[wanabidii] MABADILIKO YA 10 YA KATIBA YA ZANZIBAR YA MWAKA 1984: JE, 'SASA TUNAZO NCHI MBILI'?

Sunday, April 20, 2014

Utangulizi

Nimefurahi kwa sababu huu ni mkusanyiko wa wanazuoni na wasomi wenzangu ambao tumekusanyika hapa kujadili jambo muhimu sana juu ya hatma ya nchi yetu.

Sisemi hivyo kwa sababu huu ni mkusanyiko wa vijana; kwangu mimi ujana na uzee hautegemei umri bali unategemea fikra na mawazo. Kama wewe una fikra za kimaendeleo na ukombozi, basi wewe ni kijana bila kujali umri wako. Na kama umechagua kujiunga na matabaka ya wanyonyaji na wakandamizaji na kusambaza mtazamo wao basi, kwangu, wewe umezeeka hata kama una umri wa miaka 25!

Nakusudia kutumia nafasi hii niliyopewa kujadili mambo mazito na kuelimishana. Kwa hivyo, mhadhara wangu utakuwa wa kuchochea mawazo na fikra mbadala.

Kwa mtazamo wangu, mawazo mbadala maana yake ni mawazo ambayo huwezi kuyakuta kwenye magazeti, kusikia yakisemwa na wasemaji wa kisiasa au kuyakuta kwenye uchambuzi wa wasomi wa mambo ya utawala.

Nchi yetu (na hata bara letu la Afrika, ingawa leo nitazungumzia zaidi nchi yetu) inapitia kwenye kipindi kigumu, kiasi kwamba tuna wasiwasi kwamba nchi hii ya Tanzania itabaki kuwa nchi au itasambaratika. Na mchakato wa Katiba Mpya unadhihirisha hali hiyo na ugumu wa kipindi hiki.

Mjadala unaoendelea juu ya Katiba Mpya umejikita, karibu asilimia mia moja, kwenye suala la muungano, hususan muundo wake. Na hili suala haliepukiki kwa sababu mambo yote mengine katika Rasimu yanategemea sana muundo wa muungano.

Haraka haraka nitoe mifano miwili tu: Ukitaka kujadili malengo makuu ya taifa (Sura ya Pili ya Rasimu), awali ya yote hunabudi ujibu swali: Taifa lipi? Taifa la Tanganyika au la Zanzibar au la Tanzania? Na hili Taifa la Tanzania liko wapi, na lina nafasi gani, katika Rasimu?

Mfano wa pili: Ukitaka kujadili maadili na miiko ya uongozi (Sura ya Tatu), inakubidi ujiulize: Viongozi wepi? Viongozi wa serikali ya muungano, au serikali ya Tanganyika au serikali ya Zanzibar. Ukisoma Rasimu kwa makini, utakuta viongozi wanaomaanishwa ni viongozi wa serikali ya muungano. Kama ni hivyo, maadili haya – mazuri tu – yanawagusa vipi wananchi wa Tanganyika na wananchi wa Zanzibar, wakati viongozi hao wa serikali ya Muungano hawana mamlaka juu ya rasilimali zao, ardhi yao, huduma zao, ustawi wao na, kwa jumla, hali yao halisi ya maisha. Mambo haya yote siyo mambo ya muungano na serikali ya muungano haina mamlaka nayo.

Katika mjadala unaoendelea kumekuwa na malumbano na mabishano kati ya wasemaji, wafuasi na wapigadebe wa ama serikali tatu au serikali mbili. Wachambuzi, kama wapo, ni wachache sana – na hata hao wachache hawasemi au hawasikiki. Rai yangu kwenu ni kwamba sisi kama wanazuoni tusidandie kundi lolote kati ya makundi hayo matatu.

Jukumu na wajibu wetu ni tofauti kabisa. Wajibu wetu ni kuchambua hali halisi bila jazba; na kutokana na uchambuzi wetu kuonesha uzuri na ubaya wa mambo. Sisi wanazuoni nafasi yetu ni kuwa kioo cha jamii, kuonesha jamii uzuri na ubaya wake na kwa vipi na kwa njia gani uzuri unaweza kuimarishwa na ubaya kupunguzwa.

Na huu ndiyo mwongozo wangu katika kufanya uchambuzi wa mabadiliko ya 10 ya Katiba ya Zanzibar. Hoja nyingine juu ya muundo wa muungano, kwa kweli, sitazigusia sana kwa sababu niliwahi kutoa mhadhara juu ya Rasimu ya Kwanza, na Rasimu ya pili haijabadilika sana na vilevile mawazo yangu hayajabadilika sana. Nawashauri wale amabao hawajausoma mhadhara wangu wautafuta kwenye tovuti na wausome.

