3.2 Mzigo wa Malipo wa TANESCO
Mheshimiwa Spika, nimeeleza awali kuwa mbali na kulipia gharama ya umeme wenyewe, TANESCO inawajibika chini ya Mkataba huo kulipa gharama za uwezo wa mitambo (capacity charges) ambazo ni sh. milioni 152 kila siku hadi mwisho wa Mkataba. Aidha, chini ya Mkataba huo, TANESCO inabebeshwa mzingo wote wa kodi, malipo na gharama mbalimbali zinazoweza kumkabili mwekezaji! Kifungu cha 3.4 cha Mkataba wa TANESCO na Richmond kinasema:
"All taxes and charges arising in relation to the importation and exportation of the plant, equipment, tools, spare parts, consumables, testing and monitoring equipment or in connection with the supplier's performance of its obligations under this Agreement generally that become due in accordance with the laws of Tanzania shall be paid for by TANESCO at its sole cost and expense".
Mheshimiwa Spika, Tafsiri ya jumla ya kifungu hiki cha Mkataba ni kwamba: kodi na ada zote zinazohusiana na uingizaji ndani ya nchi na usafirishaji nje ya nchi wa mitambo yote, vifaa, vipuli n.k. na gharama zote zinazohusiana na utekelezaji wa wajibu wa Richmond (sasa Dowans) chini ya Mkataba, yaani gharama za uendeshaji (operations), za matengenezo (maintenance) ya mitambo na gharama ya gesi inayotumika kuzalishia umeme, ni wajibu wa TANESCO kuzibeba!
Mheshimiwa Spika, mzigo mkubwa ambao TANESCO inabeba chini ya mkataba na Richmond (sasa Dowans) unajirudia katika mikataba mingine kati ya TANESCO na makampuni mengine ya umeme kama vile IPTL, AGGREKO, ALSTOM na SONGAS ambayo kwa ujumla yanachukua sehemu kubwa ya mapato ya shirika hilo, hivyo kuvuruga kabisa mizania yake. Kwa wigo wa tafsiri wa mikataba hii inayotuumiza kwa kujitakia, TANESCO inawajibika kuwalipia hawa wanaojiita wawekezaji hata gharama za bima na ada za mawakili wao!
Mheshimiwa Spika, tumefikishwa hapa tulipofika na mikataba mibovu, maamuzi ya kiimla na papara ya baadhi ya watendaji waandamizi wa Serikali wasiozingatia maslahi ya muda mrefu ya Taifa. Net Group Solution (PTY) ambayo kwa kiwango kikubwa imechangia sana katika kuidumaza TANESCO kiutaalamu na kifedha, iliingizwa TANESCO kwa ubabe bila kujali hoja za msingi za wataalamu na wafanyakazi wa TANESCO. Matokeo yake wote tunayaelewa. Vivyo hivyo, Richmond Development Company LLC, kampuni isiyo na rekodi yoyote ya kiufundi hata ya kuchomeka "bulb" kwenye kishikio chake, ikapewa mradi mkubwa na Serikali wa kuzalisha umeme wa dharura bila kujali kuhusu ufanisi wake tena katika kipindi ambacho nchi ilikuwa gizani! Huu ni ujasiri wa kifisadi.
4.0 UTEKELEZAJI WA MRADI
4.1 Barua ya Dhamana ya Benki (Letter of Credit)
Mheshimiwa Spika, ili kufanikisha utekelezaji wa haraka wa mradi wa umeme wa dharura, Mkataba kati ya TANESCO na Richmond Development Company LLC, ulitoa fursa ya kufunguliwa kwa Barua ya Dhamana ya Benki (Letter of Credit), kwa kifupi nitaiita LC, kwa madhumuni ya kulipia gharama za maandalizi na za usafirishaji wa mitambo ya uzalishaji wa umeme huo wa dharura. Mkataba ulitaka TANESCO, Benki Kuu ya Tanzania, Wizara ya Fedha na Richmond Development Company LLC waketi pamoja kukubaliana masharti ya LC hiyo.
Mheshimiwa Spika, vyombo hivyo vya Serikali vilikaa tarehe 7 Julai, 2006 baada ya kupokea mapendekezo kutoka Richmond Development Company LLC ya namna ambavyo ingetaka ilipwe. Vyombo hivyo vya Serikali vikarekebisha kidogo madai ya Richmond na kuamua kuwa kampuni hiyo ilipwe Dola za Kimarekani 30,000,000 (milioni thelathini), sawa na asilimia 30 ya thamani ya malipo ya Mkataba kwa kipindi cha miaka miwili kwa masharti kwamba: asilimia 12 ya fedha hizo ilipwe kama malipo ya awali (Advance Payment) baada ya kuwasilishwa hati ya madai (Invoice), hati ya Uthibitisho wa Udhamini wa Benki (Bank Guarantee) kwa TANESCO na uthibitisho wa kusafirisha mitambo kuleta Tanzania; asilimia 10 ilipwe baada ya kuwasilishwa hati za kusafirishia mitambo kwa mpangilio wa awamu; asilimia 8 ilipwe mara baada ya uzinduzi wa mitambo.
Mheshimiwa Spika, siku tatu baadaye Richmond Development Company LLC ikataka masharti hayo yarekebishwe ili kuipa kampuni hiyo unafuu zaidi, wazo ambalo TANESCO ililikataa kwa kuhofia kuwa kampuni hiyo ingeweza kupotea baada ya kupata malipo ya awali yasiyo na masharti magumu. Tarehe 27 Julai, 2007 Wizara ya Nishati na Madini ikaingilia kati mvutano huo na kuitisha kikao kilichosimamiwa na Waziri Mhe. Dr. Ibrahim Msabaha, Mb kama Mwenyekiti. Kikao hiki kilihusisha wajumbe kutoka Wizara ya Fedha, TANESCO, Benki Kuu ya Tanzania, Mwakilishi kutoka CTI na Richmond Development Company LLC. Kama ilivyokuwa kwa kikao cha tarehe 7 Julai, 2006, Mwanasheria Mkuu wa Serikali wala mwakilishi wake hakuhudhuria.
