyadhifa za uwaziri au naibu waziri, wamekuwa katika nafasi za juu, ikiwa ni sababu inayoweza kuwafanya wajulikane sana, na hata shughuli zao za kiuwaziri ama naibu waziri zikiwapa nafasi kubwa ukilinganisha na wasio mawaziri na manaibu waziri. Sababu hii inawapa nafasi Mh. Lazaro Nyalandu (Waziri wa Maliasili na utalii), Januari Makamba (Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia), Mwigulu Nchemba (Naibu Waziri wa Fedha), Emmanuel Nchimbi (aliyewahi kuwa Naibu Waziri na Waziri), William Ngeleja (aliyewahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini).
Nne, nafasi za waliopendekezwa katika vyama vyao, mfano kwa kupitia chama cha tawala, wabunge, manaibu mawaziri na mawaziri ni wajumbe wa Halmashauri kuu ya chama, ni wajumbe wa Sekretarieti ya chama, na hata kwa wanasiasa vijana wa vyama vya upinzani. Utendaji wao katika chama, ushiriki wao katika kampeni zinazohusisha vyama vyao hadi kuwapelekea ushindi ni sehemu ya mambo yayowashawishi wapiga kura na wanachama walioshiriki katika kutoa maoni haya kadiri ya uchambuzi.
Pia, harakati za shughuli za kibunge ikiwa ni pamoja na umahiri wa wabunge vijana kutoa hoja na hata kutetea hoja zao kupitia vyombo vya habari ambapo wananchi huweza kuwajua na kuwatathmini. Fursa hii inawapa nafasi kubwa wabunge wa upinzania wengi hawajatangaza nia na hawategemei ila harakati zao bungeni zimekuwa kichocheo kwa wananchi kwa kiasi kikubwa. Ni dhahiri kwamba licha ya Mbunge Zitto Kabwe kuwa nje ya uongozi wa Chama, amepata nafasi kubwa katika mapendekezo ikiwa ni pamoja na nafasi aliyonayo katika kuongoza kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali.
Kutumiwa na chama katika kampeni za chaguzi ndogo nayo inaweza kuwa uwanja wa kisiasa kwa wanasiasa vijana kweza kufahamika, hasa pale baadhi yao walipotokea kuwa mstari wa mbele kuendesha kampeni zilizovipa vyama vyao ushindi.
Pamoja na mapendekezo ya wananchi, ni dhahiri kwamba wao kwa kutofahamu au kwa kuridhishwa na utendaji wa wanasiasa vijana kadiri ya mapendekezo, hawakuweza kuzingatia umri wa mgombea Urais kadiri inavyopendekeza Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa sababu hiyo, wapo wanasiasa vijana wasiofikisha umri wa kuwania Urais, lakini kwa kuwa mapendekezo haya ndio yanayojenga kila mwanasiasa, utafiti huu umeyawakilisha kadiri ya mapendekezo.

4.5.5 Wakishindanishwa vijana wote bila kujali itikadi za vyama
Matokeo ya utafiti huu unaonyesha kuwa endapo watashindanishwa vijana wote bila kujali itikadi zao za vyama, matokeo yakaonyesha kuwa Mwigulu Nchemba 27%, Zitto Kabwe 19%, Januari Makamba 16%, James Mbatia 11%, Emmanuel Nchimbi 10%, Tundu Lissu 5%, Lazaro Nyalandu 4 wakati 8% hawajui. Matokeo haya yameonyeshwa katika kielelezo kinachofuata.


4.5.6 Ungefanyika Uchaguzi leo vyama vyote vikiwa vimesimamisha wanasiasa vijana
Sehemu hii ya utafiti, imejumuisha vyama vyote bila nchini, na maoni ya wananchi yakionyesha kuwa 53.4% ya wananchi wangepigia kura Chama cha Mapinduzi (CCM), 27.3% ya wananchi wangepigia kura Chama cha Demokrasia na Mandeleo (CHADEMA), 7.3% wangepigia chama cha Wananchi CUF, 4.4% wangepigia NCCR-Mageuzi, 0.6% TLP na 7% wakisema hawajui. Matokeo ya sehemu hii yapo katika kielelezo kinachofuata.


1 Jacob Daniel Kateri, born in 1978 witnessed politicians contesting coming to see my father for an entry strategy, but I never saw youth in 1985 to 1995 as it is today.
2 Late Daniel S. Kateri (1932-2007) in his life-time having worked to his retirement as civil servant' was such a sage who with his wisdom made our home a landing hub for most politicians who intended to contest for various political posts in Same district, ward and even village.
3 "Viti Maalumu Wanawake" refers to special seats reserved for women in decision making bodies.
4 ICT & Media in Tanzania Education System: An Exploratory Study towards understanding ICT & Media Threats among Urban Students in Tanzania (The study underway was granted research permit from COSTECH on 28th April, 2014.
6 The UN has long recognized that Youth are major human resources for development and key agents for social change, economic growth and technological innovation.
7 Traditional thinking that "Vijana ni taifa la kesho" translated to "Youth are the nation of tomorrow"
8 After 1980s youth contests led to rethinking that "Vijana ni taifa la leo" translated to "Youth are the nation of today"
9 Frantz Fanon once contended, "each generation must out of necessity, discover its mission, fulfill it, or betray it".
10 American President Barack Obama remarks at the US-Africn Leaders Summit that focused on, "Investing in Africa's Future"
11 Koffi Annan, once said that No one is born a good citizen, no nation is born democratic. Rather both are processes that continue to evolve over a lifetime. Young people must be included, since the society that custs itself off from its youth servers, is condemned to bleed to death"
12 UNDP (2012), Enhancing Youth Political Participation throughout Electoral Circle, A Good Practice Guide.
13 Youth should be given a chance to take an active part in the decision making at local national and global levels" said, Ban Ki-moon.

14 SPSS statistical Package for Social Science Studies

--
Send Emails to wanabidii@googlegroups.com
 
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
 
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Wanabidii" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com.
For more options, visit https://groups.google.com/d/optout.

Share this :

Related Posts

0 Comments