Wapenzi wasomaji, wiki iliyopita makala hii ya uchambuzi kuhusu Mapendekezo ya Kamati za Bunge Maalumu haikutoka kutokana na sababu za kiufundi.
Tunaomba radhi kwa usumbufu uliojitokeza na tunawatakia usomaji mwema wa makala hii inayochambua kwa undani mapendekezo ya Kamati za Bunge Maalumu na kuainisha jinsi yanavyoweza kuleta athari katika Muungano wa Tanganyika na Zanzibar – Mhariri.
Ni kweli kwamba Bunge Maalumu lilitumia muda mwingi baada ya kumaliza kanuni kujadili sura ya kwanza na sura ya sita na kujiridhisha kumaliza suala la muundo wa muungano.
Uhalisia ni mbali kabisa na ukweli huu, ili kuujadili muundo wa muungano kama msingi ilipasa sura ya kwanza, sita na kumi na tano kusomwa na kujadiliwa kwa pamoja (in tandem). Rai yangu kwa wajumbe wa Bunge Maalumu ni kuhakikisha wanasoma ibara na sura zinazoendana kwa pamoja ili kupata mantinki na kutoa maboresho stahiki.
Kumekuwapo hoja kwamba ufike wakati suala la muungano maadamu limeleta ubishani mkubwa na sintofahamu nyingi basi tuliweke kando na tujadili masuala mengineyo katika rasimu. Hoja hii yaweza kuwa ina nia njema, lakini kwa hakika haitaarifiwi na uhalisia.
Taifa letu ni Muungano wa zilizokuwa nchi mbili huru kabla ya mwaka 1964. Nchi hizi zilipoungana ziliundwa mamlaka tatu tofauti kikatiba, kwa maana ya Mamlaka inayohusika na Mambo ya Muungano, Mamlaka inayohusika na mambo yasiyo ya Muungano ya Zanzibar na Mamlaka inayohusika na Mambo yasiyo ya Muungano ya Tanzania Bara.
Unapoandika Katiba ya Mamlaka ya Jamhuri ya Muungano ni lazima uzingatie masuala ambayo kiasili ni ya Muungano na huwa ni majukumu ya kidola (sovereign functions).
Hoja ninayojaribu kuijenga hapa ni kwamba kwa asili ya nchi yetu, suala la muungano huwezi kulikwepa unapozungumzia Katiba Mpya. Kabla hatujafahamu suala la maji, barabara, kilimo, elimu, afya na masuala mengine ya kimaendeleo, lazima tumalize suala la muundo wa Muungano. Ni muundo wa Muungano ndiyo utatupatia msingi wa kuenenda (framework) katika masuala ya muungano (majukumu ya kidola) na masuala yasiyo ya muungano (yote yahusuyo ustawi na maendeleo ya watu).
Tofauti kubwa kati ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba na Bunge Maalumu ni kwamba Tume ilipoanza kazi haikuwa na hoja mfukoni bali ilipaswa kisheria kupokea maoni kutoka kwa wananchi. Bunge Maalumu kisheria linapaswa kupokea hoja kutoka Tume ya Katiba, kisha kuijadili na kuipitisha.
Tume ya Katiba ilipata fursa ya kusikiliza na kupokea maoni ya wananchi katika hoja mbalimbali na hata ilipofika wakati wa uchambuzi na majadiliano ndani ya Tume, wajumbe wake walijiwekea utaratibu wa kujadili masuala mengineyo na kisha kulitizama suala la muungano.
Ni wazi kwamba Bunge Maalumu halina fursa hiyo, Sheria ya Mabadiliko ya Katiba inalielekeza Bunge Maalumu kupokea hoja kutoka kwa wananchi kupitia Tume ya Katiba. Sheria inaendelea kulielekeza Bunge Maalumu katika kifungu cha 25(2) kwamba msingi wa majadiliano ya Bunge Maalumu ni Rasimu ambayo imewasilishwa na Tume ya Katiba.
Vyombo vya utendaji vya Jamhuri ya Muungano
Kamati namba tatu chini ya uenyekiti wa Dk Francis Michael katika taarifa yake ukurasa wa 13 inatoa pendekezo la kuendelea kuwa na serikali mbili na shughuli za mamlaka ya nchi kusimamiwa na kutekelezwa na vyombo viwili vya utendaji, vyombo viwili vya kutunga sheria na vyombo viwili vyenye dhamana ya kutoa haki. Pendekezo hili kama lilivyo halina tofauti na hali ilivyo katika Katiba inayotumika sasa ya mwaka 1977 toleo la 2005.
Katika pendekezo hili najiuliza kama kamati imejiridhisha na uzoefu wa zaidi ya miaka 40 katika muundo wa serikali mbili na kuzingatia changamoto ambazo zimejitokeza kabla ya kupendekeza kuwapo kwa serikali mbili. Nachelea kusema kwamba kamati imegubikwa na ile dhana ya ukinzani wa mabadiliko kutokana na mazoea.
Kamati namba tatu inaendelea kujenga hoja katika ukurasa wa 14 kwa kusema kwa maoni ya wajumbe walio wengi zipo baadhi ya changamoto katika mfumo wa serikali mbili ila kinachohitajika ni kuzitafutia ufumbuzi, kama kazi hiyo inavyoendelea na siyo kuwa na mfumo wa shirikisho ambao utakuwa na matatizo makubwa zaidi kuliko tuliyonayo hivi sasa.