Na pia, kwa sababu, hivi karibuni imetokea hoja mpya ambayo inarudiwarudiwa sana na wasemaji na wafuasi (pamoja na magazeti) wa serikali tatu. Kwa hivyo, nimeona ni vyema nijikite kwenye hoja hiyo ya mabadiliko ya 10 ya Katiba ya Zanzibar.

HOJA YA KUWA NA NCHI MBILI

Hoja ya mabadiliko ya 10 kuzaa nchi ya Zanzibar na kwa hivyo kuwepo kwa nchi mbili zenye serikali mbili hivi sasa imewekwa vizuri na kwa ufasaha katika Taarifa ya Mwisho ya Tume iliyotoka magazetini tarehe 26 Machi, 2014 (angalia gazeti la Mwananchi la tarehe hiyo, ukurasa wa 37). Kwa hivyo, nitatumia hoja kuu nne za Taarifa hii kufanya uchambuzi wangu. Hoja zilizofafanuliwa katika Taarifa hiyo ya Tume ni hizi zifuatazo:

1.     Zanzibar imetangaza kuwa Nchi

Katika mabadiliko ya 10 Zanzibar "imetamka kwamba ni Nchi tofauti na ilivyokuwa imetamka kwamba ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano kabla ya Mabadiliko hayo."  Kwa mujibu wa Tume hii ni kinyume na Katiba ya Muungano.

2.   Upunguzaji wa Mamlaka ya Bunge la Muungano

Katiba ya Zanzibar imeweka mipaka ya mamlaka ya Bunge la Muungano katika Ibara ya 132 "ambayo inaelekeza kwamba Sheria iliyopitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kabla ya kuanza kutumika Zanzibar ipelekwe kwenye Baraza la Wawakilishi na kupata ridhaa ya kutumika Zanzibar".  Hii pia inatajwa na Tume kuwa ni kinyume na Katiba ya Muungano.

3. Upunguzaji wa Mamlaka ya Rais

Katiba ya Muungano imempa Rais wa Muungano kuigawa Jamhuri katika maeneo ya kiutawala katika mikoa na Wilaya. Mabadiliko ya 10 sasa yameweka mamlaka hayo ya kuligawa eneo la Zanzibar katika Mikoa na Wilaya mikononi mwa Rais wa Zanzibar. Kwa mujibu wa Tume, marekebisho haya yamevunja Katiba ya Muungano.

4. Upunguzaji wa Mamlaka ya Mahakama ya Rufaa

"Katiba ya Muungano ya 1977 imetoa mamlaka ya kusikiliza rufaa nchi nzima. Lakini Zanzibar imezuia mahakama hiyo kusikiliza rufaa kutoka Mahakama za kadhi, kutafsiri Katiba ya Zanzibar na rufaa kuhusu mashauri ya haki za binadamu." Tume inasema kwamba hii pia ni uvunjaji wa Katiba ya Muungano.

Baada ya kuainisha na kufafanua hoja hizo nne, Tume katika Taarifa yake ya mwisho inahitimisha kama ifuatavyo:

Waasisi walituachia Bunge lenye madaraka nchi nzima. Sasa ni lazima lipate idhini ya Baraza la Wawakilishi.

Waasisi waliacha Rais akiwa na madaraka kamili. Madaraka hayo yamepunguzwa bila kufuata utaratibu wa Katiba.

Waasisi walituachia Mahakama ya Rufani yenye madaraka kamili. Madaraka haya yamepunguzwa.

Waasisi waliunganisha nchi mbili ikawa nchi moja. Sasa tunazo nchi mbili. … … ….

Tume iliona ni vigumu kwa Zanzibar kurudi kwa hiyari kwenye hali ya awali, yaani kurudisha mambo yote yaliyotolewa kwenye orodha ya Muungano, kurudisha madaraka ya rais na kufuta kipengere cha nchi mbili kwenye Katiba yake. Tume iliona kwamba pamoja na mambo haya kufanywa kinyume na Katiba ya Muungano hali ibaki hivyo hivyo. Lakini kwa kufanya hivyo basi malalamiko ya Tanzania Bara nayo yasipuuzwe. Hivyo Tume nayo ikapendekeza Serikali ya Tanganyika iundwe.

Ndivyo, kwa hoja hizo, Tume inavyohalalisha pendekezo lake la Serikali tatu. Na bila shaka Tume iliona kwamba hoja hizo ni nzito sana kiasi kwamba ndizo hoja pekee zilizopaswa kufafanuliwa katika Taarifa yao fupi ya mwisho.

Nitakachofanya sasa ni kuangalia hoja moja baada ya nyingine. Tuwe pamoja.

