[wanabidii] Tamko la Vijana Wapenda Amani Tanzania - Rais tunayemtaka 2015

Friday, August 02, 2013
RAIS TUNAYEMTAKA 2015

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

UTAMBULISHO

Sisi ni viongozi na baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Vijana Wapenda Amani Tanzania, ambayo ni taasisi ya vijana wazalendo kutoka pande zote za Tanzania, dini zote na vyama vyote vya siasa. Baadhi ya shughuli zetu ni pamoja na kuhimiza amani, upendo, umoja na mshikamano miongoni mwa Watanzania, kufanya shughuli za kujitolea na kuhimiza ujasiriamali na kujitegemea miongoni mwa vijana. Kamati yetu ina mtandao nchi nzima kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu yetu. 

UTANGULIZI

Tumeamua leo, baada ya mjadala mrefu miongoni mwetu, vijana wenzetu na makundi mbalimbali kwenye jamii kutoka karibu kila mkoa wa nchi yetu, kujitokeza na kuchangia katika mjadala wa hatima ya uongozi wa taifa letu. 

Kama mnavyofahamu, mjadala kuhusu hatima ya uongozi wa nchi yetu umekuwa unaendelea kwa muda mrefu sasa. Vyombo vya habari na watu mbalimbali wamekuwa wanajitokeza kutoa maoni yao kuhusu nani wanafaa kuongoza nchi yetu kuanzia mwaka 2015. Majina mengi yametajwa na kujadiliwa tangu Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 ulipokwisha.

Na sisi leo tumeamua kuingia na kuchangia katika mjadala huo. Hata hivyo, katika mijadala ndani ya taasisi yetu na miongoni mwa vijana wenzetu na makundi mbalimbali, tulikubaliana kwamba kuanza na kujadili majina sio njia sahihi ya kuendesha mjadala wa kupata viongozi bora. Sisi tunaamini kwamba namna bora
 zaidi ya kuendesha mjadala huu ni: mosi, kuanza na mjadala wa hali halisi ya siasa nchini na changamoto katika nchi yetu kwa sasa; pili, kujadili mahitaji ya nchi kiuongozi kwa sasa na siku zijazo; na tatu, kujadili sifa au aina ya kiongozi atakayekidhi changamoto za sasa na mahitaji ya sasa na miaka inayokuja. Baada ya hapo ndio tunaweza kujadili majina.

Hali ya Sasa na Changamoto Zilizopo 

Kwa kifupi hali ya kisiasa nchini sio nzuri. Nyufa alizozitaja Mwalimu Nyerere sasa zinaonekana wazi. Viongozi wa siasa hawapendani, hata wale walio ndani ya Chama kimoja. Uadui wa kisiasa baina ya vyama umeongezeka. Washabiki wa vyama tofauti sasa wanazoeshwa kuchukiana. Maadili ya uongozi na ya kijamii yameporomoka. Ufanisi na weledi katika taasisi muhimu za uongozi kama vile Bunge, Mahakama na Polisi umeshuka na watu wamepunguza imani juu ya utendaji wa taasisi hizi nyeti. Tofauti ya kipato kati ya walionacho na wasio nacho imeongezeka. Viongozi hawaaminiki na hawaheshimiki tena kama zamani. Kwa kifupi matumaini juu ya mustakabali mwema wa taifa letu yamepungua.

Sifa za Viongozi Wanaohitajika

Kutokana na changamoto hizo, aina ya viongozi tunaowahitaji wanapaswa kuwa na sifa zifuatazo:

1. Tunataka kiongozi ambaye hakuna shaka kabisa kuhusu uadilifu wake. Sifa hii ni muhimu ili kurudisha imani ya wananchi juu ya uongozi wa nchi. Ingawa Mwalimu Nyerere hakuweza kuondoa ujinga, umasikini na maradhi katika nchi, uadilifu wake uliwafanya Watanzania washiriki na washirikiane naye katika jitihada zake. Uliwafanya wawe wazalendo na waipende nchi yao. Namna nzuri ya kurudisha uzalendo ni kuwa na viongozi waadilifu. Dhana kwamba afadhali kiongozi mwizi lakini mchapakazi ni dhana hatari sana. Inawezekana kupata kiongozi muadilifu na wakati huo huo mchapakazi. Tunataka kiongozi ambaye Watanzania watamuamini na kushirikiana naye.

