[wanabidii] UJUMBE WANGU KWA VIONGOZI WA DINI MINTARAFU SIASA ZA CHUKI, FITINA , HILA, MANYANYASO NA ZA KIBABE

Monday, August 04, 2014

UJUMBE  WANGU  KWA VIONGOZI WA DINI MINTARAFU SIASA ZA CHUKI, FITINA , HILA, MANYANYASO  NA ZA KIBABE NCHINI TANZANIA.

Na padre Baptiste Regina Mapunda (M.afr)

frmapunda91@gmail.com

Ni ukweli usiopingika kwamba  viongozi wa dini ni viongozi wa imani katika madhehebu yao lakini pia ni viongozi wa jamii  pana pia, tena ni viongozi wenye mamlaka ya Kimungu. Viongozi hao kwa kawaida wanaaminika sana katika jamii hata ya Watanzania.  Biblia takatifu   inamwonyesha  nabii  Jeremiya  kama  mtu  aliyeteuliwa na Mwenyezi Mungu na kukabidhiwa mamalaka ya kubomoa na kujenga.

 Nabii huyu pia alipewa mamlaka ya kukemea hata watawala wabovu wa jamii kama ilivyo jamii ya Watanzania ambayo inatafunwa na maovu ya watawala kila kukicha utasikia mara EPA, ESCROW, mafuta machafu, umeme umepand kiholela nakadhalika.

Wito wa nabii Jeremiya  ilihusu hasa kuwakemea Waisraeli waliojikita  katika  kutenda maovu baada ya kuacha njia ya Bwana, njia ya amani, upendo,njia haki na uhai. Hii pia ni kazi ya viongozi wa dini wa Tanzania  katika nyakati hizi  za sasa.

 Mahali tulipofikia  sasa jamii ya  Watanzania  inahitaji manabii wa kuonyesha njia, kuonyesha mwanga, na hasa kuwakosoa  watawala ambao wanaonekana kujifanya wapo juu ya sheria na kuonekana kama ni 'miungu watu" wakati  wao  pia ni wanadamu.

Katika makala hii nitaongelea  kwa kifupi tu juu ya matatizo yanayowakabili viongozi wa dini nchini Tanzania  hasa katika kipindi hiki cha migogoro ya ardhi, mauaji, ukandamizaji, wizi wa mali ya umma, utapeli  na mvurugano wa katiba mpya uliosababishwa na Rais pamoja na chama  chake cha CCM.

 Mambo  ninayoyaandika ni tafakari na uchambuzi wangu mimi mwenyewe   hata kama mambo mengine yanaweza yakawa yamesemwa na baadhi ya watu hii haijalishi  mathalani kama alivyosema  Tundu Lisu kwamba baadhi ya viongozi wa dini wanakula rushwa ili kupotosha mambo mimi sioni kama hayo ni matusi inawezekana  kuwa ni  hali halisi kama navyofahamu. Shida ninayoiona nchini mwetu sasa ni hii ya watu kuhruza ukweli kuwa uwongo, na ukweli ni matusi na chuki kitu ambacho hakitasaidia  maendeleo na mstakabhali wan chi yetu bali nu migongano katika jamii yetu.

Kwwanza je, kuna kiongozi yeyote wa dini aliyesimama na kusema  tumetukanwa? Sivyo, bali ni  chuki za kisiasa  ndizo zinapelekea  watu kupandikiza maneno kama hayo. Je, kusema kamba   padre mapunda  ni mwongo ni kumtukana labada ndivyo  anavyoonekana na wala hawezi kukasirika hata siku moja.Tabia  ya mtu haitegemei watu wanasema mimi, bali  yeye mwenyewe yukoje.

 Hili ni tatizo katika jamii yetu  watu kupenda kugombanisha watu. Naamini viongozi wa dini  wanabusara ya kutosadiki maneno kama hayo  wakijua kwamba  kazi ya kitume inachangamoto nyingi na mojawapo ni kutukanwa, kudharau na kutungiwa uwongo. Pia viongozi wa dini lazima watambue kwamba  siasa za Tanzania ni za majitaka na pia za kuchafuana na hivi ugonjwa huu upo katika jamii nzima zikiwamo taasisi za dini pia.

Kwa upande  wa viongozi wa dini wenyewe mimi naona kama kuna ndoa na serikali iliyopo madarakani yaani ya kuwa  watiifu hata pale  serikali inapoboronga  wanashindwa kuiambia wazi wazi. Kumbuka viongozi wakuu wa dini (Maaskofu, Wachungaji, mashekhe  enz za Mwalimu  walikuwa na heshima kubwa hata katika mambo ya kisiasa na  walisikilizwa.

 Inawezekana  viongozi hao walikuwa wamejitenga na kujishirikisha sana na mambo ya kisiasa. Mfano leo unamwalika waziri  anakuwa mgeni rasmi katika harambee yako ya kuchangia  ujenzi wa kanisa yeye anakuletea million mia tatu pmaoja na rafiki zake, je hapo hujahongwa?