Mheshimiwa Spika, kikao hiki kikaamua kurekebishwa kwa masharti ya LC kama ilivyopendekezwa na Richmond Development Company LLC. Baadhi ya marekebisho yalikuwa:
(i) Kampuni hiyo ilipwe asilimia 17.5 ya jumla ya thamani ya Mkataba baada ya Benki ya kampuni hiyo kupokea hati za usafirishaji wa mitambo (shipping documents), hati ya bima, orodha ya vifungashio (packing list), hati za uasili wa bidhaa (Certificate of origin), hati za upangaji wa mizigo (packing lists), pamoja na hati ya madai (Invoice) kwa mtambo wa MW 22.
(ii) Kampuni hiyo ilipwe vilevile asilimia 17.5 ya jumla ya thamani ya Mkataba baada ya TANESCO kutoa hati ya uthibitisho ya mitambo kuwasili eneo la kazi (Ubungo, Dar-es-Salaam).
4.2 Mchakato wa Kufungua Barua ya Dhamana ya Benki
Mheshimiwa Spika, baada ya makubaliano hayo, tarehe 23 Agosti, 2006 TANESCO iliiomba Citibank (Tanzania) kufungua LC kwa ajili ya Richmond Development Company LLC yenye thamani ya Dola za Kimarekani 30,696,598.00. Siku hiyo hiyo ya terehe 23 Agosti 2006, Citibank (Tanzania) iliwajulisha TANESCO kwamba isingeweza kufungua LC kwa ajili ya Richmond Development Company LLC, kutokana na kile walichoeleza kuwa ni kutopata muda wa kutosha kuchunguza kwa kina uwezo wa mteja anayehusishwa na dhamana ya malipo hayo (due diligence) kabla ya kuingia Mkataba huo.
Mheshimiwa Spika, baada ya kukataliwa na Citibank, TANESCO waliiomba Benki ya CRDB kufungua Barua ya Dhamana ya Benki hiyo kwa masharti sawa na yale yaliyopelekwa Citibank (Tanzania). Tarehe 25 Agosti, 2006 CRDB ikafanya mawasiliano Citibank (New York). Lakini tarehe 2 Septemba 2006, Citibank (New York) ikaifahamisha CRDB kuwa wao pia wasingeweza kushiriki katika kufungua LC kwa Richmond Development Company LLC kutokana na mahitaji ya lazima ya kuzingatiwa chini ya Kifungu Namba 7 cha Kanuni za UCP 500. Kifungu hicho ndicho kilichowafanya Citibank (Tanzania) kukataa kufungua Barua kama hiyo.
Mheshimiwa Spika, kitendo cha benki hizo mbili za Kimarekani kukataa kufungua LC kwa jili ya kampuni ya Kimarekani, kilitosha kuzua wasiwasi wa msingi kuhusu kampuni hiyo. Kwa kuwa Watanzania tuliishaamua kufa na Richmond, tukasonga mbele! Hivyo, tarehe 2 Septemba 2006, CRDB ikafungua upya LC kwa ajili ya Richmond Development Company LLC kupitia Benki nyingine ya nje iitwayo HSBC kwa masharti yale yale ambayo CRDB ilipokea kutoka TANESCO. Hatimaye HSBC ikafungua LC kwa ajili ya kampuni hiyo lakini kwa kutumia jina lingine la RDEVCO na siyo Richmond Development Company LLC!
4.3 Maombi ya Mapya ya Richmond kubadilisha tena Masharti ya LLC.
Mheshimiwa Spika, baada ya LC kufunguliwa na kuthibitishwa uwajibikaji kwa utekelezaji wa masharti ya Mkataba ulianza rasmi. Hata hivyo, tarehe 4 Oktoba 2006, Richmond Development Company LLC kwa mara nyingine tena, iliipelekea TANESCO maombi ya kutaka kuifanyia marekebisho ya LC kwamba:-
(i) LC iruhusu malipo ya awali (upfront payment) ya Dola za Kimarekani milioni 10;
(ii) Richmond Development Company LLC iruhusiwe kusafirisha mtambo wa kwanza kwa njia ya ndege kwa gharama ya Dola za Kimarekani 5,696,568.00;
(iii) Asilimia 50 ya Barua ya Dhamana ya Benki ilipwe baada ya uthibitisho kutoka TANESCO juu ya kupokelewa kwa mitambo nchini.
Mheshimiwa Spika, tarehe hiyo hiyo ya 4 Oktoba, 2006 Wizara ya Nishati na Madini ikaitisha kikao kujadili maombi hayo. Kikao hiki kilichohudhuriwa na wawakilishi kutoka Wizara ya Nishati na Madini, TANESCO, Benki ya CRDB na Richmond Development Company LLC, kikakubali maombi yote ya Richmond Development Company LLC na kuagiza kuwa hatua za utekelezaji zifuatie mara moja.
Mheshimiwa Spika, pamoja na ukweli kwamba mchakato mzima ulitawaliwa na udharura, Kamati Teule haielewi ni vipi Wizara ya Nishati na Madini ilikuwa ikitekeleza kila pendekezo jipya lililotolewa na Richmond Development Company LLC bila kujali madhara ambayo yangewea kutokea pindi kampuni hiyo ingelipwa na kuingia mitini.