2. Tunataka kiongozi ambaye hana chuki, visasi na ugomvi na wanasiasa wenzake ndani ya Chama chake na nje ya Chama chake. Taifa letu halipaswi kuendelea kupoteza muda na kugharamika kwa ugomvi baina ya wanasiasa. Katika miaka nane iliyopita, tumeona gharama ya ugomvi wa wanasiasa. Viongozi ambao wamekwishaanza kutangaziana uadui na kuapa kulipa visasi watakapochaguliwa hawaifai nchi yetu. Tukipata kiongozi ambaye ni sehemu ya ugomvi wa sasa, nchi yetu na siasa yetu itaendelea kuwa ya ugomvi, visasi, chuki na fitina kwa miaka mingine kumi ijayo na hatutapiga hatua ya maendeleo.

3. Tunataka kiongozi ambaye sio mbabe na ambaye hana chembechembe za udikteta wala uongozi wa imla. Watanzania sasa wamezoeshwa kuwa huru katika kutoa maoni yao na kuikosoa Serikali na viongozi wa Serikali bila kuhofia kukamatwa. Kuna dhana kwamba nchi inahitaji Rais dikteta. Dhana hii ni hatari sana. Tunamshukuru Rais wetu Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete kwa kujenga hali hii ya uvumilivu. Tunataka kiongozi atakayekuwa na sifa hii kama yake, atayekuwa na uwezo wa maamuzi magumu lakini yasiyosukumwa na sifa wala jazba. 

4. Tunataka kiongozi atayewaunganisha Watanzania kwa dini zao, makabila yao, kanda zao, pande zao za muungano na hali yao ya vipato. Hatutaki kiongozi atayeingia madarakani kwa fadhila za pesa za marafiki zake, watu wa dini yake, kanda yake au kabila lake. Tunataka kiongozi atakayeiweka nchi mbele kabla ya kitu kingine chochote. Tunataka kiongozi anayejua na anayeumizwa hali halisi ya maisha ya Watanzania.

5. Tunataka kiongozi mwenye maono na ufahamu wa ulimwengu wa karne hii ya 21. Mzee Mwinyi alipata kusema kwamba "kila zama na kitabu chake". Na kila Nabii na zama zake. Tunataka kiongozi wa zama hizi. Kila rika lina wajibu wake na wakati wake. Ni wakati sasa wa rika la sasa kupokea kijiti cha uongozi wa taifa. Tunataka kiongozi anayeyajua mawanda ya kimataifa na ambaye ataendeleza kazi nzuri aliyoifanya Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere, Mheshimiwa Rais Mstaafu Mkapa na sasa Mheshimiwa Rais Kikwete ya kuijengea nchi yetu heshima duniani.

Majina ya wanaokidhi au kukaribia sifa hizi

1. Mheshimiwa Zitto Z. Kabwe

Kwa katiba ya sasa na ile inayopendekezwa, Mheshimiwa Zitto hana sifa za kugombea Urais. Lakini iwapo rasimu ya mwisho itakayopitishwa itapunguza umri wa kugombea nafasi ya Urais, Mheshimiwa Zitto anafaa katika nafasi hiyo. Amethibitisha uzalendo wake katika masuala mbalimbali kuanzia masuala ya madini. Sifa zake zilionekana tangu wakati wa suala la Buzwagi na ushiriki wake kwenye kutengeneza sera mpya ya madini. Siku zote amekuwa anatetea watu wa hali ya chini. Siku zote amekuwa mzalendo anayeipenda nchi yake kabla ya Chama chake jambo ambalo limemfanya wakati mwingine apate matatizo na viongozi wa Chama chake. 

Pia ameonyesha uwezo wake mkubwa katika kusimamia hesabu za mashirika ya umma na hesabu za Serikali. Ni nafasi iliyompa uwezo na uzoefu wa kuijua Serikali vizuri kuliko Wabunge wengi. Sifa zake pia katika kuhakikisha kwamba nchi hii inanufaika na rasilimali ya gesi na mafuta ziko wazi. Harakati zake za kuhakikisha kwamba fedha zilizofichwa nje ya nchi zinarudishwa nchini na kuwanufaisha wananchi pia ni sifa za kiongozi jasiri. 