 Mambo kama hayo yanawafunga midomo na hivi kushindwa kuwakemea viongozi hao wanapoboronga au serikali inapokiuka sheria. Askofu ni mtu mkubwa na jimbo lina watu wengi sana maskini na matajiri, je kweli inashindikana kuongoza harambee bila wanasiasa? Hili ni doa mojawapo kwa upande wa viongozi wa dini  na wanasiasa wanatumia kama njia   mojawapo ya kuwaziba midogo yenu. Je,bado hatujapoteza nafasi yetu katika masuala ya jamii hasa siasa?

Pia naona  kuna unafiki kwa serikali na hivi kutoa taswira ya kushirikiana na mafisadi na hili nimeshalisema mara nyingi hata likanijengea chuki  hata hivi napenda tena kulirudia leo  kwa manufaa yetu sote kama viongozi wa dini. Je, kwa mantiki hii wananchi wakisema sisi tumepoteza nafasi yetu katika siasa nchini Tanzania  tutawajibu vipi?

Viongozi wa dini  wanaonekana  kuamini kinachosemwa na viongozi wa serikali  ya CCM na kukifuata hata kama pengine kina madhara kwa taifa. Mfano halisi ni propaganda ya CCM kwamba waliopotosha  mchakato wa katiba mpya ni UKAWA, hivi warudi bungeni. Lakini  wakati wakipigia kelele UKAWA mbona  hawajaisema kisawasawa serikali ya CCM kulikoni, wananchi wengi wanahoji kwanini kuegemea upande mmoja. Kama  wamefanya vikao na viongozi wa CCM kwa nini basi hawajakutana na viongozi wa UKAWA?

Pia wananchi wanawasiwasi kwamba  viongozi wa dini  ni waoga, na wana hofu kwa CCM, na hili wengi  wanalisemea wazi wazi. Je, viongozi wa dini tunategemewa kuwa na ujasiri wa kusema ukweli pale ambapo watu wote wanakaa kimya ili uwongo usitamalaki na hivi kumwinua shetani. Ni vema viongozi wa dini wakajitathimini upya kuhusu suala la hofu kwa CCM. Au viongozi hao hawajiamini katika  utendaji wao kwamba wanasauti ya Mungu ambayo inapashwa kusikika  hasa katika kipindi kama hiki.

 Je, wanahofia kutekwa , au wanahofia kushambuliwa  na waandishi wa habari pamoja na kujenga uadui na serikali ya CCM? Sisemi kwamba viongozi wa dini tuanzishe mapambano sivyo. Hata hivi mapambano tayari yapo katika jamii, sasa  tunafanya nini kama viongozi wa dini? Waingereza wanasema " if you cant  beat them, then join them" (Usipoweza kupambana nao , basi ungana nao). Sisi tumechagua upane upi?

Wananchi wanaona tatizo jingine la baadhi ya viongozi wa dini katika nyakati hizi ni kushiriki unafiki na pengine  hata uwongo wa serikali  ya CCM  kama tunavyoshuhudia  siku hizi juu ya upotoshwaji wa nani kavuruga Bunge tukufu la Kutunga katiba nchini. Rais na wanaCCM  wanajua walichofanya kwa kung'ang'ania  sera zao na kuacha kujadili  Rasimu ya maomi ya wananchi na hicho ndicho chanzo halisi cha mkwamo wa katiba hii.

 Propaganda za CCM  zimegeuza kibao na kuwabambikiza UKAWA ndiyo wanaokwamisha  upatikanaji  wa katiba eti  kwa sababu wamesusia bunge hilo. Na kwa hiyo UKAWA wanamapepo (sijui ni mangapi) wanapaswa  kuombewa, sijasikia kama viongozi wa dini wamewaombea UKAWA au la. Lakini imesikika miito mingi kutoka kwaa viongozi wa dini kuwasihi UKAWA warudi bungeni  tena bila mashariti kujadili katiba mpya kupitia rasimu ya Warioba.

Viongozi wa dini kuwasihi tu UKAWA kurejea  na kujadili rasimu ya Warioba  bila kuwakemea CCM  kuacha  kuchakachua  moani ya wananchi haitoshi na si sahihi.   Hapa inaonekana wazi kwamba shida mojawapo ya viongozi wa dini ni kutotambua kwamba katika uwanja wa siasa kuna shida kubwa sana ya kubadilisha uwongo kuwa  ukweli na kutaka na hata kulazimisha  wananchi waamini hivyo.

Mkwamo wa katiba mpya ni mfano mzuri ambao kila mtu anajua nani kaharibu, yaani inakuwa kama baba anamlazimisha mtoto wake wa miaka mitano kwenda kulala akimwaminisha  saa tano asubuhi ni usiku, wakati mtoto naye anajua ni  bado mchana. Je hili linawezekana? Mtoto atakwenda kulala kama haelewi maana ya mchana na usiku, au atakwenda sababu ni mwoga anaogopa kupigwa, namna nyingine  watoto wa siku hizi basi utaishia kuchekwa kwa sababu umebugi men.