1.     Zanzibar imetangaza kuwa Nchi

Kabla ya kuingia kwenye ibara yenyewe ya Mabadiliko ya 10, kwanza tuelewe dhana ya nchidola na serikali na jinsi ilivyotumika katika katiba zetu.

Nchi maana yake ni eneo la ardhi yenye mipaka ambayo inatambulika; na eneo hilo lina utambulisho wake.

Dola maana yake ni chombo au mamlaka ya utawala ambayo inatawala eneo maalum lenye mipaka yake. Yaani mipaka ya utawala wa dola ni mipaka ya jurisdiction au mamlaka yake.  Vyombo vitatu, yaani chombo cha utendaji (ambacho huitwa serikali), chombo cha utungaji sheria (tunakiita Bunge) na chombo cha kutoa haki (tunakiita Mahakama) ndivyo kwa pamoja vinaunda dola. Mara nyingi sana katika lugha nyepesi tunachanganya dhana ya dola na serikali. Serikali ni chombo kimoja tu katika vyombo vitatu vinavyokamilisha dola.  Ni muhimu sana kutofautisha serikali na dola.

Kwa mfano, huko Zanzibar kabla ya kuundwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa, CCM ndicho kilikuwa chama tawala. Kwa hivyo, tunasema ilikuwa serikali ya CCM, lakini dola ni ya Zanzibar. Kama, kwa mfano, CUF wangeshika madaraka, serikali ingekuwa serikali ya CUF, lakini dola ingebaki kuwa dola ya Zanzibar.

Sasa mara nyingi katika msamiati wa kawaida maneno serikali na dola yanachanganywa. Ili kujua tafsiri yake sahihi hatunabudi tuangalie maneno haya katika muktadha (context) wake.

Sasa tuangalie mabadiliko ya 10 yanasemaje: Nukuu ya ibara ya 1:

Zanzibar ni Nchi ambayo eneo la mipaka yake ni eneo lote la Visiwa vya Unguja na Pemba pamoja na Visiwa vidogo vilivyoizunguka na bahari yake ambayo kabla ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ikiitwa Jamhuri ya watu wa Zanzibar.

Neno linalotatiza hapa ni "nchi". Lakini tujiulize, neno hili 'nchi' linamaanisha dhana ipi? Hoja yangu ni kwamba neno 'nchi' katika muktadha wa Katiba linamaanisha dhana ya DOLA na ndivyo lilivyotumika katika Katiba ya Zanzibar pamoja na Katiba ya Muungano. Nitathibitisha:

Angalia ibara ya 9(1) ya Katiba ya Zanzibar. Ibara hiyo inasema"Zanzibar ni nchi ya kidemokrasia na haki za kijamii". Maneno hayo hayo yametumika katika Katiba ya Muungano. Angalia Ibara ya 8(1): "Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni Nchi inayofuata misingi ya demokrasia na haki ya kijamii …". Tafsiri yake rasmi ya kiingereza ni, nitanukuu tafsiri ya 1998: "The United Republic of Tanzania is a state which adheres to the principles of democracy and social justice ….". Katika hili hakuna shaka kwamba neno NCHI limetumika kumaanisha dhana ya dola, ambayo ni sahihi kabisa.

Hata Katiba ya Muungano inatambua dola ya Zanzibar (pamoja na dola ya muungano). Ninukuu ibara ya 4:

4 (1) Shughuli zote za Mamlaka ya Nchi katika Jamhuri ya Muungano zitatekelezwa na kudhibitiwa na vyombo viwili vyenye mamlaka ya utendaji, vyombo viwili vyenye mamlaka ya kutekeleza utoaji haki, na pia vyombo viwili vyenye mamlaka ya kutunga sheria na kusimamia utekelezaji wa shughuli za umma.

Na ibara ndogo (2) inaainisha vyombo hivyo. Nanukuu:

4 (2). Vyombo vyenye mamlaka ya utendaji vitakuwa ni serikali ya Jamhuri ya muungano na serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar; vyombo vyenye mamlaka ya kutekeleza utoaji haki vitakuwa ni Mahakama ya serikali ya Jamhuri ya Muungano na Mahakama ya serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, na vyombo vyenye mamlaka ya kutunga sheria na kusimamia utekelezaji wa shughuli za umma vitakuwa ni Bunge na Baraza la Wawakilishi.

Sasa ukijumlisha vyombo viwili viwili unapata dola ya Muungano na dola ya Zanzibar.

Kwa hivyo, kama Katiba ya Zanzibar imetambua na kufafanua kwamba Zanzibar ni dola, kosa liko wapi? Kwa nini, jambo hilo linakuzwa mpaka kudai kwamba Zanzibar imetangaza kuwa nchi?