Mheshimiwa Spika, baada ya kubaini kwamba mapendekezo hayo mapya ya kuibeba Richmond yalikuwa nje ya masharti ya LC yaliyoainishwa katika Mkataba wa malipo kati ya TANESCO, Benki Kuu ya Tanzania, Wizara ya Fedha na CRDB Bank, Wizara ya Nishati na Madini ikaijulisha Wizara ya Fedha kuhusu maamuzi mapya ya LC kutokana na maombi ya Richmond Development Company LLC.
Mheshimiwa Spika, Wizara ya Fedha haikuridhishwa na mapendekezo yaliyotolewa kwani malipo yoyote ya awali kutoka fungu maalum la Multilateral Debt Relief Initiative ni lazima yafanyike kwa uthibitisho wa kuridhisha. Sehemu ya barua hiyo iliyoandikwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Ndugu Gray Mgonja, inasema:
: "... tunaona kuwa tofauti na taarifa zilizotolewa wakati wa majadiliano ya Mkataba kuwa mkandarasi aliyechaguliwa alikuwa na vifaa tayari kuvileta nchini, sasa ni wazi kuwa si hivyo.
Kama unavyojua, msingi wa malipo kuhusu mitambo ya kununua au kukodisha chini ya Mradi wa Nishati ya Dharura unaofadhiliwa kupitia IMF MDRI, ni mkataba unaotokana na majadiliano.
Napenda kupendekeza kuwa malipo yoyote ya awali kutoka akaunti ya MDRI lazima yaandamane na dhamana ya kuridhisha kutoka kwa mkandarasi. Sharti hili linaonyesha kutokuzingatiwa chini ya mapendekezo yenu".
Mheshimiwa Spika, pamoja na maelekezo na ushauri huu wa Wizara ya Fedha, Wizara ya Nishati na Madini siku hiyo hiyo ikaiandikia barua TANESCO kuitaka itekeleze maombi ya Richmond Development Company LLC mara moja kubadilisha masharti ya malipo:-
" . . . I wish to inform you that the proposed amendments to the existing Letter of Credit are acceptable and you are advised to liaise with CRDB Bank to effect the changes as soon as is practical. . . ." Barua ya Katibu Mkuu wa Nishati na Madini (Kumb. Na. CBD.214/324/01 ya tarehe 6/10/2006) inasomeka.
Mheshimiwa Spika, Kamati Teule imejiuliza bila kupata majibu: Ni nini kilifanyika hadi Wizara ya Nishati na Madini ikatoa kauli hii ambayo ni tofauti kabisa na ushauri ilioupata kutoka Wizara ya Fedha? Nini msingi wa ukereketwa au ufukukutwa bayana wa Wizara ya Nishati na Madini kuhusu Richmond?
Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza maagizo ya Wizara, TANESCO iliiandikia barua Benki ya CRDB tarehe 6 Oktoba, 2006 kuitaka kufanya mabadiliko hayo mapya kwenye LC ya Richmond. Tarehe 9 Oktoba, 2006 Benki ya CRDB iliijibu TANESCO na kuikumbusha kwamba LC inasimamiwa na makubaliano ya pamoja chini ya uangalizi wa Benki Kuu ya Tanzania. Kwa msingi huo TANESCO ikatakiwa kufuata taratibu kwa kuiomba Benki Kuu ya Tanzania kibali cha kufanya marekebisho katika Kifungu 1(a) cha Mkataba wa makubaliano ya taratibu za malipo ili kuwezesha maombi yaliyopendekezwa kufanyiwa kazi. Jibu hilo likailazimu TANESCO kufuta maombi hayo.
Mheshimiwa Spika, hadi LC hiyo ya Richmond inaisha muda wake (tarehe 30 Novemba, 2006), kampuni hiyo ya Kimarekani haikuweza kutekeleza sharti hata moja na hivyo kushindwa kuchukua fedha kama ilivyokuwa imepangwa. Swali linalojitokeza ni: Iwapo CRDB ingekubali kubadilisha masharti ya LC na kuipa Richmond Development Company LLC fedha ilizoomba bila kibali cha Benki Kuu ya Tanzania; Je, Richmond ingeleta nchini mitambo kama ilivyokusudiwa au ingekuwa ni hasara kwa Taifa?
Kwa upande mwingine, mchakato mzima wa Richmond Development Company LLC wa kutaka kufanya mabadiliko katika Barua ya Dhamana ya Benki mara kwa mara unadhihirisha nia yao ya kutaka kupata mtaji. Pia inadhihirisha kwamba Richmond Development Company, LLC haikuwa na uwezo wa kifedha wa kutekeleza Mkataba huu kinyume na tamko kwenye Mkataba kuwa:-
"The Supplier (i.e. Richmond) has the equipment and the financial and technical capability to construct, install, commission, operate and maintain such a plant as required by TANESCO". (Msambazaji (yaani Richmond) ana vifaa na uwezo wa kifedha na wa kitaalam kujenga, kusimika, kuiwasha, kuendesha na kuendeleza mtambo huo kama TANESCO inavyohitaji.)
Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo Kamati Teule ilijiuliza maswali yafuatayo:-
(i) Je, utafiti ulifanywa kufahamu gharama halisi za mitambo mipya kutoka kwa watengenezaji wenyewe bila ya kupitia kwa mawakala? Kamati Teule ilibaini kuwa zoezi hilo liliwahi kufanyika mwaka 1998 tu ambapo Wizara ya Nishati na Madini ilitoa kazi hiyo kwa wataalam wa sekta (consultants) na kufanikisha kugundua kuwa bei ya mitambo ya umeme ya IPTL (400 MW) ambayo ilitakiwa kuuzwa kwa Dola za Kimarekani milioni 150 (Tsh. 187.5 bilioni) bei yake halisi ilikuwa ni Dola za Kimarekani milioni 85 (Tsh.106.2 bilioni) tu na hivyo kupata kigezo cha kukataa bei yao. Hivyo basi, kutokana uzoefu huo, Wizara ya Nishati na Madini kwa kushirikiana na TANESCO walitakiwa kufuatilia bei hizo za mitambo na pia makadirio ya kazi za ujenzi ili kupata picha ya gharama halisi ya mradi jambo, ambalo halikufanyika.
Mheshimiwa Spika, kwa viongozi wa Wizara na TANESCO kushindwa kujua bei halisi ya mitambo kutoka kwa watengenezaji wenyewe kwa takribani miaka 10 huku wakisafiri kwenda nje ya nchi kila kukicha kwa mikutano, warsha, makongamano, n.k, na kwa Wizara kung'ang'ania kutumia mawakala badala ya watengenezaji wa mitambo, nchi yetu imegeuzwa gulio la wajanja kuikamua na kuwabebesha wananchi mzigo wa kodi.
Mheshimiwa Spika, Kamati Teule ilipotembelea Marekani, iliamua kuwatembelea baadhi ya watengenezaji wa mitambo ya uzalishaji wa umeme huko huko Houston Marekani kujua bei za mitambo yao. Mmoja wa watengenezaji wenye jina kubwa duniani, Kawasaki Gas Turbines – Americas, anatengeneza na kuuza Mtambo mpya aina ya GPB180 wenye uwezo wa kuzalisha MW 17.5 kwa Dola za Kimarekani 7.5 milioni (Tsh. 9.4 bilioni). Mawakala huwa wanatuletea mitambo ya aina hiyo hiyo kwa bei mara mbili ya bei halisi.
(ii) Iwapo TANESCO au Serikali iliweza kufungua LC ya Dola za Kimarekani 30,696,598; je, fedha hizo zisingeweza kutosheleza kununua mitambo mipya ya uzalishaji umeme, na mitambo hiyo kubakia mali ya TANESCO, badala ya kuingia katika Mikataba ya ghali ya kukodisha mitambo?
Aidha, taarifa za watendaji wa Wizara ya Nishati na Madini kwamba wakati wa kipindi cha mchakato wa zabuni ya umeme wa dharura kulikuwa na ugumu wa kupatikana mitambo ya umeme wa dharura zimethibitishwa na Kamati Teule kuwa sio za kweli.
Mheshimiwa Spika, ni ukweli kwamba kulikuwa na ukame, lakini ukame huo haukuwa wa mitambo ya kuzalisha umeme kwani mitambo hiyo hutengenezwa muda wote na sio kwa kutegemea mvua. Aidha, utafiti wetu umebaini kuwa katika kipindi hicho cha matatizo ya umeme nchini, kampuni zote za kutengeneza mitambo hiyo ya umeme zilikuwa zina mitambo kadhaa ikisubiri wateja. Kawasaki ilikuwa na mitambo 8 ya kisasa tena yenye kutumia gesi na dizeli (dual fuel plant). Serikali nyingi, ikiwemo ya Nigeria, ni wateja wazuri wa kampuni hiyo ambao huteremshiwa bei kwa mtambo moja hadi Dola za Kimarekani milioni 6.7 milioni badala ya Dola za Kimarekani milioni 7.5 bei ya kawaida.
Mheshimiwa Spika, kwa thamani ya LC iliyofunguliwa kwa Richmond Development Company LLC ya Dola za Kimarekani milioni 30.7 au Tsh 38.4 bilioni, TANESCO ingeweza kununua mitambo mipya yote minne pamoja na kumudu kulipia gharama za kusafirisha kwa meli hadi Dar-es-Salaam. Hivyo ili zipatikane MW 105.6 zilizohitajiwa na TANESCO ingehitajika mitambo sita (6) ambayo ni sawa sawa Dola za Kimarekani milioni 45 au Tsh. 56.25 bilioni badala ya Dola za Kimarekani milioni 87 au Tsh. 108.7 bilioni tulizobebeshwa na Richmond Development Company LLC.
Mheshimiwa Spika, Je, si dhahiri kuwa hii ndiyo ilikuwa nia ya Richmond Development Company LLC, yaani kupata fedha za malipo ya awali (advance payment) ili ikatununulie mtambo mmoja na kuja kutukodisha sisi wenyewe, hivyo kufaidika na capacity charge ya kila mwezi kwa Mkataba wa miaka miwili? Kwa mtambo mmoja wa MW 22, capacity charge ni Dola za Kimarekani takriban 730,871 au Tsh. Milioni 913.6 kwa mwezi, hivyo kwa miezi 24 ni wastani wa Dola za Kimarekani 17,540,912 au Tsh. Bilioni 21.9.
(iii) Kwa kuwa thamani ya LC inalipwa kama malipo ya awali (advance payment), Je, hii si sawa na kutoa mkopo kwa Richmond Development Company LLC? Kamati Teule inaona kwamba hiyo ni sawa na kutoa mkopo usio na riba kwa mfanyabiashara wa nje ili awe mwekezaji.
(iv) Kwa nini katika Mkataba wa Richmond Development Company LLC kifungu cha kufidia malipo ya awali (advance payment) ya LC hakikuwekwa bayana ndani ya Mkataba tofauti na Mikataba mingine, badala yake ikawekwa fursa ya kujadiliana na mkandarasi? Kamati Teule haioni sababu yeyote ya msingi mbali na wahusika kujiwekea fursa ya kukidhi maslahi yao binafsi.