2. Mheshimiwa James Mbatia 

Ni kiongozi mzalendo na mwenye uchungu na nchi yake. Ni kiongozi aliyetulia na anayeonyesha hekima kubwa ya kiuongozi. Uongozi wake katika Baraza la Vyama vya Siasa Tanzania umedhihirisha busara zake kubwa. 

Katika siku za hivi karibuni harakati zake katika kupigania ubora wa elimu ya watoto wetu umeonyesha jinsi anavyojali ujenzi wa taifa bora zaidi. Pia ni kiongozi ambaye ameonyesha uwezo wa kufanya kazi na viongozi kutoka vyama tofauti vya siasa. Ni kiongozi ambaye ana sifa ya kuwaunganisha Watanzania. Ni kiongozi anayefahamu mahitaji ya karne ya 21.

Kuteuliwa kwake na Rais kuwa Mbunge kumeonyesha jinsi anavyoaminiwa na viongozi wa juu wa nchi, Mheshimiwa Mbatia ana sifa, busara na uwezo wa kushika nafasi hii kubwa. Vilevile anayo busara na ushawishi wa kutafuta na kupata ushirikiano wa kisiasa na vyama mbalimbali katika kuendesha nchi. 

3. Mheshimiwa Januari R. Makamba

Mheshimiwa Januari Makamba ni Naibu Waziri wa Sayansi na Teknolojia. Katika kipindi ambacho amekuwa kwenye siasa ameonyesha uwezo mkubwa wa uongozi. Kazi yake akiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini imeweka na rekodi ya kuwa msema kweli na jasiri hata wa kuikosoa Serikali ya Chama chake. Vilevile, yeye ndiye aliyewezesha kuanzisha mijadala ya gesi Bungeni na kupigania manufaa yake kwa taifa. Pia, aliwasilisha Bungeni sheria ya udhibiti wa kodi za nyumba na upangaji wa nyumba yenye kutetea maslahi ya wapangaji jambo lililoonyesha kwamba anao uwezo na nia ya kupigania wanyonge na watu wa kipato cha chini wanaonyanyaswa. Msimamo wake pia katika kuwatetea wakulima wa chai jimboni kwake unadhihirisha sifa hii ya utetezi wa wanyonge.

Mheshimiwa Makamba amefanya kazi Serikalini katika Wizara ya Mambo ya Nje na amekuwa Msaidizi wa karibu wa Mheshimiwa Rais Kikwete kwa miaka mitano na kuongozana naye nchi nzima kuanzia kwenye kampeni za uchaguzi kwahiyo nchi hii anaijua yote na anaijua vizuri na tunaamini changamoto zake anazijua. Kwa tunavyofahamu Wasaidizi wa Rais wanahudhuria vikao vya Baraza la Mawaziri kwahiyo kwa kuhudhuria vikao hivyo kwa yote aliyokuwa Ikulu na kwa kuwa Msaidizi wa karibu wa Rais kwa miaka mitano na kuongozana naye kote nchini na nchi za nje anajua jinsi nchi na Serikali vinavyoendeshwa na hatakuwa mgeni kabisa kuhusu uendeshaji wa taasisi ya urais.

Pia amekuwa kiongozi wa juu wa Chama chake, kuanzia kuwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu, Mjumbe wa Sekretarieti ya Chama na Mjumbe wa kikao kikubwa cha Kamati Kuu. Na kwa kuwa CCM ndio Chama kinachotawala hatuna shaka amepata uzoefu mkubwa na kushiriki katika maamuzi makubwa yanayohusu uongozi wa nchi. 

Pia katika mijadala yetu na tathmini katika vyuo vikuu nchini tumebaini kwamba ni kijana anayeheshimika, kuaminika na kukubalika na vijana wengi wa vyama karibu vyote vya siasa nchini, kwahiyo atakuwa na uwezo wa kuwaunganisha Watanzania. Ushindi wa kishindo alioupata kwenye Mkutano Mkuu wa Chama Chimwaga katika kugombea U-NEC Taifa unaonyesha pia kukubalika na kuheshimika na viongozi na wanachama wenzake, na hivyo Watanzania wengi, kutoka kona zote za Tanzania. 