Kama kweli mabadiliko ya 10 yaliitangaza Zanzibar kama Nchi kwa maana ya "country", basi Zanzibar wangeuandikia Umoja wa Mataifa (UN) kwamba kwa mujibu wa Katiba yao Zanzibar ni Jamhuri ('sovereign republic') yenye hadhi na malaka ya kidola ndani ya jumuiya ya kimataifa ('international personality'). Hii haijafanyika. Katika ngazi ya kimataifa kuna 'sovereign republic' moja tu nayo ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Bila shaka, kwa mambo ya ndani mamlaka ya Jamhuri ya Muungano yamegawanyika kati ya dola ya Muungano na dola ya Zanzibar (divided sovereignty). Na ndivyo inavyotokea katika muungano na shirikisho.

  1. Kama kweli, Zanzibar ni nchi yenye madaraka kamili tangu 2010, kwa mujibu wa tafsiri ya Taarifa ya ufafanuzi ya Tume, kwa nini baadhi ya Wazanzibari wanadai mamlaka kamili wakati tayari wanayo tangu 2010?
  2. Kama kweli, neno nchi maana yake siyo dola, basi, tujiulize Rasimu ya Katiba katika pendekezo lake la muundo wa serikali tatu limependekeza nchi tatu? Yaani Nchi ya Tanganyika, Nchi ya Zanzibar na Nchi ya Tanzania? Na hii nchi ya Tanzania ni ipi? Ni nchi hewa!

Ni wazi, na inathibitishwa na Rasimu yenyewe, kilichopendekezwa ni nchi moja yenye dola tatu: dola ya Jamhuri ya Muungano, dola ya Tanganyika na dola ya Zanzibar. Sasa ugumu wa kukubali kuwa Zanzibar ni dola uko wapi?

Ni kweli, kama Tume inavyosema katika Taarifa yake fupi ya mwisho, kwamba kabla ya mabadiliko haya, Katiba ya Zanzibar ilisema kwamba "Zanzibar ni sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania". Kwa nini basi Wazanzibari waliamua kutoa ufafanuzi 2010? Ninavyohisi mimi ni kwamba kwa kweli Wazanzibari walikuwa wamechoshwa na wanasiasa, wasomi na hata mahakama [angalia Hukumu ya Mahakama ya Rufaa iliyoandikwa na Jaji Ramadhani katika kesi ya S. M. Z. v. Machano Khamis Ali & 17 Others,] kutokutambua Zanzibar kama dola. Pigo la mwisho lilikuwa mwaka 2008 wakati Mhe. Waziri Mkuu aliposema kwamba Zanzibar siyo Nchi. Kauli hii ya Waziri Mkuu ilileta mabishano na malumbano makali ambayo hatimaye yalitulizwa na Rais Kikwete katika hotuba yake Bungeni. Itafuteni hotuba hiyo ya Rais muisome. Nionavyo mimi, hii ndiyo sababu iliyowafanya Wazanzibari waweke wazi kwamba Zanzibar ni nchi kwa maana ya dola.

2.     Upunguzaji wa Mamlaka ya Bunge la Muungano.

Hii inahusu Ibara ya 132 ya Katiba ya Zanzibar. Kwanza, ibara hii haikuongezwa wakati wa mabadiliko ya 10. Imekuwa katika Katiba ya Zanzibar tangu 1984, wakati muasisi mmojawapo wa Muungano (Mwalimu Nyerere) akiwa madarakani. Na Rasimu ya Katiba hii iliridhiwa na CCM. Nukuu ya ibara yenyewe ni hii:

132(1) Hakuna Sheria yoyote itakayopitishwa na Bunge la Muungano ambayo itatumika Zanzibar mpaka Sheria hiyo iwe ni kwa ajili ya mambo ya Muungano tu na ipitishwe kulingana na maelekezo yaliyo chini ya vifungu vya Katiba ya Jamhuri ya Muungano.

(2) Sheria kama hiyo lazima ipelekwe mbele ya Baraza la Wawakilishi na Waziri anayehusika.

Ibara hii inaweka masharti matatu ili sheria iliyopitishwa na Bunge la Muungano  itumike Zanzibar.

a)      Iwe kwa ajili ya mambo ya Muungano. Hii haina ubishi kwa sababu ndivyo Ibara ya Katiba ya Muungano (ib. 64) inavyoelekeza.

b)      Iwe imepitishwa kulingana na maelekezo ya vifungu vya Katiba ya Muungano. Hii pia haina ubishi.

c)      Ipelekwe mbele ya Baraza la Wawakilishi. Kinachozungumzwa hapa na sheria hiyo ni kuwa sheria husika iwe tabled katika Baraza la Wawakilishi kwa taarifa.