Mheshimiwa Spika, nimeeleza awali kuwa mbali na kulipia gharama ya umeme wenyewe, TANESCO inawajibika chini ya Mkataba huo kulipa gharama za uwezo wa mitambo (capacity charges) ambazo ni sh. milioni 152 kila siku hadi mwisho wa Mkataba. Aidha, chini ya Mkataba huo, TANESCO inabebeshwa mzingo wote wa kodi, malipo na gharama mbalimbali zinazoweza kumkabili mwekezaji! Kifungu cha 3.4 cha Mkataba wa TANESCO na Richmond kinasema:
"All taxes and charges arising in relation to the importation and exportation of the plant, equipment, tools, spare parts, consumables, testing and monitoring equipment or in connection with the supplier's performance of its obligations under this Agreement generally that become due in accordance with the laws of Tanzania shall be paid for by TANESCO at its sole cost and expense".
Mheshimiwa Spika, Tafsiri ya jumla ya kifungu hiki cha Mkataba ni kwamba: kodi na ada zote zinazohusiana na uingizaji ndani ya nchi na usafirishaji nje ya nchi wa mitambo yote, vifaa, vipuli n.k. na gharama zote zinazohusiana na utekelezaji wa wajibu wa Richmond (sasa Dowans) chini ya Mkataba, yaani gharama za uendeshaji (operations), za matengenezo (maintenance) ya mitambo na gharama ya gesi inayotumika kuzalishia umeme, ni wajibu wa TANESCO kuzibeba!
Mheshimiwa Spika, mzigo mkubwa ambao TANESCO inabeba chini ya mkataba na Richmond (sasa Dowans) unajirudia katika mikataba mingine kati ya TANESCO na makampuni mengine ya umeme kama vile IPTL, AGGREKO, ALSTOM na SONGAS ambayo kwa ujumla yanachukua sehemu kubwa ya mapato ya shirika hilo, hivyo kuvuruga kabisa mizania yake. Kwa wigo wa tafsiri wa mikataba hii inayotuumiza kwa kujitakia, TANESCO inawajibika kuwalipia hawa wanaojiita wawekezaji hata gharama za bima na ada za mawakili wao!
Mheshimiwa Spika, tumefikishwa hapa tulipofika na mikataba mibovu, maamuzi ya kiimla na papara ya baadhi ya watendaji waandamizi wa Serikali wasiozingatia maslahi ya muda mrefu ya Taifa. Net Group Solution (PTY) ambayo kwa kiwango kikubwa imechangia sana katika kuidumaza TANESCO kiutaalamu na kifedha, iliingizwa TANESCO kwa ubabe bila kujali hoja za msingi za wataalamu na wafanyakazi wa TANESCO. Matokeo yake wote tunayaelewa. Vivyo hivyo, Richmond Development Company LLC, kampuni isiyo na rekodi yoyote ya kiufundi hata ya kuchomeka "bulb" kwenye kishikio chake, ikapewa mradi mkubwa na Serikali wa kuzalisha umeme wa dharura bila kujali kuhusu ufanisi wake tena katika kipindi ambacho nchi ilikuwa gizani! Huu ni ujasiri wa kifisadi.
4.0 UTEKELEZAJI WA MRADI
4.1 Barua ya Dhamana ya Benki (Letter of Credit)
Mheshimiwa Spika, ili kufanikisha utekelezaji wa haraka wa mradi wa umeme wa dharura, Mkataba kati ya TANESCO na Richmond Development Company LLC, ulitoa fursa ya kufunguliwa kwa Barua ya Dhamana ya Benki (Letter of Credit), kwa kifupi nitaiita LC, kwa madhumuni ya kulipia gharama za maandalizi na za usafirishaji wa mitambo ya uzalishaji wa umeme huo wa dharura. Mkataba ulitaka TANESCO, Benki Kuu ya Tanzania, Wizara ya Fedha na Richmond Development Company LLC waketi pamoja kukubaliana masharti ya LC hiyo.
Mheshimiwa Spika, vyombo hivyo vya Serikali vilikaa tarehe 7 Julai, 2006 baada ya kupokea mapendekezo kutoka Richmond Development Company LLC ya namna ambavyo ingetaka ilipwe. Vyombo hivyo vya Serikali vikarekebisha kidogo madai ya Richmond na kuamua kuwa kampuni hiyo ilipwe Dola za Kimarekani 30,000,000 (milioni thelathini), sawa na asilimia 30 ya thamani ya malipo ya Mkataba kwa kipindi cha miaka miwili kwa masharti kwamba: asilimia 12 ya fedha hizo ilipwe kama malipo ya awali (Advance Payment) baada ya kuwasilishwa hati ya madai (Invoice), hati ya Uthibitisho wa Udhamini wa Benki (Bank Guarantee) kwa TANESCO na uthibitisho wa kusafirisha mitambo kuleta Tanzania; asilimia 10 ilipwe baada ya kuwasilishwa hati za kusafirishia mitambo kwa mpangilio wa awamu; asilimia 8 ilipwe mara baada ya uzinduzi wa mitambo.
Mheshimiwa Spika, siku tatu baadaye Richmond Development Company LLC ikataka masharti hayo yarekebishwe ili kuipa kampuni hiyo unafuu zaidi, wazo ambalo TANESCO ililikataa kwa kuhofia kuwa kampuni hiyo ingeweza kupotea baada ya kupata malipo ya awali yasiyo na masharti magumu. Tarehe 27 Julai, 2007 Wizara ya Nishati na Madini ikaingilia kati mvutano huo na kuitisha kikao kilichosimamiwa na Waziri Mhe. Dr. Ibrahim Msabaha, Mb kama Mwenyekiti. Kikao hiki kilihusisha wajumbe kutoka Wizara ya Fedha, TANESCO, Benki Kuu ya Tanzania, Mwakilishi kutoka CTI na Richmond Development Company LLC. Kama ilivyokuwa kwa kikao cha tarehe 7 Julai, 2006, Mwanasheria Mkuu wa Serikali wala mwakilishi wake hakuhudhuria.