Viongozi wa dini ni muhimu mujielimishe juu ya mkwamo wa mchakato wa katiba nchini Tanzania na wajibu wenu katika kusaidi kukwamua kwa kusimamia ukweli na siyo kuwa upande mmoja au kukaa kimya kabisai. Viongozi wa dini lazima wajue kwamba Bunge la Katiba linaendeleza mchakato  na siyo kuanzisha upya kwa kutoa maoni tena bungeni. Hii hatua ya kutoa maoni imepita na tume imeshapendekeza muundo ambao ni waserikali tatu  ambayo ni maoni ya wananchi.

Sasa uchakachuaji huu wa maoni ya wananchi na  Serikali ya CCM ni alama wazi ya kulewa madaraka. Mara moja niliandika katika makala zangu kwamba ulevi ni ugonjwa unaomfumba mtu asijitambue ni nani na anafanya nini.  Naomba  kwa manufaa ya kutoa elimu nirudie tena kwamba  katika dunia ya leo hakuna ugonjwa au ulevi mbaya kama wa "MADARAKA" katika jamii yeyote ile hata kama ni taasisi  ya  madhehebu ya dini. Hayo tunayashuhudia kila kukicha dunia nzima.

Inaonekana wazi kwamba CCM haitaki katiba mpya wala haitaki tume huru ya uchaguzi, bali inataka maigizo tu ya katiba mpya na tume huru ya kisanii.

 Hayo tuyakatae wote kwa nguvu, akili na moyo mmoja na  ndiyo wanayoyakataa  UKAWA. Je, viongozi wa dini hawaoni hoja hizo? Sisi wengine kwa kuandika ukweli na kuonekana kama tunashabikia UKAWA  tunatukanwa  sana lakini kwa sababu ya ukweli tutaendelea  kusimamia ukweli hata kama watu hawaupendi. Yesu alitufundisha kwamba " Ukweli utatuweka huru."

Jamii ya Watanzania  ilitegemea viongozi wa dini iwaokoe na maovu, fitina, chuki,manyanyaso na ubabe wa serikali ya CCM, lakini sasa viongozi hao  nao wanaonekana wamezama katika matope ya serikali hiyo hiyo. Wananchi  waelewa hawaelewi maana yake ni nini na wanaoana kama viongozi wa dini  wanajikosha (Kujikomba,kujipendekeza) kwa serikali ya  mafisadi na kuonekana kama nao kunufaika na ufisadi huo.

Kinachotakiwa viongozi wa dini lazima tujitenganishe na maovu kama hayo.Na wale  viongozi wa dini walioko katika Bunge la Katiba wasimamie ukweli na kuacha kuungana na wale wanaotaka kuchakachua rasimu ya maoni ya wananchi kiubabe. Wananchi sasa  wanajiuliza dawa ni nini kama viongozi wao wanaona hawawasaidii kutetea  katiba na mfumo wa haki, upendo, na usawa katika jamii?  Je, hii siyo alama ya kupoteza nafasi zenu  katika medani  za siasa nchini Tanzania?

Wananchi wanaona sasa dawa ni moja tu yaani  kuelimishana na kujisimamia wenyewehasa huko vijijini  na kuiambia ukweli serikali ya CCM pamoja na viongozi wa dini kwamba  tunaelekea pabaya. Na zaidi ya hapo wanaona kamba umaskini, maovu, mauaji, utesaji, utapeli, wizi wa mali ya umma, mikataba mibovu inayotesa  wananchi ikiwamo ya gesi kule Mtwara inasababishwa na watawala wa serikali ya CCM.

  Wananchi  wengi wamechoka na ahadi hewa na kilichobaki ni ubinafsi na kulindana. Ajira ni shida kwa vijana isipokuwa kama wewe ni mtoto wa kigogo au unamjua yeyote ngazi ya juu au uhonge. Wananchi  wanaona sasa ni muda mwafaka kuachana na CCM kwani imeshindwa kuwakwamua katika uamaskini  wao  pamoja na kwamba nchi imejaa rasilmali kibao nchini nzima.

 

 Mtazamo huu ni wa wananchi wengi ingawaje hawana pa kusemea.  Mimi binafsi naona ni changamoto kubwa sana kwetu sisi  viongozi wa dini hasa  katika kipindi hiki cha kueelekea  uchaguzi wa serikali za mitaa na uchaguzi mkuu mwaka 2015.  Je  sisi viongozi wa dini bado tuna nafasi yetu katika kusaidia kuendesha siasa safi  na zenye sera nzuri nchini Tanzania hasa kwa ushairi, kukemea maovu,na kwa uwepo wetu.?

 Kazi mojawapo ya viongozi je siyo kuwajengea  viongozi  wetu wa kisiasa hasa watawala  roho ya uchamungu na kuongoza kwa kufuata  misngi ya haki, usawa, demokrasia na utawala bora kwa wote bila kujali vyama vilivyopo. Wahenga hunena kwamba ' utavuna  ulichopanda'  kama ulipanda chuki utavuna chuki, na kama ulipanda 'upendo  haki na amani  basi wewe  utavuna upendo,haki na amani' Mungu ibariki  Tanzania  na viongozi wote wa dini.

--
Send Emails to wanabidii@googlegroups.com
 
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
 
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Wanabidii" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com.
For more options, visit https://groups.google.com/d/optout.

Share this :

Related Posts

0 Comments