Hii haina madhara yoyote. Ni kawaida kabisa kwa nyaraka mbalimbali (kwa mfano sheria ndogondogo zinazopitishwa na serikali za mitaa au Taarifa za Mashirika ya Umma) hupelekwa mbele ya Bunge kwa taarifa. Lakini hii haina maana kwamba Bunge linaidhinisha au linaridhia nyaraka hizo.

Kwa bahati mbaya, Taarifa ya Tume imeongeza sharti lingine jipya la kupata idhini ya Baraza la Wawakilishi ambalo halimo kabisa katika ibara ya 132.

Ili kuthibitisha hoja yake kwamba sheria kama hizo zinahitaji idhini ya Baraza la Wawakilishi, Tume inanukuu mifano miwili. Moja ni Sheria ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (Commission for Human Rights and Good Governance Act) na nyingine ni ya Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu (Deep Sea Fishing Authority Act) ambazo zilirudishwa na zilitakiwa ziridhiwe na Baraza la Wawakilishi.  Lakini hii ilikuwa ni sahihi kabisa kwa sababu sheria zote hizo mbili hazikuwa juu ya mambo ya Muungano – haki za binadamu au uvuvi siyo mambo ya Muungano.

Ukweli ni kwamba ni Bunge la Muungano ndilo lilivuka mipaka ya mamlaka yake kwa kupitisha sheria juu ya mambo yasiyo ya muungano na kutaka zitumike Zanzibar.

3.     Upunguzaji wa Mamlaka ya Rais

Jambo hili linahusu madaraka ya rais kuigawa Jamhuri katika maeneo ya utawala, yaani Mikoa na Wilaya. Ni kweli kwamba ibara ya 2 ya Katiba ya Muungano imeweka mamlaka haya mikononi mwa Rais wa Jamhuri lakini Rais wa Muungano anapogawa Zanzibar katika mikoa na wilaya anatakiwa kushauriana na Rais wa Zanzibar.  Ni kweli pia kwamba, mabadiliko ya 10 yameweka mamlaka haya mikononi mwa Rais wa Zanzibar.

Labda tuchambue jambo hili kwa kina kabla hatujafikia hitimisho.

  1. Mambo ya utawala wa mikoa na wilaya, kwa jumla serikali za mitaa, siyo ya Muungano. Kwa hivyo, ni kosa kutoa mamlaka haya kwa Rais wa Jamhuri.
  2. Katiba ya Zanzibar ya 1979 (ambayo ilikuwa Katiba ya kwanza ya Zanzibar baada ya mapinduzi) katika ibara yake ya 2(2) inasema, nainukuu:

Kwa ajili ya utekelezaji bora wa shughuli za Serikali, Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Rais wa Zanzibar aweza kuigawa Zanzibar katika Mikoa, Wilaya na maeneo mengineyo kwa kufuata utaratibu au kukubaliwa na Chama cha Mapinduzi.

Rasimu ya Katiba ya 1979 iliidhinishwa na Kamati Kuu ya CCM.

Kwa hivyo, kilichofanyika katika mabadiliko ya 10 ni kurudisha mamlaka haya mikononi mwa Rais wa Zanzibar. Hii ni sahihi. Kwa hivyo, kama kuna Katiba inayotakiwa kurekebishwa, basi ni Katiba ya Muungano na siyo Katiba ya Zanzibar.

4. Upunguzaji wa Mamlaka ya Mahakama ya Rufaa

Ni kweli kwamba Mahakama ya Rufaa ni jambo la Muungano, ingawa uamuzi wa kuongezwa kwake katika orodha ya mambo ya Muungano una utatanishi. Ni kweli pia kwamba Katiba ya Zanzibar imeweka mipaka ya mamlaka yake, kwa mfano, kesi kutoka Mahakama za Kadhi, kesi kuhusu tafsiri ya Katiba ya Zanzibar na kesi kuhusu haki za binadamu haziwezi kwenda Mahakama ya Rufaa. Kwa hivyo, kuna mgongano kati ya Katiba ya Zanzibar na Katiba ya Muungano. Hata hivyo, Mahakama zetu, pamoja na Mahakama ya Rufaa yenyewe, wamekwepa kutolea maamuzi jambo hili, wamewaachia wanasiasa kufanya marekebisho.

Mgongano huo ungeepukika pale ambapo Mahakama ya Rufaa ya Afrika Mashiriki ilipovunjika na pia kama kungekuwa na mashauriano zaidi na Wazanzibari jinsi ya kuunda Mahakama ya Rufaa ya Muungano na mamlaka yake. Hata hivyo, kwangu mie jambo hilo siyo kubwa na wala halipaswi kukuzwa. Linarekebishika bila shida. Na mgongano huo haujawahi kuhatarisha uhai wa Muungano.