4. Mheshimiwa Dr. Hussein A. Mwinyi

Dr. Hussein Mwinyi ni Waziri wa Afya. Ni kiongozi mtulivu, rahimu na mwenye busara. Ni aina ya kiongozi ambaye taifa letu linahitaji kwa sasa. Hana papara katika maamuzi na utendaji, ni msikivu mzuri na ni muadilifu wa hali ya juu. 

Dr. Mwinyi ameongoza vizuri nafasi za Uwaziri alizopata kuzishika, ikiwemo Wizara nyeti ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. Ni kiongozi asiyependa sifa katika utendaji wake na anafanya kazi zake kimya kimya lakini kwa ufanisi mkubwa. Kwa kushiriki kwake kwenye Baraza la Mawaziri amepata uzoefu wa namna Serikali inavyoendeshwa na hatatetereka iwapo atakalia kiti cha Rais. 

Amekuwa pia kiongozi wa ngazi ya juu wa Chama chake hasa kwenye Halmashauri Kuu na Kamati Kuu ambapo ameshiriki kwenye maamuzi makubwa yanayohusu uongozi wa nchi. Kuchaguliwa kwake kwa kura nyingi kwenye Halmashauri Kuu na baadaye Kamati Kuu kunaonyesha kukubalika kwake na wanachama na viongozi wenzake nchini.

Dr. Mwinyi ni Mbunge pekee aliyechaguliwa kwa kura kwa majimbo mawili ya pande zote za Muungano, kwa upande wa Bara (Mkuranga) na upande wa Zanzibar (Kwahani) kwahiyo ni kiungo kizuri katika kuimarisha Muungano wetu na kielelezo cha umoja wetu. 

Umri na Uzoefu wa Uongozi

Upo mjadala unaoendelea kuhusu suala la ujana na uongozi. Sisi tunaamini kwamba ujana peke yake sio sifa ya uongozi. Lakini pia tunaamini kwamba ujana sio kigezo cha kunyimwa fursa ya kuongoza. Taifa hili limekombolewa na vijana. Mwalimu Nyerere alikabidhiwa Urais wa TANU na kuongoza jukumu la kutafuta uhuru wa nchi yetu akiwa na miaka 32. Alishika madaraka ya nchi akiwa na miaka 39. Alifanikiwa kwasababu alifanya kazi na wazee na alishauriwa na wazee. Kwahiyo bado wazee wana nafasi ya ushauri katika uongozi wa nchi. 

Katika nchi ya Marekani Rais anayeheshimika hadi leo Rais John Kennedy alipewa uongozi akiwa na miaka 41, baada ya kuwa Mbunge kwa miaka michache. Rais Barack Obama pia wakati anagombea aliambiwa kwamba wakati wake bado kwa kuwa alikuwa bado kijana na mchanga sana kwenye siasa na hata hajamaliza nusu ya kipindi chake cha Ubunge. Hakusikiliza maneno hayo na Wamarekani hawakujali uchanga wake kwenye siasa kwa kuwa walitaka mabadiliko.

Katika nchi inayohitaji mabadiliko makubwa kama nchi yetu uzoefu wa miaka mingi wa siasa sio kipimo kizuri cha uongozi bora. Nchi yetu haihitaji uzoefu wa siasa, uzoefu wa kufanya yale yale ambayo hayajatusukuma mbele. Wakati wa mkutano mkuu wa kuteua mgombea wa Urais wa CCM mwaka 2005, Mwenyekiti Mstaafu wa CCM Mheshimiwa Benjamin Mkapa aliwaasa wajumbe kwamba ili Chama chake kishinde kinapaswa kuteua mgombea anayeshahabiana na Watanzania walio wengi, ambao ni vijana. Kauli hiyo bado ni ya kweli hadi leo. Nasi tunasema ili nchi yetu isonge mbele tunataka mwanzo mpya na tunataka fikra mpya.

Mungu Ibariki Tanzania!

Imesainiwa na Chifu Msopa 
Kamati ya Vijana Wapenda Amani Tanzania

--
Send Emails to wanabidii@googlegroups.com
 
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
 
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Wanabidii" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com.
For more options, visit https://groups.google.com/groups/opt_out.
 
 

Share this :

Previous
Next Post »
0 Comments