[wanabidii] Waziri wa Mambo ya Ndani aunda kikosi cha kukomesha mauaji ya wazee

Saturday, October 12, 2013
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dkt. Emmanuel Nchimbi ameunda Kikosi Kazi kitakachokuwa na jukumu la Kuratibu  na Kusimamia Ukomeshwaji wa Vitendo vya mauaji ya Wazee, yanayotokea mara kwa mara katika maeneo ya  Kanda ya Ziwa hapa nchini.

Kuundwa kwa Kikosi Kazi hicho kunatokana na kukithiri kwa ongezeko la matukio ya mauaji ya wazee, yanayotokana na imani za kishirikina yanayotokea  katika baadhi ya Mikoa ya Tanzania Bara hususani Kanda ya Ziwa ambayo yamekuwa yakisababisha madhara makubwa katika jamii ya Watanzania. 

Miongoni mwa madhara hayo ni pamoja na Watu kufariki dunia hususani wazee, Matukio hayo kuendelea kuacha makovu 
ya chuki  na hisia  za kulipiza kisasi, Matumizi  ya ziada ya rasilimali  katika kuimarisha miundo mbinu  ya ulinzi na usalama, ikiwemo pia Nchi kupoteza sifa  ya kuwa kisiwa cha amani.

Kikosi Kazi hicho chenye wajumbe kumi (10) ambacho kimeanza kazi tangu  Oktoba Mosi mwaka huu kinaongozwa na Mwenyekiti wake Naibu Kamishna wa Polisi Ernest Mangu ambaye pia ni Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza.

Wajumbe wengine wa Kikosi Kazi hicho ni pamoja na Kamishna Msaidizi wa Polisi Leornard Paul ambaye ni  Kamanda wa Polisi mkoa wa Geita,Kamishna Msaidizi wa Polisi Salum Msangi ambaye ni Kamanda wa Polisi Mkoa wa Simiyu,Kamishna Msaidizi wa Polisi Peter Ouma ambaye ni Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora.

Wajumbe wengine kutoka vyombo vya ulinzi na usalama ni  pamoja na Jacob Mutashongerwa, Gaston Peter Ndwata, Fulcon Nguli, Roman Matemu, na Anna Tegullo.

Hatua ya kuundwa kwa Kikosi Kazi hicho, kitakachofanya kazi kwa muda wa miezi sita ni Mkakati wa Serikali kupitia Jeshi la Polisi kushughulikia ukomeshwaji  wa tatizo la mauaji ya wazee yanayotokea hasa katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa ikiwemo Mwanza, Shinyanga, Geita, Simiyu na Tabora.

Lengo la kuundwa kwa Kikosi Kazi hicho ni kutafuta njia mbadala za kukomesha mifumo  ya kijamii inayoweka  imani za kishirikina zinazosababisha  mauaji katika umri wa wazee ambao wanahitaji kuishi kama raia wengine.

Kikosi kazi hiki kitakuwa na jukumu la kuhakikisha kuwa njia zitakazotumika kukomesha mifumo ya kijamii inayochangia kasi ya kuongezeka kwa mauaji ya wazee zinabadilisha mtazamo hasi wa jamii ambayo badala ya kuwaenzi wazee imegeuka kwa kuwatuhumu kuwa ni watu wabaya na hawafai kuishi na hatimaye kuwaua kikatili kwa visingizio vya imani za kishirikina.

Imetolewa na 
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI,
11Oktoba, 2013

--
Send Emails to wanabidii@googlegroups.com
 
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
 
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Wanabidii" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com.
For more options, visit https://groups.google.com/groups/opt_out.

Share this :

Related Posts

0 Comments