Mwisho, ningependa kutoa tahadhari. Hoja za Tume zinajaribu moja kwa moja kuwalaumu Wazanzibari kwamba ni wakosaji yaani wamevunja Katiba ya Jamhuri ya Muungano. Siyo sahihi kuwatupia lawana Wazanzibari. Ningependa kutoa mfano mmoja ambao uzito wake unapita hoja hizo zote zilizofafanuliwa na Tume. Na mfano huu utadhihirisha kwamba kuna kasoro kubwa mno katika Katiba ya Muungano.

Ibara ya 64 ya Katiba ya Muungano inasema kwamba Mamlaka ya Kutunga sheria juu ya mambo ya Muungano yamo mikononi mwa Bunge la Muungano na mamlaka ya kutunga sheria za Zanzibar juu ya mambo yasiyo ya muungano ni ya Baraza la Wawakilishi. Hii ni sawa kabisa na inaendana na mfumo wa "serikali mbili", au kwa usahihi zaidi, dola mbili, zilizowekwa na Hati ya Muungano mnamo mwaka 1964 na katika Katiba ya Muungano ya 1977.

Lakini ibara ndogo ya 64(4) inasema: [nitanukuu maneno yanayohusika]

Sheria yoyote iliyotungwa na Bunge kuhusu jambo lolote haitatumika Tanzania Zanzibar ila kwa mujibu wa masharti yafuatayo –

a) Sheria hiyo iwe imetamka wazi kwamba itatumika Tanzania Bara na vilevile Tanzania Zanzibar ….; au

(b)               ……

(c)     Sheria hiyo iwe inahusu Mambo ya Muungano, …

Maana ya ibara hii ni kwamba Bunge la Muungano linaweza kutunga sheria juu ya mambo yoyote yale hata kama siyo mambo ya Muungano na yakatumika Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar ilimradi sheria hiyo iwe imesema tu kwamba yatatumika Tanzania Bara na Zanzibar. Hii, kwa kweli, inamaanisha kwamba Bunge la Muungano limepokonya mamlaka ya Baraza la Wawakilishi na kwa hivyo kuvuruga kabisa muundo wa dola mbili.  Ibara hii iliwekwa katika mabadiliko ya Katiba ya Muungano ya 1984 baada ya machafuko ya hali ya hewa ya kiasiasa wakati Mheshimiwa Warioba akiwa Waziri wa Sheria [Ilitakiwa kuwekwa neno 'na' badala ya 'au']. Mbaya zaidi, ibara hii imetumika kupitisha zaidi ya sheria 40 juu ya mambo yasiyo ya muungano na kutumika Zanzibar mpaka Wazanzibari walipoamka na kupinga sheria zile mbili ambazo tumekwisha zizungumzia.

Ibara hii moja kwa moja inaathiri muundo uliowekwa na Hati ya Muungano. Kwa hivyo, tunapowalaumu Wazanzibari kwa kuvunja Katiba lazima pia tuangalie upande mwingine wa sarafu. Na tukifanya hivyo tutaweza kusawazisha mambo haya yote katika Katiba mpya, badala ya kuyatumia kuhalalisha muundo wa serikali tatu ambao ni wazi kabisa kwamba utauvunja Muungano.

***

Sasa nije kwenye hitimisho la Tume. Kama nilivyoonesha, hoja tatu kati ya nne za ufafanuzi wa hoja kuu ya Tume siyo sahihi. Na hoja ya Mahakama ya Rufaa siyo nzito. Kwa vyovyote vile, hoja hii ya mwisho haituruhusu kabisa kuhitimisha kwa kusema kwamba waasisi waliziunganisha nchi mbili zikawa moja na sasa tunazo nchi mbili zenye serikali mbili. Kutokana na uchambuzi wangu ambao ninauwasilisha kwenu, hitimisho langu ni kwamba waasisi walidhamiria kuwa na Muungano wa nchi moja yenye dola mbili na mpaka sasa tuna nchi moja yenye dola mbili. Ni kweli muundo wa Muungano tuliyonao una matatizo lakini haya yanaweza kutatuliwa bila kuhatarisha uhai wa Muungano.