Mheshimiwa Spika, kikao hiki kikaamua kurekebishwa kwa masharti ya LC kama ilivyopendekezwa na Richmond Development Company LLC. Baadhi ya marekebisho yalikuwa:
(i) Kampuni hiyo ilipwe asilimia 17.5 ya jumla ya thamani ya Mkataba baada ya Benki ya kampuni hiyo kupokea hati za usafirishaji wa mitambo (shipping documents), hati ya bima, orodha ya vifungashio (packing list), hati za uasili wa bidhaa (Certificate of origin), hati za upangaji wa mizigo (packing lists), pamoja na hati ya madai (Invoice) kwa mtambo wa MW 22.
(ii) Kampuni hiyo ilipwe vilevile asilimia 17.5 ya jumla ya thamani ya Mkataba baada ya TANESCO kutoa hati ya uthibitisho ya mitambo kuwasili eneo la kazi (Ubungo, Dar-es-Salaam).
4.2 Mchakato wa Kufungua Barua ya Dhamana ya Benki
Mheshimiwa Spika, baada ya makubaliano hayo, tarehe 23 Agosti, 2006 TANESCO iliiomba Citibank (Tanzania) kufungua LC kwa ajili ya Richmond Development Company LLC yenye thamani ya Dola za Kimarekani 30,696,598.00. Siku hiyo hiyo ya terehe 23 Agosti 2006, Citibank (Tanzania) iliwajulisha TANESCO kwamba isingeweza kufungua LC kwa ajili ya Richmond Development Company LLC, kutokana na kile walichoeleza kuwa ni kutopata muda wa kutosha kuchunguza kwa kina uwezo wa mteja anayehusishwa na dhamana ya malipo hayo (due diligence) kabla ya kuingia Mkataba huo.
Mheshimiwa Spika, baada ya kukataliwa na Citibank, TANESCO waliiomba Benki ya CRDB kufungua Barua ya Dhamana ya Benki hiyo kwa masharti sawa na yale yaliyopelekwa Citibank (Tanzania). Tarehe 25 Agosti, 2006 CRDB ikafanya mawasiliano Citibank (New York). Lakini tarehe 2 Septemba 2006, Citibank (New York) ikaifahamisha CRDB kuwa wao pia wasingeweza kushiriki katika kufungua LC kwa Richmond Development Company LLC kutokana na mahitaji ya lazima ya kuzingatiwa chini ya Kifungu Namba 7 cha Kanuni za UCP 500. Kifungu hicho ndicho kilichowafanya Citibank (Tanzania) kukataa kufungua Barua kama hiyo.
Mheshimiwa Spika, kitendo cha benki hizo mbili za Kimarekani kukataa kufungua LC kwa jili ya kampuni ya Kimarekani, kilitosha kuzua wasiwasi wa msingi kuhusu kampuni hiyo. Kwa kuwa Watanzania tuliishaamua kufa na Richmond, tukasonga mbele! Hivyo, tarehe 2 Septemba 2006, CRDB ikafungua upya LC kwa ajili ya Richmond Development Company LLC kupitia Benki nyingine ya nje iitwayo HSBC kwa masharti yale yale ambayo CRDB ilipokea kutoka TANESCO. Hatimaye HSBC ikafungua LC kwa ajili ya kampuni hiyo lakini kwa kutumia jina lingine la RDEVCO na siyo Richmond Development Company LLC!
4.3 Maombi ya Mapya ya Richmond kubadilisha tena Masharti ya LLC.
Mheshimiwa Spika, baada ya LC kufunguliwa na kuthibitishwa uwajibikaji kwa utekelezaji wa masharti ya Mkataba ulianza rasmi. Hata hivyo, tarehe 4 Oktoba 2006, Richmond Development Company LLC kwa mara nyingine tena, iliipelekea TANESCO maombi ya kutaka kuifanyia marekebisho ya LC kwamba:-
(i) LC iruhusu malipo ya awali (upfront payment) ya Dola za Kimarekani milioni 10;
(ii) Richmond Development Company LLC iruhusiwe kusafirisha mtambo wa kwanza kwa njia ya ndege kwa gharama ya Dola za Kimarekani 5,696,568.00;
(iii) Asilimia 50 ya Barua ya Dhamana ya Benki ilipwe baada ya uthibitisho kutoka TANESCO juu ya kupokelewa kwa mitambo nchini.
Mheshimiwa Spika, tarehe hiyo hiyo ya 4 Oktoba, 2006 Wizara ya Nishati na Madini ikaitisha kikao kujadili maombi hayo. Kikao hiki kilichohudhuriwa na wawakilishi kutoka Wizara ya Nishati na Madini, TANESCO, Benki ya CRDB na Richmond Development Company LLC, kikakubali maombi yote ya Richmond Development Company LLC na kuagiza kuwa hatua za utekelezaji zifuatie mara moja.
Mheshimiwa Spika, pamoja na ukweli kwamba mchakato mzima ulitawaliwa na udharura, Kamati Teule haielewi ni vipi Wizara ya Nishati na Madini ilikuwa ikitekeleza kila pendekezo jipya lililotolewa na Richmond Development Company LLC bila kujali madhara ambayo yangewea kutokea pindi kampuni hiyo ingelipwa na kuingia mitini.