Hoja ya uchache wa changamoto haina ukweli na ni upotoshwaji, naomba turejee taarifa ya utafiti kutoka Tume ya Katiba katika suala la muungano katika ukurasa wake wa 32-34, yameainishwa maeneo zaidi ya 40 yenye changamoto katika Muungano. Mambo haya siyo mageni, yako na yanajulikana, kujiaminisha kwamba ziko changamoto chache ni ishara ya ama kutokuelewa uhalisia (ambao uko vitabuni) au ni kuonyesha dalili za kutokuwa na dhamira ya dhati ya kuzifanyia kazi changamoto hizo.
Nieleze kwa ufupi sifa na tabia za miundo mbalimbali pamoja na namna ya kwenda na mambo ya muungano na yale yasiyo ya muungano.
Muundo wa serikali moja huwa na sifa ya kushughulikia mambo yote na tabia mojawapo ni uratibu, usimamizi na ufuatiliaji wa jumla kutoka Mamlaka Kuu (Supreme Authority).
Muundo wa shirikisho huwa na sifa ya kuwa na mambo machache ya muungano pamoja na ngazi mbili za usimamizi, uratibu na ufuatiliaji. Ngazi ya kwanza ni serikali ya muungano au shirikisho kwa mambo machache yenye asili ya majukumu ya kidola na ngazi ya pili ni serikali za washirika kwa mambo yanayosalia ambao huwa na asili ya kimaendeleo zaidi.
Bado katika muundo wa shirikisho unaweza kuwekwa utaratibu ambao unahakikisha kwamba serikali ya muungano inakuwa na mfumo mahususi wa kuratibu, kusimamia na kufuatilia ustawi wa masuala ya maendeleo hata katika ngazi za nchi washirika, mfano ni pendekezo la Rasimu ya Katiba Mpya juu ya uwepo wa Tume ya Uhusiano na Uratibu ambayo kimsingi ina kazi hiyo, ibara ya 111(1)(b) inasema Tume ya Uhusiano na Uratibu ndiyo chombo maalumu cha Jamhuri ya Muungano chenye dhamana ya kusimamia, kuratibu na kuhakikisha kwamba kuna kuwiana kwa sera na sheria za nchi washirika katika mambo yasiyo ya muungano.
Muundo wa Mkataba huwezesha mahusiano katika maeneo fulani yanayokubaliwa na nchi zinazoingia katika mkataba. Sifa ya Muungano wa Mkataba huwa ni lazima uingiwe na mataifa mawili au zaidi yaliyo huru (sovereign states). Kwa mazingira ya hapa kwetu ni kurudi nyuma ya mwaka 1964. Kwa mtizamo wangu huko hatuko na binafsi sidhani kama tunapaswa hata kufikiri kwenda huko.
Sifa kubwa mojawapo ya muundo wa serikali mbili ni kuwapo kwa mambo mengi ya muungano kama ilivyo kwenye Katiba ya 1977 au zaidi. Sifa nyingine ni uwezo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano kuwa na mamlaka na madaraka ya usimamizi na ufuatiliaji wa ufanisi kwa masuala yasiyo ya muungano upande wa Zanzibar sambamba na Tanganyika ili awe na uhusiano wa moja kwa moja na raia wa Tanzania waishio Zanzibar kama ilivyo kwa wale wa Tanganyika.
Jambo hili linabishaniwa vikali na serikali zetu mbili hasa kutoka upande wa Zanzibar, huu ndiyo ukarabati usiowezekana.
Mambo ya Muungano
Kamati namba tatu katika taarifa yake ukurasa wa 21 inakubaliana na pendekezo la rasimu kwamba mambo ya muungano yabaki saba, pendekezo hili linapaswa lisomwe pamoja na pendekezo la serikali mbili katika ukurasa wa 13.
Kwa mtu yeyote anayejua masuala ya muungano lazima aone tatizo la msingi hapa. Huwezi kutaka serikali mbili halafu ukapunguza mambo ya muungano. Kitendo cha kupunguza mambo ya muungano kinakuleta katika muundo wa shirikisho ambao mambo machache yanabaki kwa serikali ya shirikisho (kama kwenye rasimu) na yanayobaki yanakuwa kwa washirika.
Unapokuwa na mambo machache ya muungano ndani ya muundo wa serikali mbili ambapo serikali ya muungano inashughulikia mambo ya muungano na yasiyo ya muungano ya Tanzania Bara au Tanganyika tafsiri yake ni kwamba; Jamhuri ya Muungano ndiyo itakuwa Tanganyika na Zanzibar itakuwa imepachikwa tu katika muungano huu. Kwa maneno mengine tutakuwa tumeweka uhusiano kati ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano katika masuala ya ulinzi na usalama kwa kiasi kikubwa pekee.
Kwa mapendekezo haya ya kamati namba tatu, hayatatuacha tena na nchi moja yenye uraia mmoja bali tutakuwa tumeigeuza Zanzibar kuwa nchi kamili yenye mamlaka yote isipokuwa ulinzi na usalama ambalo litakuwa jukumu ya Jamhuri ya Muungano. Tukifika hapo tutakuwa tunafanana kabisa na uhusiano uliopo kati ya nchi ya Italia na San Marino au uhusiano wa nchi ya Ufaransa na Monako. Narudia huo utakuwa Muungano dhaifu kabisa wa serikali mbili ambao utaendeleza kero na kwa vile una mianya mingi ya udhaifu mwishowe utavunja muungano wetu wa kihistoria.
Itaendelea wiki ijayo.
http://www.mwananchi.co.tz/kolamu/Mapendekezo-yatakayovunja-Muungano/-/1607214/2399508/-/item/2/-/agkd8sz/-/index.html
Send Emails to wanabidii@googlegroups.com
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Wanabidii" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com.
For more options, visit https://groups.google.com/d/optout.
0 Comments