Hoja ya Tume kwamba ni vigumu kwa "Zanzibar kurudi kwa hiyari kwenye hali ya awali" na ndiyo maana wamependekeza Serikali ya Tanganyika haina mashiko na inagongana yenyewe. Kwanza, kama nilivyoeleza kwamba siyo sahihi kusema kwamba Zanzibar imejitangaza kuwa ni nchi huru kwa maana ya nchi. Pili, hata kama hii ingekuwa kweli, au kuna migongano kati ya Katiba hizi mbili, basi lilikuwa ni lengo la mchakato huu wa Katiba Mpya kusawazisha na kuondoa migongano hii. Isitoshe, pendekezo lenyewe la Tume halitambui Zanzibar kuwa nchi na Tanganyika kuwa nchi, bali linaweka dola tatu katika nchi moja badala ya dola mbili katika nchi moja kama ilivyo chini ya Katiba ya 1977.  Na hatunabudi, sisi ambao tunadai kuwa wataalam wa sheria za Katiba kuwaeleza wananchi wote kwamba ikiwa Katiba Mpya (ya aina yoyote ile) itapita kwa kura ya maoni ya wananchi wa pande zote mbili, basi sheria na Katiba ya sasa ya Zanzibar hazinabudi zirekebishwe au hata kuandikwa upya ili kuendana na Katiba Mpya ya Muungano. Kwa kuwa itakuwa ni mara ya kwanza kwa katiba ya Muungano kupitishwa kwa kura ya maoni, hakuna haja ya yeyote, pamoja na wanasiasa wa pande zote mbili, kung'ang'ania katiba yao ya sasa. Kisheria na kikatiba, Hati ya Muungano pamoja na Katiba ya Zanzibar ya 1984 hazitakuwa na nguvu za kisheria; zitakuwa, kama tunavyosema, 'superceded'. Muungano utakuwa umewekwa kwenye misingi imara ya kikatiba ambayo chimbuko lake ni wananchi wenyewe wa pande zote mbili.

HITIMISHO

Katika kuhitimisha mada yangu juu ya hoja hizi zinazojikita kwenye mabadiliko ya 10 ya Katiba ya Zanzibar, ningependa kutoa tahadhari kama ifuatavyo:

  1. Bila kukusudia, hoja hii kama ilivyoandikwa katika Taarifa ya mwisho ya Tume inaweza kuwa hatarishi. Nasema hivyo kwa sababu, moja, inaamsha na kuhamasisha hisia za Utanganyika, na, pili, inawafanya watu wa Tanzania Bara wawachukie wenzao wa Zanzibar.  Kwa hivyo, inadhoofisha muungano badala ya kuuimarisha. Na muungano wowote hauwezi kudumu, au kudumu kwa amani, kama hauna mizizi katika watu na hisia zao.Mimi binafsi sina shaka na nia ya wazee wa Tume. Naamini kabisa kwamba wazee hawa walikuwa na nia njema tu. Lakini kama usemi wa kizungu unavyosema: The road to hell is paved with good intentions kwa maana kwamba 'Njia ya jehanam imetandikwa na nia njema.'
  2. Juu ya hilo la Utanganyika, ningependa kuongeza maneno machache hasa kwa faida ya vijana wetu. Nimeshangaa kidogo kwamba hata mzee na mwanazuoni mwenzangu Prof. Mpangala ametumia msamiati wa 'Utaifa wa Tanganyika' bila kudadisi kihistoria 'Utaifa wa Tanganyika'.Kwa muhtasari tu, kabla ya vita vya kwanza, hatukuwa na Tanganyika. Tulikuwa na 'German East Africa' ambayo eneo lake lilijumuisha Burundi, Rwanda na eneo hilo la 'Tanganyika' chini ya himaya ya ubeberu wa Wajerumani. Baada ya Ujerumani kushindwa katika vita, Rwanda na Burundi ziligawiwa kwa Ubelgiji na Tanganyika kwa Uingereza. Waingereza ndipo wakaunda neno hili 'Tanganyika' na iliitwa 'Tanganyika Territory', yaani, bustani ya wakoloni, siyo taifa.Mababu zetu waliopigania uhuru walijikita kwenye dhana ya Utaifa wa Kiafrika, kama alivyoeleza vizuri tu Profesa Mpangala. Vyama vya wananchi, kutoka TAA (Tanganyika African Association) mpaka TANU (Tanganyika African National Union), viliweka msisitizo kwenye 'African', Uafrika wao. Iliwabidi kuweka neno Tanganyika kwa sababu tu ndilo lililokuwa eneo la utawala wa wakoloni.Tulipopata uhuru mnamo Desemba 1961, hatukuwa taifa kwa sababu mkuu wa nchi bado alikuwa Malkia. Mwezi wa Novemba 1962 ndipo tukawa Jamhuri ya Tanganyika wakati Mwalimu alipochaguliwa kuwa Rais. Na Mwalimu tangu mwanzo alisistiza kwamba sisi hatukuwa taifa bali mkusanyiko wa makabila na lilikuwa jukumu la serikali huru kujenga utaifa (nation-building). Lakini Mwalimu hakupata muda wa kutosha kujenga utaifa wa Tanganyika kwa sababu mwezi Aprili 1964, yaani baada ya miezi 14 tu, tukaungana na Zanzibar kuwa Tanzania.  Na kwa takriban nusu karne tumekuwa tunajenga Utaifa wa Tanzania. Sasa hii dhana ya Utaifa wa Tanganyika, au Utanganyika, unatoka wapi? Na mantiki na historia yake ni ipi?Ningependa kujua hapa tulipo ni vijana wangapi kati yenu mlizaliwa kama Watanganyika. Nyoosheni mikono juu. Nyinyi wote mlizaliwa mkiwa Watanzania, utaifa wenu ni Utanzania; utambulisho wenu ni Utanzania; mnajitambua kama Watanzania na mnatambuliwa na wengine kama Watanzania.Ukweli ni kwamba mking'ang'ania Utanganyika wenu, ambao wala hamjui kama mtakuwa mnavunja taifa, mtakuwa mnatumikia maslahi na matakwa ya mabeberu na wanasiasa wachache wenye uchu wa madaraka. Na Utanganyika wenu hautadumu kwa sababu mtaanza kudai sasa Jamhuri ya Makonde na Jamhuri ya Sukuma! Mtakuwa vipande vipande. Hivi siyo vitisho; kuna mifano hai mbele yetu. Somalia imesambaratika, Libya pia, Sudan, Afrika ya Kati, na nchi nyingine nje ya Afrika – Afghanistan, Pakistan, Syria, Iraq bila kutaja nchi za Ulaya.
  3. Kuna suala la Utaifa wa Zanzibar. Ukweli wa kihistoria ni kwamba Wazanzibari angalau wanaweza kuzungumzia utambulisho wao kwa sababu Zanzibar ina umri wa zaidi ya karne mbili. Na katika muungano wetu utambulisho wao ulipewa kipaumbele kuondoa hisia za kumezwa na kupoteza utambulisho wao kutokana na hali halisi ya watu wachache, nchi ndogo n.k. Na Zanzibar kupewa hadhi maalum (special dispensation) siyo jambo geni hata kidogo. Popote pale panapokuwa na muungano wa nchi ambazo hazilingani kutakuwa na hadhi maalum kwa nchi ndogo (special dispensation).