Mheshimiwa Spika, baada ya kubaini kwamba mapendekezo hayo mapya ya kuibeba Richmond yalikuwa nje ya masharti ya LC yaliyoainishwa katika Mkataba wa malipo kati ya TANESCO, Benki Kuu ya Tanzania, Wizara ya Fedha na CRDB Bank, Wizara ya Nishati na Madini ikaijulisha Wizara ya Fedha kuhusu maamuzi mapya ya LC kutokana na maombi ya Richmond Development Company LLC.
Mheshimiwa Spika, Wizara ya Fedha haikuridhishwa na mapendekezo yaliyotolewa kwani malipo yoyote ya awali kutoka fungu maalum la Multilateral Debt Relief Initiative ni lazima yafanyike kwa uthibitisho wa kuridhisha. Sehemu ya barua hiyo iliyoandikwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Ndugu Gray Mgonja, inasema:
: "... tunaona kuwa tofauti na taarifa zilizotolewa wakati wa majadiliano ya Mkataba kuwa mkandarasi aliyechaguliwa alikuwa na vifaa tayari kuvileta nchini, sasa ni wazi kuwa si hivyo.
Kama unavyojua, msingi wa malipo kuhusu mitambo ya kununua au kukodisha chini ya Mradi wa Nishati ya Dharura unaofadhiliwa kupitia IMF MDRI, ni mkataba unaotokana na majadiliano.
Napenda kupendekeza kuwa malipo yoyote ya awali kutoka akaunti ya MDRI lazima yaandamane na dhamana ya kuridhisha kutoka kwa mkandarasi. Sharti hili linaonyesha kutokuzingatiwa chini ya mapendekezo yenu".
Mheshimiwa Spika, pamoja na maelekezo na ushauri huu wa Wizara ya Fedha, Wizara ya Nishati na Madini siku hiyo hiyo ikaiandikia barua TANESCO kuitaka itekeleze maombi ya Richmond Development Company LLC mara moja kubadilisha masharti ya malipo:-
" . . . I wish to inform you that the proposed amendments to the existing Letter of Credit are acceptable and you are advised to liaise with CRDB Bank to effect the changes as soon as is practical. . . ." Barua ya Katibu Mkuu wa Nishati na Madini (Kumb. Na. CBD.214/324/01 ya tarehe 6/10/2006) inasomeka.
Mheshimiwa Spika, Kamati Teule imejiuliza bila kupata majibu: Ni nini kilifanyika hadi Wizara ya Nishati na Madini ikatoa kauli hii ambayo ni tofauti kabisa na ushauri ilioupata kutoka Wizara ya Fedha? Nini msingi wa ukereketwa au ufukukutwa bayana wa Wizara ya Nishati na Madini kuhusu Richmond?
Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza maagizo ya Wizara, TANESCO iliiandikia barua Benki ya CRDB tarehe 6 Oktoba, 2006 kuitaka kufanya mabadiliko hayo mapya kwenye LC ya Richmond. Tarehe 9 Oktoba, 2006 Benki ya CRDB iliijibu TANESCO na kuikumbusha kwamba LC inasimamiwa na makubaliano ya pamoja chini ya uangalizi wa Benki Kuu ya Tanzania. Kwa msingi huo TANESCO ikatakiwa kufuata taratibu kwa kuiomba Benki Kuu ya Tanzania kibali cha kufanya marekebisho katika Kifungu 1(a) cha Mkataba wa makubaliano ya taratibu za malipo ili kuwezesha maombi yaliyopendekezwa kufanyiwa kazi. Jibu hilo likailazimu TANESCO kufuta maombi hayo.
Mheshimiwa Spika, hadi LC hiyo ya Richmond inaisha muda wake (tarehe 30 Novemba, 2006), kampuni hiyo ya Kimarekani haikuweza kutekeleza sharti hata moja na hivyo kushindwa kuchukua fedha kama ilivyokuwa imepangwa. Swali linalojitokeza ni: Iwapo CRDB ingekubali kubadilisha masharti ya LC na kuipa Richmond Development Company LLC fedha ilizoomba bila kibali cha Benki Kuu ya Tanzania; Je, Richmond ingeleta nchini mitambo kama ilivyokusudiwa au ingekuwa ni hasara kwa Taifa?
Kwa upande mwingine, mchakato mzima wa Richmond Development Company LLC wa kutaka kufanya mabadiliko katika Barua ya Dhamana ya Benki mara kwa mara unadhihirisha nia yao ya kutaka kupata mtaji. Pia inadhihirisha kwamba Richmond Development Company, LLC haikuwa na uwezo wa kifedha wa kutekeleza Mkataba huu kinyume na tamko kwenye Mkataba kuwa:-
"The Supplier (i.e. Richmond) has the equipment and the financial and technical capability to construct, install, commission, operate and maintain such a plant as required by TANESCO". (Msambazaji (yaani Richmond) ana vifaa na uwezo wa kifedha na wa kitaalam kujenga, kusimika, kuiwasha, kuendesha na kuendeleza mtambo huo kama TANESCO inavyohitaji.)
Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo Kamati Teule ilijiuliza maswali yafuatayo:-
(i) Je, utafiti ulifanywa kufahamu gharama halisi za mitambo mipya kutoka kwa watengenezaji wenyewe bila ya kupitia kwa mawakala? Kamati Teule ilibaini kuwa zoezi hilo liliwahi kufanyika mwaka 1998 tu ambapo Wizara ya Nishati na Madini ilitoa kazi hiyo kwa wataalam wa sekta (consultants) na kufanikisha kugundua kuwa bei ya mitambo ya umeme ya IPTL (400 MW) ambayo ilitakiwa kuuzwa kwa Dola za Kimarekani milioni 150 (Tsh. 187.5 bilioni) bei yake halisi ilikuwa ni Dola za Kimarekani milioni 85 (Tsh.106.2 bilioni) tu na hivyo kupata kigezo cha kukataa bei yao. Hivyo basi, kutokana uzoefu huo, Wizara ya Nishati na Madini kwa kushirikiana na TANESCO walitakiwa kufuatilia bei hizo za mitambo na pia makadirio ya kazi za ujenzi ili kupata picha ya gharama halisi ya mradi jambo, ambalo halikufanyika.
Mheshimiwa Spika, kwa viongozi wa Wizara na TANESCO kushindwa kujua bei halisi ya mitambo kutoka kwa watengenezaji wenyewe kwa takribani miaka 10 huku wakisafiri kwenda nje ya nchi kila kukicha kwa mikutano, warsha, makongamano, n.k, na kwa Wizara kung'ang'ania kutumia mawakala badala ya watengenezaji wa mitambo, nchi yetu imegeuzwa gulio la wajanja kuikamua na kuwabebesha wananchi mzigo wa kodi.
Mheshimiwa Spika, Kamati Teule ilipotembelea Marekani, iliamua kuwatembelea baadhi ya watengenezaji wa mitambo ya uzalishaji wa umeme huko huko Houston Marekani kujua bei za mitambo yao. Mmoja wa watengenezaji wenye jina kubwa duniani, Kawasaki Gas Turbines – Americas, anatengeneza na kuuza Mtambo mpya aina ya GPB180 wenye uwezo wa kuzalisha MW 17.5 kwa Dola za Kimarekani 7.5 milioni (Tsh. 9.4 bilioni). Mawakala huwa wanatuletea mitambo ya aina hiyo hiyo kwa bei mara mbili ya bei halisi.
(ii) Iwapo TANESCO au Serikali iliweza kufungua LC ya Dola za Kimarekani 30,696,598; je, fedha hizo zisingeweza kutosheleza kununua mitambo mipya ya uzalishaji umeme, na mitambo hiyo kubakia mali ya TANESCO, badala ya kuingia katika Mikataba ya ghali ya kukodisha mitambo?
Aidha, taarifa za watendaji wa Wizara ya Nishati na Madini kwamba wakati wa kipindi cha mchakato wa zabuni ya umeme wa dharura kulikuwa na ugumu wa kupatikana mitambo ya umeme wa dharura zimethibitishwa na Kamati Teule kuwa sio za kweli.
Mheshimiwa Spika, ni ukweli kwamba kulikuwa na ukame, lakini ukame huo haukuwa wa mitambo ya kuzalisha umeme kwani mitambo hiyo hutengenezwa muda wote na sio kwa kutegemea mvua. Aidha, utafiti wetu umebaini kuwa katika kipindi hicho cha matatizo ya umeme nchini, kampuni zote za kutengeneza mitambo hiyo ya umeme zilikuwa zina mitambo kadhaa ikisubiri wateja. Kawasaki ilikuwa na mitambo 8 ya kisasa tena yenye kutumia gesi na dizeli (dual fuel plant). Serikali nyingi, ikiwemo ya Nigeria, ni wateja wazuri wa kampuni hiyo ambao huteremshiwa bei kwa mtambo moja hadi Dola za Kimarekani milioni 6.7 milioni badala ya Dola za Kimarekani milioni 7.5 bei ya kawaida.
Mheshimiwa Spika, kwa thamani ya LC iliyofunguliwa kwa Richmond Development Company LLC ya Dola za Kimarekani milioni 30.7 au Tsh 38.4 bilioni, TANESCO ingeweza kununua mitambo mipya yote minne pamoja na kumudu kulipia gharama za kusafirisha kwa meli hadi Dar-es-Salaam. Hivyo ili zipatikane MW 105.6 zilizohitajiwa na TANESCO ingehitajika mitambo sita (6) ambayo ni sawa sawa Dola za Kimarekani milioni 45 au Tsh. 56.25 bilioni badala ya Dola za Kimarekani milioni 87 au Tsh. 108.7 bilioni tulizobebeshwa na Richmond Development Company LLC.
Mheshimiwa Spika, Je, si dhahiri kuwa hii ndiyo ilikuwa nia ya Richmond Development Company LLC, yaani kupata fedha za malipo ya awali (advance payment) ili ikatununulie mtambo mmoja na kuja kutukodisha sisi wenyewe, hivyo kufaidika na capacity charge ya kila mwezi kwa Mkataba wa miaka miwili? Kwa mtambo mmoja wa MW 22, capacity charge ni Dola za Kimarekani takriban 730,871 au Tsh. Milioni 913.6 kwa mwezi, hivyo kwa miezi 24 ni wastani wa Dola za Kimarekani 17,540,912 au Tsh. Bilioni 21.9.
(iii) Kwa kuwa thamani ya LC inalipwa kama malipo ya awali (advance payment), Je, hii si sawa na kutoa mkopo kwa Richmond Development Company LLC? Kamati Teule inaona kwamba hiyo ni sawa na kutoa mkopo usio na riba kwa mfanyabiashara wa nje ili awe mwekezaji.
(iv) Kwa nini katika Mkataba wa Richmond Development Company LLC kifungu cha kufidia malipo ya awali (advance payment) ya LC hakikuwekwa bayana ndani ya Mkataba tofauti na Mikataba mingine, badala yake ikawekwa fursa ya kujadiliana na mkandarasi? Kamati Teule haioni sababu yeyote ya msingi mbali na wahusika kujiwekea fursa ya kukidhi maslahi yao binafsi.
0 Comments