    Mie sina shaka kwamba kama tungefanikiwa kuunda Shirikisho la Afrika Mashariki, Zanzibar ingeomba na ingepewa hadhi maalum (special dispensation). Ushahidi wa hili upo. Kwa sasa sina muda wa kutosha wa kufafanua zaidi.
  4. Mwisho, narudia tu nilichosema katika mhadhara wangu juu ya Rasimu ya Kwanza ya Katiba. Rasimu hii ya Katiba ina matatizo mengi. Kwa kweli Muungano hauwezi kudumu ikiwa Rasimu hii itapitishwa na Bunge Maalum kama ilivyo. Shirikisho lolote lile ambalo lina serikali ya shirikisho dhaifu, bila vyanzo vya uhakika vya mapato, bila udhibiti madhubuti wa rasilimali, bila kuwa na mamlaka juu ya sera za uchumi, fedha, forodha na masoko ya nje, na bila kuwa na mamlaka juu ya ukusanyaji kodi, hauwezi kujiendesha.
  5. Pamoja na hayo, mimi sisemi kwamba muundo wa serikali au dola mbili tulionao sasa hauna matatizo. Unayo. Lakini tusiangalie muungano kwa jicho la idadi ya serikali. Tuuangalie kwa mtazamo wa demokrasia. Na tukifanya hivyo tunaweza kubuni muundo ambao utakidhi mahitaji yetu bila kuhatarisha uhai wa muungano.
  6. Mie mwenyewe nimewahi kupendekeza mfumo mbadala lakini sina muda wa kutosha kuelezea mfumo huo. Hata hivyo, nikipata nafasi nyingine mwafaka nitajaribu kufanya hivyo.
  7. Nawashukuru sana kwa kunisikiliza.



[1] Mada hii iliwasilishwa kwenye Kongamano la Vijana kutoka kwenye Taasisi za Elimu ya Juu lilofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 30 Machi 2014 kwa ajili ya Madhimisho ya Miaka 50 ya Muungano. Kongamano hilo liliandaliwa na Wizara ya Habari,  Utamaduni, Vijana  na Michezo


--
Send Emails to wanabidii@googlegroups.com
 
Kujiondoa Tuma Email kwenda
wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com Utapata Email ya kudhibitisha ukishatuma
 
Disclaimer:
Everyone posting to this Forum bears the sole responsibility for any legal consequences of his or her postings, and hence statements and facts must be presented responsibly. Your continued membership signifies that you agree to this disclaimer and pledge to abide by our Rules and Guidelines.
---
You received this message because you are subscribed to the Google Groups "Wanabidii" group.
To unsubscribe from this group and stop receiving emails from it, send an email to wanabidii+unsubscribe@googlegroups.com.
For more options, visit https://groups.google.com/d/optout.

Share this :

Related Posts

0 Comments